MWEKEZAJI AAGIZWA KULIPA SHILINGI MILIONI 700 ANAZODAIWA NA WAKULIMA



Naibu Waziri wa Kilimo Chakula na Ushirika, Godfrey Zambi amemtaka mmiliki wa kiwanda cha mvinyo cha CETAWICO kilichopo Dodoma kuhakikisha analipa deni lote la wakulima wa zabibu lipatalo Sh milioni 700 kabla ya mwisho wa mwezi huu.
Wakulima hao kutoka Kijiji cha Hombolo waliitaka Serikali kuwasimamia ili waweze kulipwa madai yao ya zaidi ya Sh milioni 700 wanazomdai mwekezaji wa kiwanda cha Cetawico.
Madai hayo yalithibitishwa na Mhasibu wa kiwanda cha Cetawico Jacson Temu ambaye alimwambia Naibu huyo kwamba kiwanda hicho kinadaiwa kiasi cha Sh milioni 703.
Naibu Waziri Zambi amesema kwamba kama muda huo utapita na mwekezaji huyo hajawalipa wakulima, Serikali itamchukulia hatua kali.
Katibu wa Ushirika wa Wakulima wa Zabibu na Masoko Hombolo Ramadan Mkombozi alisema wakulima wanamdai mwekezaji wa kiwanda hicho cha Cetawico Dk Florenzo Chesini, raia wa Italia fedha hizo kwa zaidi ya miezi 9.
Alisema pamoja na jitihada mbalimbali walizofanya zikiwemo kushirikisha Serikali ya Wilaya na Mkoa ili madeni yao yalipwe hawajafanikiwa kutokana na kutopewa ushirikiano na badala yake kuishia kupewa majibu yasiyoridhisha.
‘’Mheshimiwa Naibu Waziri kwa kuwa umekuja tunaweza kupata madai yetu lakini huyu mwekezaji hii siyo mara yake ya kwanza kutotulipa hata mwaka jana msimu wa mwezi wa pili ilibidi Waziri Chiza aingilie kati ndiyo tukalipwa, japo si malipo yote,“ alisema na kuongeza kwamba pamoja na kukosa ushirikiano pia bei yenyewe si nzuri na hupanga bei yeye.
Alisema akipelekewa zabibu huwa zinapimwa zinaachwa kiwandani na kisha anajipangia bei. Alisema wakati wa kiangazi analipa kilo moja Sh 800 au 1000  na wakati wa masika 500 au 400 bila kujali gharama za uendeshaji hali inayowapa hasara kubwa wakulima.

No comments: