MUSWADA WA SHERIA YA BAJETI WAJA



Serikali inaandaa Muswada wa Sheria ya Bajeti, ambao utakamilika kabla ya mwisho wa mwaka 2014/15.
Waziri wa Fedha, Saada Salum Mkuya  alisema hayo aliposoma hotuba ya Bajeti ya Serikali kwa mwaka 2014/15.
“Bajeti hii imelenga pia kuimarisha zaidi usimamizi na udhibiti wa matumizi ya fedha za umma. Ili kutekeleza azma hii, serikali inaandaa Muswada wa Sheria ya Bajeti,” alisema.
Saada alisema Sheria hiyo inalenga kuongeza nidhamu ya matumizi na uwajibikaji kwa wadau wote, wanaotekeleza Bajeti ya Serikali.
Alitaja wadau hao kuwa ni viongozi na maofisa wa serikali, wabunge, mashirika ya umma, wakala na taasisi za serikali, makandarasi na wazabuni.
Alisema katika kuandaa muswada huo, wadau muhimu,  ikiwemo wabunge watashirikishwa kupitia kamati za kudumu za Bunge.
Aidha, alisema katika mwaka 2014/15, Sh bilioni 8.7 zimetengwa kwa ajili ya ujenzi na ukarabati wa hospitali tisa za mikoa nchini. 
Mikoa hiyo ni Katavi, Simiyu, Njombe, Geita, Arusha, Pwani, Kilimanjaro, Singida na Tabora.

No comments: