MALARIA SASA KUBAKI HISTORIA ZANZIBAR



Wizara ya Afya Zanzibar, imezindua ugawaji wa vyandarua vyenye dawa ya muda mrefu ikiwa ni mkakati wa kuhakikisha ugonjwa wa malaria unatokomezwa Zanzibar.
Akizindua mpango huo, Waziri wa Wizara hiyo, Juma Duni Haji alisema kukamilika kwa ugawaji wa vyandarua hivyo kunaweza kutokomeza moja kwa moja ugonjwa wa malaria ambao kwa Zanzibar upo chini ya asilimia moja.
Alisema licha ya maambukizi kuwa chini ya asilimia moja, lakini mikakati ya wizara ni kuhakikisha ugonjwa huo unabaki kuwa historia katika Visiwa vya Zanzibar.
“Kwa kweli hadi sasa maambukizi yapo chini ya asilimia moja, lakini mipango yetu ni kuhakikisha malaria yanabaki kuwa historia nchi hii, ndiyo maana tunaandaa kila mkakati kufikia lengo hilo,” alisema Duni.
Alisema jumla ya vyandarua 315, 465 vinatarajiwa kugawiwa kwa wakazi wa Unguja na Pemba ambapo Unguja vitagawiwa vyandarua 221,803. Pemba watapata vyandarua 78,637.
Amewataja watakaonufaika na vyandarua hivyo kuwa ni wajawazito, walemavu, wajane na waliofikwa na majanga yanayosababisha kukosa uwezo wa kununua vyandarua.
Kwa upande wa Msaidizi Meneja wa Kitengo cha Kupambana na Malaria Zanzibar, Mwinyi Mselem alisema pamoja na kutoa vyandarua hivyo, kitengo chake pia kinaendelea na upigaji dawa kwa ajili ya kuua mazalio ya mbu wa malaria.

No comments: