WABUNGE WANOGESHA MIAKA 25 YA UASKOFU WA NGALALEKUMTWA



Spika wa Bunge la Tanzania, Anne Makinda ameongoza wananchi wa Mkoa wa Iringa waishio Dar es Salaam kwenye harambee ya kuchangia Jubilee ya Miaka 25 ya Askofu Tarcisius Ngalalekumtwa wa Jimbo Kuu Iringa.
Katika harambee hiyo iliyofanyika Dar es Salaam jana, jumla ya Sh milioni 20.2 zilipatikana zikiwa ni ahadi na fedha taslimu ambazo zitajumuishwa ili kusaidia maendeleo jimboni Iringa. 
Akiongoza harambee hiyo, Makinda alisema ni jambo la furaha kwa watu kuona umuhimu wa kusaidia kazi za maendeleo ya wananchi na kusema maendeleo ya watu huletwa na watu wenyewe ikiwa watashirikiana.
Alisema kwa kuona umuhimu wa harambee hiyo ya Jubilee ya Miaka 25 ya uaskofu wa Ngalalekumtwa ambaye pia anatimiza miaka 40 ya upadri, yeye na wabunge wa Njombe na Iringa wametoa Sh milioni 10 kusaidia maendeleo Jimbo la Iringa.
"Mimi na wabunge wenzangu wa Iringa na Njombe tumeona jambo hili ni jema na kwa umoja wetu tumechangia Sh milioni 10," alisema Makinda.
Naye Mwakilishi wa Askofu wa Iringa jijini Dar es Salaam, Padri Luciano Mpoma alisema harambee hiyo itasaidia kuboresha mahitaji ya maendeleo anayoyafanya Askofu  Ngalalekumtwa jimboni Iringa.
Askofu Ngalalekumtwa, pamoja na kuwa askofu wa Jimbo la Iringa, pia ni Rais wa Baraza la Maaskofu wa Katoliki Tanzania.  Alipata daraja la upadri mwaka 1973 nchini Italia na mwaka 1988 aliteuliwa na Baba Mtakatifu Yohane Paul wa pili kuwa Askofu Mwandamizi wa Jimbo la Sumbawanga. 
Hata hivyo, mwaka 1992 alihamishwa na Baba Mtakatifu, Papa John Paul kuwa askofu wa Iringa nafasi aliyonayo hadi leo anapotimiza miaka 25 ya uaskofu na 40 ya upadri.

No comments: