KINONDONI YATOA SHILINGI MILIONI 54 KUJENGA BARABARA ZA KATI 27



Halmashauri ya Manispaa ya Kinondoni imetoa Sh milioni 54 kwa kata zake zote 27 zilizopo katika manispaa hiyo, kuhakikisha barabara za mitaa zinajengwa kwa kiwango cha lami nyepesi na kifusi.
Ofisa Mahusiano wa Manispaa ya Kinondoni, Sebastian Muhowera aliliambia gazeti hili juzi Dar es Salaam kuwa licha ya kusubiri fedha walizoziomba kutoka serikalini kurekebisha barabara zilizoharibiwa na mvua, kila kata inaendelea na ujenzi wa barabara hizo. Kila kata itapata Sh milioni mbili kwa ajili ya ukarabati huo.
Alisema kazi hiyo wameziachia kila Serikali za mitaa kwani wao wanajua barabara zao na kwamba Manispaa yenyewe itahusika na barabara kuu na matengenezo madogo ambayo yanagharimu Sh bilioni 8.4.
Alisema kata husika zinatambua mgawanyo wa fedha hiyo na sasa wanatoa ratiba ya maendeleo ya ujenzi katika barabara zote zilizopo katika kata hizo.
Pia, alisema wameandaa tingatinga ambalo litatumiwa na kata endapo watahitaji kutoka manispaa kwa ajili ya uchongaji wa barabara na kushindilia kifusi, kwa kuwa wanataka barabara zote ziwe na kifusi cha moramu na sio udongo.
"Katika mwaka huu wa fedha unaoanza Julai mwaka huu, tumejipanga kuhakikisha kila barabara iliyopo katika manispaa yetu inakuwa katika kiwango cha lami nyepesi au kifusi,’’alisema Muhowera.
Aliongeza kuwa kiasi walichotoa kwa kata ni kutokana na asilimia 20 ya mapato yanayokusanywa na serikali za mitaa yanabaki katika akiba yao. Alisema mapato hayo yanatokana na leseni za sheria za barabara.
Aidha, katika kufanikisha bajeti ya mwaka 2014/15 Manispaa imeweka mpango wa kudumu kujenga barabara ya lami na kituo cha daladala kuepusha wanaoegesha katika hifadhi za barabara.
Alisema ifikapo Julai mwaka huu wataanza ujenzi wa barabara na kituo cha daladala maeneo ya Goba, Bunju, Mabwepande na kuongeza kuwa watahakikisha barabara hizo zinatumika kwa muda mrefu.
"Tumeunda kitengo kinachohusika na ujenzi wa barabara ambao watasimamia na kukagua barabara zote za kata na barabara kuu kuhakikisha kazi inafanyika kwa usahihi," aliongeza.

No comments: