Mwanaume mmoja aliyejulikana kwa
jina la Cosmas Njiliwi (45) mkazi wa Kijiji cha Msikisi, Kata ya Namatutwe
Halmashauri ya Wilaya Masasi mkoani Mtwara, amejinyonga kwa
kutumia shuka yake kwa kile kilichoelezwa kuwa ni wivu wa
mapenzi.
Akithibitisha kutokea kwa tukio hilo
Ofisa Mtendaji Kata ya Namatutwe, Salumu Mapunda alisema kuwa
tukio hilo limetokea usiku wa kuamkia juzi katika Kijiji cha
Msikisi umbali wa mita 15 kutoka nyumbani kwa marehemu alikokuwa akiishi na
familia yake.
Alisema kwamba kwa siku za hivi
karibuni Njiliwi hakuwa na mahusiano mazuri na mke wake mara baada ya kuhisi
kuwa kuna mwanamume ana mahusiano ya kimapenzi na mkewe.
Kwa mujibu wa Ofisa Mtendaji huyo
alisema kuwa baada ya kugundua hilo Njiliwi aliamua kumpa talaka mke wake
lakini katika hali isiyokuwa ya kawaida mama huyo alikataa kuondoka nyumbani
hapo kwa madai kwamba hawezi kuishi peke yake bila ya mume wake.
Mtendaji huyo aliendelea kueleza
kuwa maisha yaliendelea kuwa magumu yasiyokuwa na maelewano kati ya wanandoa
hao na ndipo siku ya tukio Njiliwi aliondoka asubuhi nyumbani hapo huku
akiwaaga watoto wake ingawa hakuweka wazi ni wapi anaelekea na lini
atarudi.
Mapunda alisema baada ya Njiliwi
kuondoka nyumbani hapo watoto wake walianza kuingiwa na hofu kwani hata
ilipofika jioni hawakumuona nyumbani na ndipo walipoamua kutoa taarifa kwa babu
yao pamoja na majirani ambao pia walikiri kutomuona.
Alisema kuwa wakati jitihada za
kumtafuta zinaendelea mke wake aliona mtu akiwa nyuma ya nyumba yao akiwa
ananing'inia kwenye mti wa mkorosho na aliposogea kwa karibu
alibaini kuwa ni mume wake amejinyonga ndipo alipotoa taarifa Ofisi ya
Mtendaji Kata ili kuja kuuteremsha mwili wa mume wake juu ya mti.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mtwara
Zelothe Steven amethibitisha kutokea kwa tukio na kueleza kuwa wanandoa wanapaswa
kuishi kwa amani ili kudumisha ndoa na kuweza kulea familia zao kwa pamoja bila
mifarakano yoyote ambayo huvunja amani ndani ya nyumba.
No comments:
Post a Comment