Ile
hali ya kufanya kazi kwa mazoea iliyojengeka kwa baadhi ya watendaji wa
Serikali jana iliwatokea puani watendaji wa Manispaa ya Dodoma wakati Waziri
Mkuu alipoamua kufanya ziara kukagua miradi ya maendeleo.
Akiwa
katika eneo la kwanza ambalo alipangiwa kukagua ujenzi wa Kituo cha Afya cha
Mkonze, Waziri Mkuu alipokea taarifa ya ujenzi wa kituo na kubaini kuwa
hawajafanya chochote ili kutekeleza maagizo yake aliyoyatoa Machi 22, 2014.
Katika
taarifa yake, Kaimu Mkurugenzi wa Manispaa ya Dodoma, Mhandisi Lusako Kilembe
alimweleza Waziri Mkuu kwamba walifanya tathmini ya ujenzi wa kituo hicho na
kubaini kuwa zinahitajika Sh milioni 24.15 na kwamba maombi ya matumizi hayo
yamepangwa kujadiliwa kwenye kikao cha kamati ya fedha na uongozi kitakachofanyika
Juni 10, mwaka huu.
Akiwa
katika maadhimisho ya kilele cha Wiki ya Maji ambayo Kitaifa yalifanyika mkoani
Dodoma, Waziri Mkuu alizindua mradi wa maji jirani na Kituo hicho cha Afya cha
Mkonze na kubaini kuwa kuna hitilafu za ujenzi wakati alipokagua kituo. Ndipo
akaagiza ufanyike ukarabati na yeye akaahidi kuja kukagua ukarabati huo mwezi
huu.
Mara
baada ya kusomewa taarifa ya mradi, Waziri Mkuu akahoji ni kwa nini hawajafanya
chochote tangu alipotoa maelekezo Machi, mwaka huu. Hakupata jibu la kueleweka
kutoka kwa viongozi wa wilaya na mkoa.
Waziri
Mkuu alisalimia wananchi waliokuwepo kwenye eneo hilo na kuwaeleza kwamba
hawezi kukagua kituo hicho ilhali hakuna kilichotekelezwa tangu afike hapo
Machi mwaka huu.
Alisema
haiwezekani yeye atoe maagizo katika kipindi chote hicho halafu kisifanyike
kitu chochote. Akaondoka na kuendelea na ziara hadi Kijiji cha Manzase ambako
alikagua mradi wa kisima cha maji.
Mapema,
katika taarifa yake, Mhandisi Kilembe alisema kituo hicho cha afya kilijengwa
chini ya ufadhili wa ubalozi katika makubaliano yaliyofikiwa Novemba 11, 2009
kwamba ungetoa dola za Marekani 84,307 sawa na Sh milioni 152.86.
Hata
hivyo, mara baada ya ujenzi kukamilika Agosti 29, 2012, kituo hicho kilipata
nyufa nyingi hali iliyosababisha kifungwe na wananchi walitoa malalamiko yao
kwa Waziri Mkuu Machi mwaka huu wakati alipokwenda kuzindua mradi wa maji
kwenye Kijiji cha Mkonze jirani na kituo hicho.
Akiwa
katika Kijiji cha Manzase Waziri Mkuu aliridhishwa na ujenzi wa mradi wa maji
kwa ajili ya wakazi 9,000 wa eneo ambapo alielezwa kwamba utakamilika Julai 16,
2014.
No comments:
Post a Comment