UMATI YATOA BAISKELI 40 KWA WAHUDUMU WA AFYA RUFIJI



Chama cha Uzazi na Malezi Bora Tanzania (UMATI) kimekabidhi  baiskeli  40 zenye thamani ya sh milioni 4.8 wahudumu wa afya ya uzazi na ujinsia ngazi ya jamii waliopo katika Kata za Chumbi 'A' na Bungu zilizopo wilayani Rufiji, Mkoa wa Pwani.
Akizungumza wilayani hapa mwishoni mwa wiki, Mkurugenzi Mtendaji wa UMATI, Lulu Ng'wanakilala katika hotuba yake iliyosomwa na Meneja Miradi wa UMATI, Tausi Hassan alisema lengo la kukabidhi baiskeli hizo ni kuunga mkono juhudi za Serikali za kuboresha afya ya mama na mtoto .
Ng'wanakilala alisema UMATI kupitia ufadhili washirika la MERCK Sharp and Dohme (MSD) kutoka nchini Marekani liliweza kupata mradi wa uwiano katika ubunifu wa kuboresha Afya ya Mama na Mtoto, mradi unaotekelezwa katika kwa kipindi cha miaka mitatu katika mikoa ya Pwani na Katavi na kushirikiana kwa karibu zaidi na Ofisi za Mganga Mkuu wa Wilaya.
Kwa upande wake Kaimu Mganga Mkuu wa Wilaya ya Rufiji, Rasmo Msabaha alisema Mkoa huo umepanga kufikia asilimia 60 ya malengo iliyojiwekea katika kuzuia vifo vya Mama na Mtoto na hadi kufikia sasa umefikia asilimia 37, na hivyo jitihada za pamoja hazina budi kufanywa katika kufikia kiasi kilichobaki.
"Uzazi wa Mpango ni muhimu sana, hapo zamani Serikali iliweza kutoa bure huduma za afya na elimu, lakini kwa sasa idadi ya wananchi imekuwa kubwa na ndio maana Serikali imeamua kushirikiana na sekta binafsi ikiwemo UMATI ilikuweza kusaidia huduma za afya, hivyo ni lazima tuzae kwa mpangilio na kwa kadri tunavyoweza kuwahudumia" alisema.
Naye Diwani wa Kata ya Bungu, Ramadhani Mkwaya alisema Ofisi yake imeupokea kwa moyo mmoja mradi huo na ipo tayari kuutekeleza, na akaishukuru UMATI kuichagua Kata yake kati ya Kata 27 zilizopokatika Wilaya hiyo na kusema kuwa hicho nikielelezo kuwa Kata hiyo inakubalika kimaendeleo.
Aidha Diwani wa Kata ya Chumbi, Ramadhani Mikole aliwataka wahudumu hao wa afya ya uzazi ngazi ya jamii kutokuwa kimya iwapo kutatokea tatizo la kiutendaji katika majukumu yao,na badala yake wawasiliane mara moja na wahusika wa mradi ili kuhakikisha kuwa mradi unafikia malengo yake.

No comments: