Asasi ya kiraia ya SIKIKA imewataka
wabunge kuishawishi Serikali kuongeza bajeti ya Wizara ya Afya na Ustawi wa
Jamii, kwa lengo la kukabiliana na tatizo la ukosefu wa dawa muhimu na vifaa
tiba katika vituo mbalimbali vya afya nchini.
Akizungumza na waandishi mbalimbali wa
habari jijini Dar es Salaam jana, Mkurugenzi wa Sikika Irene Kiria, alisema
hatua hiyo itasaidia kutatua tatizo hilo la dawa kwani wabunge walio wengi
wanalalamikia tatizo hilo.
Ombi la Sikika kwa wabunge hao
limetolewa wakati Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii ikitarajia kuwasilisha makadirio ya mapato na matumizi
yake wiki hii huku kilio kikubwa cha asasi
hiyo, kikilenga kuhamasisha upatikanaji wa huduma bora za afya kwa wananchi.
Alisema tathmini mbalimbali zinaonesha
kuwa, upatikanaji wa dawa muhimu na
vifaa tiba katika vituo vya huduma za afya za umma ni mdogo; hivyo kusababisha
wananchi wengi kulazimika kutafuta dawa hizo kutoka katika maduka ya kawaida.
"Kwa mfano utafiti uliofanywa na
Sikika mwaka 2012 umeonesha kuwa asilimia 52 ya hospitali hazikuwa na dawa
muhimu na vifaa tiba kwa zaidi ya wiki nne na moja ya sababu kuu za kukosekana
kwa dawa muhimu na vifaa tiba ni bajeti ndogo inayotengwa na Serikali,"
alisema Kiria.
Alisema ingawa mojawapo ya vipaumbele
vya Wizara ya afya ni kuboresha upatikanaji wa
dawa muhimu, mgao wa fedha kwa ajili ya ununuzi wa dawa muhimu na vifaa
tiba umekuwa hauendani mahitaji yake na hivyo kutosaidia tatizo linalojitokeza.
"Kwa mujibu wa makadirio ya Wizara
ya afya zinahitajika kiasi cha Sh bilioni 250 kukidhi mahitaji ya dawa muhimu
kwa mwaka 2014/2015, hata hivyo mgao unaotarajiwa kupangwa ni Sh bilioni 45
sawa na asilimia 7.7 ya mahitaji yote," aliongeza Kiria.
Pia alisema pamoja na kipaumbele cha
Wizara hiyo kupunguza vifo vya akinamama na watoto vitokanavyo na kujifungua,
bajeti ya vifaa vya kujifungulia inapungua mwaka hadi mwaka na hivyo kuondoa
matumaini ya kupunguza vifo hivyo kwa wananchi.
No comments:
Post a Comment