MENEJA RAIA WA KIGENI TANZANITE ONE ATIWA MBARONI



Meneja Mauzo wa Kampuni ya madini ya Tanzanite One yenye makao yake Makuu jijini Arusha, Jacques Beytel (39) raia wa Afrika ya Kusini amekamatwa na maofisa wa Idara ya Uhamiaji mkoani Arusha kwa kosa la kufanya kazi nchini bila ya kuwa na kibali. 
Kukamatwa kwa raia huyo wa Afrika ya Kusini aliyekuwa akifanya kazi ya mauzo katika Ofisi Kuu za Tanzanite One zilizopo barabara ya India jijini Arusha tangu mwaka 2008 zimethibitishwa na Ofisa Mkuu wa Uhamiaji Mkoa wa Arusha,Daniel Namomba. 
Namomba alikiri kukamatwa kwa Beytel alipofuatwa ofisini kwake kuzungumzia tukio hilo na alisema kuwa mtuhumiwa alikamatwa Juni 11 mwaka huu ofisini kwake bado anashikiliwa na maofisa wake kwani mahojiano bado hayajakamilika. 
‘’Tunamshikilia Beytel ambaye ni raia wa Afrika ya Kusini kwa kosa la kufanya kazi nchini bila ya kuwa na kibali na anahojiwa na maofisa wake,mahojiano yakikamilika itawapa taarifa na hiyo inaweza kuwa wiki ijayo,’’ alisema Namomba 
Kwa mujibu wa habari kutoka ndani ya Kampuni ya Tanzanite One zinasema kuwa Beytel aliwahi kufukuzwa kazi mwanzoni mwa mwaka 2008 akituhumiwa kwa wizi wa madini kurudishwa kwao kwa kosa hilo. 
Habari ziliendelea kusema kuwa haikueleweka meneja huyo alirudishwaje kazini tena kwa wadhifa huo huo, wakati alifukuzwa kazi kwa tuhuma za wizi.
Meneja Uhusiano wa Kampuni ya Tanzanite One ambaye pia ni Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa kampuni hiyo kwa sasa, Doto Mwidadi alikiri kukamatwa kwa meneja huyo.
Mwidadi alisema vibali vya kufanya kazi vya raia wa Afrika ya Kusini wanaofanya kazi Tanzanite One hutolewa Uhamiaji makao makuu hivyo wamewasiliana na viongozi wa Uhamiaji makao makuu ili waweze kuvituma Arusha.

No comments: