MAMA SALMA KIKWETE AFAGILIWA MKOANI LINDI



Uongozi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) mkoani Lindi, umempongeza Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa (MNEC) anayewakilisha wilaya ya Lindi Mjini, Mama Salma Kikwete kutokana na kazi nzuri anazofanya katika kutimiza majukumu yake.
Pongezi hizo zilitolewa kwa mara ya kwanza na Katibu wa CCM wa Mkoa wa Lindi, Adelina Geffi alipokuwa akisoma taarifa ya kazi, uhai na Utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya Chama hicho kinachotawala ya mwaka 2010/2015 kwa Mwenyekiti wa Taifa wa Jumuiya ya Wazazi, Abdallah Bulembo aliyekuwa katika ziara ya siku sita mkoani hapa.
Katika taarifa yake hiyo, Geffi alisema kuwa Mama Salma amenunua gari la kubeba wagonjwa na kulikabidhi Hospitali ya Rufaa ya Mkoa huo kama mchango wake binafsi kwa ajili ya huduma hiyo muhimu kwa sekta ya afya.
Mbali na gari hilo la kubeba wagonjwa ambao ni pamoja na akina mama wenzake wakiwemo wajawazito, Geffi pia alitaja misaada mingine iliyotolewa na Mama Salma kuwa ni baiskeli 84 alizonunulia matawi yote 84 ya CCM ya wilaya hiyo anayoiwakilisha katika vikao vya NEC.
Bulembo alipokuwa mjini Lindi hapo juzi, jina la Mama Salma lilishangiliwa kwa nderemo na vifijo na Wajumbe wa Halmashauri Kuu ya CCM ya Wilaya hiyo waliokuwa kwenye kikao chao cha ndani baada ya kutamkwa na Bulembo aliyekuwa mgeni rasmi.
Kutokana na hali hiyo, Bulembo ambaye pia ni Mjumbe wa Kamati Kuu ya CCM alisema anampongeza MNEC huyo kwa kutimiza vizuri majukumu yake ya Utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya Mwaka 2010/2015, lakini pia kwa kukifanyia kazi kubwa chama hicho licha ya kutingwa na shughuli nyingi za kitaifa na kimataifa.

No comments: