Viongozi
pamoja na wafanyabiashara kutoka jimbo la Katanga katika Jamhuri ya
Kidemokrasia ya Kongo (DRC) wamewasili nchini kwa ziara inayolenga kuimarisha
uhusiano wa kibiashara kati ya nchi hiyo na Tanzania.
Ujumbe
huo wa watu 16 unaongozwa na Naibu Gavana wa jimbo hilo, Yav Guilbert na Waziri
wa Uchukuzi wa jimbo hilo, Kahozi Sumba.
Akizungumza
na waandishi wa habari baada ya kupokea ujumbe huo jijini Dar es Salaam juzi,
Waziri wa Uchukuzi, Dk Harrison Mwakyembe alisema, “Tunataka kumaliza
mazungumzo tuliyoaanza ili kuimarisha uhusiano wetu”.
Mwanzoni
mwa mwezi uliopita, Tanzania ilifungua ofisi ndogo ya mawasiliano ya Mamlaka ya
Bandari (TPA) mjini Lubumbashi nchini DRC katika jimbo hilo la Katanga.
Ofisi
hiyo inalenga kurahisisha na kuleta ufanisi katika kusafirisha mizigo ya
wafanyabiashara wa DRC wanaotumia bandari ya Dar es Salaam.
Inalenga
pia kusaidia wafanyabiashara wa nchi hiyo kumaliza matatizo yao Lubumbashi
badala ya kusafiri hadi Dar es Salaam.
Mienendo ya taarifa za mizigo itafanyika mjini
humo na hivyo kuharakisha taratibu za mizigo bandarini Dar es Salaam.
Waziri
Mwakyembe alisafiri kwa barabara kutoka Dar es Salaam hadi Lubumbashi kupitia
Zambia kwa zaidi ya kilometa 2000 kuangalia na kupata taarifa za changamoto
wanazokumbana nazo wafanyabiashara wa DRC kuanzia bandarini Dar es Salaam.
Kwa
upande wake, Gavana Guilbert, alishukuru serikali ya Tanzania kwa mapokezi
mazuri waliyopata. “Tunashukuru sana kwa mapokezi…tunajisikia nyumbani,”
alisema.
Katika ziara yao, ujumbe huo ulitarajiwa kutembelea maeneo mbalimbali yakiwemo bandari
pamoja na kuzungumza na maofisa wa serikali ya Tanzania.
Taarifa
za Mamlaka ya Bandari Tanzania (TPA), zinaonesha mizigo ya DRC imekuwa
ikiongezeka kwa asilimia takribani 24 kwa mwaka tangu mwaka 2004 ikiongezeka
kutoka tani 155,611 hadi tani 1,117,249 mwaka 2013.
DRC
ni ya pili kwa kupitisha mizigo mingi katika bandari ya Dar es Salaam. Kwa mujibu wa takwimu zilizopo, mizigo ya DRC
inachukua asilimia 25 ya mizigo yote ya nchi jirani inayopita katika bandari
hiyo.
No comments:
Post a Comment