Mahakama
Kuu Kanda ya Dar es Salaam imetupilia mbali kesi ya kikatiba iliyokuwa
inamkabili Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, kwa kuwa waliofungua kesi hiyo hawana
haki kisheria.
Kesi
hiyo namba 24 ya mwaka jana ilifunguliwa na Kituo cha Msaada wa Kisheria na
Haki za Binadamu (LHRC) kwa kushirikiana na Chama cha Wanasheria Tanganyika
(TLS) dhidi ya Waziri Mkuu Pinda na Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG).
Katika
madai yao LHRC na TLS walidai, Pinda alivunja Katiba kutokana na kauli
aliyoitoa bungeni Juni 20, 2013, wakidai ni amri kwa vyombo vya utekelezaji wa
sheria ya kuwapiga wananchi wakati wa vurugu.
Akisoma
uamuzi wa pingamizi la awali lililowasilishwa na Pinda na AG, Jaji Kiongozi Fakhi
Jundu, alisema waliofungua kesi hiyo hawana haki kisheria kwa sababu madhara
ambayo yangetokana na kauli hiyo yangekuwa kwa wananchi na siyo mashirika.
Alisema
walalamikaji wangeweza kufungua kesi endapo kauli hiyo ingekuwa inaathiri
mashirika, lakini kauli iliyotolewa inaweza kumuathiri mtu mmoja pia wamefungua
kesi kwa niaba ya watu wengine wakati
kilichotakiwa ni mtu aliyeathirika na kauli husika ndiye awasilishe ombi au
kufungua kesi.
Katika
pingamizi lao pamoja na hoja nyingine, walidai kesi hiyo imefunguliwa isivyo
halali kwa kuwa inakiuka Katiba na Sheria ya Mamlaka, Kinga na Haki za Wabunge,
ya mwaka 1988 kwa kuwa Waziri Mkuu analindwa na Katiba Ibara ya 100 (1) na (2).
Jaji
Jundu alisema kwa upande wa haki na upendeleo wa wabunge mahakama haina mamlaka
ya kuhoji jambo lolote, lakini kuhusu kinga mahakama ina uwezo wa kusikiliza
kwa kuwa kinga yao ina mipaka hivyo mbunge anaweza kukamatwa na kushitakiwa kwa
kufuata taratibu za kisheria.
Aliongeza kwa mujibu wa kanuni ya 71 (1)C ya Bunge, bila kuathiri ibara ya 100, mtu
yeyote ambaye ataona ameathirika na hoja au kauli iliyotolewa bungeni na mbunge
anaweza kupeleka malalamiko yake kwa Spika wa Bunge na mtu huyo awe raia wa
Tanzania.
Katika
uamuzi huo ulioandikwa na majaji watatu, Jaji Jundu alisema kwa mujibu wa ibara
ya 100 (1) wabunge wana uhuru wa kujadili jambo lolote bila kuhojiwa, lakini
ibara ya 100(2) kinga ya wabunge ina mipaka na mtu binafsi anaweza kuhoji
endapo kauli iliyotolewa inaweza kumuathiri.
Akizungumza
nje ya Mahakama, Wakili Harold Sungusia alisema wiki ijayo jopo la mawakili
waliofungua kesi hiyo litakutana na kujadili hatua watakazochukua.
No comments:
Post a Comment