Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa
(UN), Ban Ki-moon amesifu jitihada za Rais Jakaya Kikwete na mchango wake
mkubwa katika kupigania Afya ya Mama na Mtoto.
Alitoa pongezi hizo juzi wakati
alipokuwa akizungumzia juhudi za kumwokoa Mama na Mtoto baada ya Mwaka 2015,
mwishoni mwa mkutano wa siku 3 kuhusu Afya ya Mama na Mtoto kama ilivyoainishwa
katika Malengo ya Milenia.
Rais Kikwete na Waziri Mkuu wa
Canada, Stephen Harper, kwa miaka
minne wamekuwa Wenyeviti Wenza wa
Kamisheni ya Habari na Uwajibikaji katika masuala ya Afya ya Mama na Mtoto,
ambayo imekuwa mstari wa mbele kuhakikisha vifo vya watoto wachanga na mama
wajawazito vinapunguzwa kwa nusu ifikapo
mwaka 2015.
"Napenda kumpongeza Rais
Kikwete kwa mchango wake mkubwa katika jitihada hizi za kupunguza vifo vya
watoto na akina mama. Rais Kikwete na Waziri Harper wamedhihirisha uongozi
katika kukuza Afya ya Mama na Mtoto, nawapongeza sana," alisema na
kuwataka viongozi wengine kuiga mfano wa Canada wa kuchangia zaidi katika
jitihada hizo.
Pamoja na mafanikio hayo, Rais
Kikwete amesema bado jitihada zinahitajika katika kuhakikisha mafanikio haya
yanaimarishwa zaidi na kwamba hayapotei.
“Bado tunahitaji wataalamu wa
afya wenye ujuzi, vifaa na teknolojia ya kisasa." Amesema na kuongeza kuwa
bado zinahitajika juhudi za pamoja katika kusimamia mafanikio yaliyokwisha
kupatikana.
Katibu Mkuu huyo wa UN amesema
afya ya mama na mtoto ni ajenda muhimu kupigania hata baada ya mwaka 2015 kwani
ni muhimu kwa maendeleo.
Rais Kikwete pia alihudhuria
chakula cha jioni kilichoandaliwa na wafanya biashara wa Canada na Tanzania
ambapo ameelezea umuhimu wa biashara na uwekezaji nchini kwa madhumuni ya
kukuza uchumi wa Tanzania.
Alisema Tanzania inahitaji
vitega uchumi zaidi kutoka Canada na hivyo kuwakaribisha wawekezaji na
wafanyabiashara wa Canada kuja kuwekeza Tanzania.
Rais Kikwete alitarajiwa
kuondoka Toronto jana kurejea Dar es Salaam, kupitia Marekani.
No comments:
Post a Comment