MAADHIMISHO SIKU YA MTOTO WA AFRIKA KUFANYIKA JUMATATU



Maadhimisho ya mwaka huu ya Siku ya Mtoto wa Afrika, yataadhimishwa nchini Jumatatu Juni 16, mwaka huu katika ngazi ya mkoa. 
Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto, Sophia Simba alisema hayo mjini hapa jana kwenye mkutano wake na waandishi wa habari.
“Maadhimisho ya mwaka huu ya Siku ya Mtoto wa Afrika, yataadhimishwa katika ngazi ya Mkoa, ambapo kila mkoa utaadhimisha siku hii kwa kushirikisha halmashauri za wilaya, manispaa, miji, kata, vijiji, mashirika na taasisi mbalimbali zilizoko katika mkoa husika na watu binafsi,” alisema Waziri Simba.
Simba alisema hatua ya kufanya sherehe hizo katika ngazi ya Mkoa, itaipa mikoa nafasi nzuri ya kutafakari matatizo yanayolikabili kundi hili la watoto, ikiwa ni pamoja na kuwapatia haki zao za msingi.
“Mikoa itapata pia nafasi ya kufikiria kuweka miradi endelevu kwa ajili ya watoto hawa,” alisema. 
Alisema maadhimisho ya kila mwaka, huwa na kaulimbiu yake na kwamba kaulimbiu ya mwaka huu ni: “Kupata Elimu Bora na Isiyo na Vikwazo; Ni Haki ya Kila Mtoto”.
Alisema kaulimbiu hiyo, inalenga kukumbusha wazazi, walezi, serikali na jamii kuhusu umuhimu wa kumuendeleza mtoto bila kumbagua, kulingana na rangi, jinsi na hali aliyokuwa nayo.
Simba alisema tarehe 16 Juni ya kila mwaka ni kilele cha maadhimisho ya Siku ya Mtoto wa Afrika. Siku hiyo huadhimishwa na nchi zote wanachama wa Umoja wa Afrika (AU), kukumbuka mauaji ya watoto wa shule, yaliyofanyika katika kitongoji cha Soweto nchini Afrika Kusini tarehe 16 Juni 1976. 
Katika tukio hilo la kusikitisha, inakadiriwa kuwa watoto wapatao 2,000 waliuawa kikatili na serikali ya makaburu.

No comments: