MTOTO AFARIKI DUNIA BAADA YA KUTUMBUKIA KISIMANI



Mtoto Jeremiah Nyamuhanga (2) mkazi wa Machimbo amekufa baada ya kutumbukia kwenye kisima cha maji karibu na nyumbani kwao.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Ilala, Marietha Minangi alisema, mtoto huyo alitumbukia juzi saa 10 jioni katika eneo la Machimbo, Kitunda, Wilaya ya Ilala.
Alisema maiti yake ilikutwa ikielea ndani ya kisima hicho kilicho karibu na nyumba yao. Inasadikiwa mtoto huyo alimtoroka baba yake aliyekuwa kwenye banda la kuku na kwenda kucheza ambapo alitumbukia ndani ya kisima hicho.
Maiti ya mtoto huyo amehifadhiwa katika Hospitali ya Taifa Muhimbili na upelelezi unaendelea.
Katika tukio jingine, abiria wa pikipiki ambaye bado hajafahamika amekufa baada ya pikipiki aliyokuwa amepanda kugonga lori kwa nyuma.
Kamanda Minangi alisema ajali hiyo ni ya juzi saa 5 asubuhi katika Barabara ya Pugu eneo la Mombasa.
Alisema pikipiki aina ya Lingken yenye namba T116 CTF iliyokuwa ikiendeshwa na mtu asiyefahamika akitoka Mombasa kwenda Gongo la Mboto, akiwa amempakia abiria asiyefahamika mwanamke anayekadiriwa kuwa na umri kati ya miaka 40 na 45 aligonga kwa nyuma lori aina ya Scania lenye namba T743 lililokuwa likiendeshwa na Charles Yusuph (35).
Katika ajali hiyo ambapo wote walikuwa katika uelekeo mmoja, abiria huyo alikufa papo hapo na maiti imehifadhiwa Hospitali ya Taifa Muhimbili na jitihada za kumtafuta dereva wa pikipiki aliyekimbia baada ya ajali zinaendelea, huku pikipiki ikiwa imehifadhiwa Kituo cha Polisi Stakishari.

No comments: