MSAKO WA POLISI, INTERPOL WANASA WATU 247



Watu 247 wametiwa mbaroni kutokana na makosa mbalimbali baada ya kunaswa katika Operesheni Usalama Namba Moja iliyofanywa na jeshi la polisi nchini kwa kushirikiana na Polisi wa Kimataifa (INTERPOL) katika mikoa mbalimbali.
Hayo yalisemwa jana na Mkurugenzi wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai (DCI), Issaya Mngulu wakati akizungumza na waandishi wa habari Jijini Dar es Salaam.
Alisema  operesheni tajwa imetokana na maamuzi yaliyofikiwa kwenye mkutano wa wakuu wa majeshi wa kanda zote mbili na kisha kuwekewa mpango mkakati  wa utekelezaji kwenye kikao  kilichowakutanisha wakuu wa upelelezi.
Aliongeza kuwa operesheni hii imekuwa na mafanikio makubwa kwa sababu pamoja na kukamatwa vitu mbalimbali pia wametuma ujumbe kwa wahalifu kuwa jeshi letu lipo imara kuhakikisha maisha na mali za watu ziko salama.
Alisema katika operesheni hiyo jumla ya wahamiaji haramu 84 walikamatwa ambao saba ni kutoka Kongo na 77 kutoka Burundi, na pia walifanikiwa kukamata madawa ya kulevya heroin gramu 5, bangi gramu 8, misokoto 195 na mirungi kilo 200.
Pia kwa upande wa wizi wa magari jumla ya magari 18 yalikamatwa, kati ya magari hayo 11 yaligunduliwa kuingiliwa chasis na injini namba, magari manne na pikipiki tatu yaligunduliwa kutoka nchi tofauti kama Afrika Kusini, Japan na Burundi.
Aliongeza kuwa pia walifanikiwa kukamata silaha haramu  pisto moja, gobori 1 na risasi 3.
Aidha alitoa mwito kwa wananchi  kuwa jeshi hilo litaendelea kufanya misako ya mara kwa mara ili kupunguza uhalifu nchini na pia aliwataka wananchi waendelee kutoa ushirikiano wao katika harakati za kupambana na uhalifu wa aina yeyote hapa nchini.

No comments: