TRENI YA KWENDA BARA KUANZA SAFARI LEO


Huduma ya usafiri wa treni ya abiria  kuelekea bara zinaanza rasmi leo, huku, Kampuni  ya Reli ya Tanzania (TRL) ikiwahakikishia wananchi kutokuwa na hofu juu ya usafiri huo. 
Usafiri huo ulisitishwa Januari 10, mwaka huu  baada ya kuharibika kwa miundombinu ya reli kutokana na mvua kubwa zilizokuwa zikinyesha. 
Meneja Mkuu wa Masoko wa TRL, Charles Ndenge alisema hayo  Dar  es Salaam jana. 
“Takribani miezi mitano imepita tangu kusitishwa kwa huduma hiyo, uamuzi wa kuanza kutoa tena huduma leo unatokana na kukamilika kwa kazi ya ukarabati wa reli  eneo la kati ya stesheni za Kilosa mkoani Morogoro na Gulwe mkoani Dodoma,” alisema . 
Aidha alisema  licha ya TRL kutangaza kuanza upya kwa huduma hiyo na kuwataka wasafiri kukata tiketi kuanzia Mei 22,  mwitikio umekuwa wa wastani katika baadhi ya vituo. 
Alifafanua zaidi kuwa  katika safari zitakazoanza leo, mizigo inayozidi uzito wa kawaida itafanyiwa utaratibu wa kusajiliwa mapema ili kuweza kusafirishwa katika behewa la breki siku moja kabla ya safari husika.
Meneja Mkuu wa Usafirishaji, Rowland Simtengu alisema kampuni hiyo imejiandaa vya kutosha kukidhi matakwa ya huduma na haitarajiwi kuwepo kwa usumbufu wa aina yoyote wala vitendea kazi. 

Kuhusu siku za safari alisema zimebakia kama zilivyo; Mara mbili ambapo kwa treni ya kutoka Dar es Salaam kwenda Kigoma na Mwanza ni Jumanne na Ijumaa wakati zinazotoka Kigoma na Mwanza kwenda  Dar es Salaam ni Alhamisi na Jumapili.

No comments: