WANAOPEWA MISAMAHA YA KODI SASA KUTANGAZWA



Katika mwaka wa fedha 2014/15 Serikali itakuwa inatangaza watu wanaonufaika na misamaha ya kodi.
Lengo la hatua hiyo ni kuongeza haki na usawa katika kutoa misamaha hiyo.
Kauli hiyo imetolewa na Waziri wa Fedha, Saada Mkuya Salum kwenye Hotuba yake ya Bajeti ya Serikali kwa mwaka 2014/15.
“Sambamba na kupunguza misamaha ya kodi na kuongeza haki na usawa katika kutoa misamaha, kuanzia mwaka 2014/15 serikali itachukua hatua kuu mbili muhimu”, alisema.
Saada alisema hatua ya  kwanza itakayochukuliwa ni Serikali itakuwa inatoa taarifa ya misamaha ya kodi kila robo mwaka, kwa kuwatangaza walionufaika  na misamaha kwenye tovuti ya Wizara ya Fedha.
Taarifa hiyo itajumuisha majina ya watu, taasisi, asasi na kampuni zilizonufaika  na misamaha ya kodi, thamani na sheria iliyotumika kutoa misamaha hiyo.
Alieleza kuwa zoezi hilo, litahusisha  taarifa ya misamaha ya kodi
ya kuanzia mwaka 2010 na kuendelea.
“Hatua hii itasaidia kuleta uwazi na uwajibikaji katika suala la misamaha ya kodi na kuwafanya wananchi wajue ni nani anayenufaika na misamaha hiyo,” alisema.
Alisema, hatua ya pili itakayochukuliwa ni kutoa taarifa ya kina ya misamaha yote ya kodi iliyotolewa na kuiwasilisha bungeni kila mwaka ili wabunge wapate nafasi ya kujadili na kutoa maoni yao.

No comments: