Wiki moja baada ya moto kuteketeza
soko la Mchikichini, wafanyabiashara wa soko hilo waliopoteza mali zao
wameorodheshwa majina yao ili kusaidiwa ikiwemo orodha hiyo kupelekwa kwenye
taasisi za fedha kuomba wafanyabiashara hao waongezewe muda wa makato ya mikopo
waliochukua.
Akizungumza na mwandishi jana,
Mwenyekiti wa Wafanyabiashara wa Mitumba sokoni hapo, Hajali Mohamed alisema
kuwa moto huo umeteketeza mali za wauza mitumba 3,800.
Alisema kutokana na hali hiyo,
uongozi wa soko hilo ukishirikiana na Serikali ya Mtaa Mchikichini umeanzisha
utaratibu wa kuandika barua zinazowatambulisha wafanyabiashara waliopoteza mali
zao ambazo zinapelekwa kwenye taasisi mbalimbali za fedha walizokopa.
Alisema kuwa moto umeathiri mitaji
ya wafanyabiashara mbalimbali na ambao hawana uwezo wa kurejesha mikopo kwa
wakati kama wanavyotakiwa na taasisi husika za fedha walizokopa, hivyo barua
hizo maalumu walizopewa zinawatambulisha kwenye taasisi hizo kuwa ni waathirika
wa moto huo.
"Uandikishaji huu umeanza leo
(jana) na kesho (leo) suala hili litamalizika na kisha kujua ni wafanyabiashara
wangapi wamepewa barua za kuwatambulisha kwenye taasisi za fedha kwa ajili ya
kusaidiwa kwenye urejeshwaji wa mikopo," alisema Mohamed.
Aliongeza kuwa pia Kamati ya Maafa
ya Mkoa imewataka wafanyabiashara hao kuorodhesha mali za wafanyabiashara hao
zilizopotea ifikapo kesho.
"Naipongeza kamati hiyo kwa
hatua ambayo inaonekana kuwa ni nzuri na itakuja kuwa yenye mafaniko pengine
kwa baadaye manake mali zilizoteketea hapa ni nyingi na sijui kama itawezekana
kwa kila mfanyabiashara kujigharimia mwenyewe katika kuimarisha mtaji
wake," alisema Mohamed.
Mwandishi alifanya ufuatiliaji wa
hali inavyoendelea sasa sokoni hapo na kuona wafanyabiashara mbalimbali
wakijengea mabanda yao huku wengine wakiwa wameanza kufanya biashara zao kama
kawaida.
Sehemu kubwa ya maeneo yaliyokuwa
yameungua yameanza kujengwa upya ambapo wajenzi wamekutwa wakijenga mabanda na
kuweka mabati.
No comments:
Post a Comment