MSAKO WA VITA DHIDI YA UJANGILI SASA ANGANI NA ARDHINI...



Ahadi za wadau wa uhifadhi na vita dhidi ya ujangili nchini wameanza kutimiza ahadi zao baada ya jana kukabidhi helikopta ya kisasa itakayotumika katika kazi hiyo maalumu kwa ajili ya Pori la Akiba la Selous.
Helikopta hiyo aina ya Robertson R44 yenye thamani ya dola za Kimarekani 500,000 (sh milioni 800), ni moja ya ahadi za Howard Buffett, mtoto wa bilionea wa Marekani anayeshika nafasi ya tatu kwa utajiri duniani, Warren Buffet mwenye utajiri wa dola za Kimarekani bilioni 64.8 (sh trilioni 105).
Howard, akiwa nchini miezi ya hivi karibuni alikutana na Rais Jakaya Kikwete Ikulu, Dar es Salaam na kuahidi kuchangia helikopta katika kukabilia na ujangili hususan wa tembo kwa kile alichosema ameguswa na kazi nzuri inayofanywa na Serikali ya Tanzania katika kukabili ujangili. 
Mbali ya helikopta hiyo, Buffet pia anakusudia kusaidia vifaa vyenye thamani ya dola za Kimarekani milioni 5 (sh bilioni 8) katika kuimarisha ulinzi dhidi ya wanyamapori na uhifadhi kwa ujumla.
Na jana, Balozi wa Marekani Mark Childress alikabidhi helikopta hiyo yenye uwezo wa kubeba watu wanne kwa Waziri wa Maliasili na Utalii, Lazaro Nyalandu. Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Mazingira, James Lembeli na Waziri Kivuli wa Wizara ya Maliasili, Mchungajui Peter Msigwa pia walihudhuria hafla ya makabidhiano hayo kwenye Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Dar es Salaam.
Balozi Childress alisema vita dhidi ya ujangili inahitaji vifaa na teknolojia ya kisasa, akisema helikopta ni sehemu ya kampeni katika mapambano hayo. Ujangili dhidi ya tembo umesababisha vifo 20,000 katika muongo mmoja, asilimia 80 kati yavifo hivyo vikitokea katika nchi za Afrika Mashariki.
Akipokea helikopta hiyo, Nyalandu aliishukuru Serikali ya Marekani  na juhudi za wahisani,  kwa kuunga mkono juhudi za serikali ya Tanzania katika vita dhidi ya ujangili, huku akisema serikali itaongeza helikopta nyingine mbili kwa ajili ya kupambana na majangili.
Alisema moja itakuwa aina ya Bell 206 na nyingine Robertson 44 zitanunuliwa ili kuimarisha ulinzi dhidi ya majangili katika Hifadhi ya Taifa ya Ngorongoro na nyingine zenye matukio yanayohusiana na ujangili.
Naye Lembeli alielezea kufurahishwa kwake na juhudi za serikali za kuonesha kwa vitendo mikakati ya kukomesha ujangili nchini, huku akitaka wanaobeza kazi nzuri ya serikali wapuuzwe.
“Jamani, kazi nzuri inafanywa na Nyalandu na wizara yake na serikali kwa ujumla, badala ya kuwakatisha tamaa na kuingiza siasa, tuwaunguze mkono ili kulinda rasilimali hizi za taifa kama lilivyokuwa lengo la mwasisi wa taifa hili, Hayati baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere…,” alisema.
Kwa upande wa Mchungaji Msigwa, alisema anashukuru kuona kelele nyingine wanazopiga kwa lengo la kuisukuma serikali kufanya kazi zinafanyiwa kazi, na sehemu ya matunda hayo ya kupatikana kwa helikopta ya kusaidia vita dhidi ya ujangili.
Alisema kwa kazi nzuri inayofanywa na serikali, atashangaa kusikia watu wakibeza hatua zinachukuliwa kukabili ujangili, huku akisisitiza kuwa, watakuwa sawa na wendawazimu kwani dhamira ya Watanzania wengi ni kuona inapatikana tiba ya kudumu dhidi ya mauaji ya wanyama kama tembo.
Rubani wa helikopta hiyo, Peter Achammer alisema chombo chake ni imara na kinaweza kuwa hewani kwa saa tatu na kusafiri kwa kasi ya kilomita 240 kwa saa.
Ofisa wanyamapori kutoka kikosi cha ujangili Kanda ya Mashariki na Pwani inayohusisha mikoa ya Dar es Salaam, Tanga, Lindi, Mtwara and Morogoro,  Dickson Machumu alisema helikopta hiyo itaongeza ufanisi katika majukumu, huku ofisa mwingine katika kikosi hicho, Mariam Haji akisema itasaidia katika mambo mengi, ikiwa pamoja na kuwawahisha hospitali wapiganaji inapotokea wamejeruhiwa katika mapambano na majangili.

No comments: