Ukatili,
udhalilishaji na ukiukaji wa haki za mtoto, ikiwemo tabia ya wazazi au walezi
kuwatuma watoto vileo na kwenda nao kumbi za starehe vinadaiwa kukithiri
hali ambayo serikali imeshauriwa kuchukua hatua kuvidhibiti.
Wakati
wanasheria kupitia Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC) wamepaza sauti
kukemea vitendo hivyo, kwa upande wao watoto kutoka maeneo tofauti nchini,
wametaka haki zao ziheshimiwe ikiwa ni pamoja na kuhakikisha serikali
inadhibiti nyumba za wageni na madanguro karibu na shule zao.
Hayo
yamesemwa jana katika Maadhimisho ya Siku ya Mtoto wa Afrika yaliyofanyika jana
katika maeneo mbalimbali nchini.
Akizungumza
na waandishi wa habari jana jijini Dar es Salaam, Kaimu Mkurugenzi wa LHRC,
Harold Sungusia, alisema matukio ya ukiukwaji wa haki za watoto
yanaongezeka.
Alizungumzia
pia matumizi mabaya ya picha za watoto katika mitandao ya kijamii na vyombo vya
habari hususani walioathirika na vitendo vya ukatili.
Alisema
vitendo vyote vinavyonyima watoto haki vinakwenda kinyume na Sheria ya Mtoto ya
mwaka 2009.
“Kumekuwepo
na tabia ya wazazi ama walezi kuwatuma watoto wao vileo kama pombe na sigara na
hata wengine kudiriki kwenda na watoto wao katika kumbi za starehe mpaka
majira ya usiku sana… hivyo vyote ni vitendo ambavyo vinakwenda kinyume na haki
ya mtoto,” alisema Sungusia.
Alisema
wazazi hawajasimamia vyema wajibu wao kuhakikisha watoto wao wanakua
katika malezi yenye maadili salama kwa kuwathamini na kuwalinda katika
matukio mbalimbali ambayo yanaweza kuwanyima haki stahiki.
Alisema
katika kuadhimisha Siku ya Mtoto wa Afrika, wazazi na walezi waitumie kwa
kutokuruhusu kuwepo kwa picha mbaya za watoto walioathirika na vitendo vya
ukatili, katika mitandao ya kijamii. Alisema picha hizo huwaumiza
watoto.
Kuhusu
watoto kufanyishwa kazi za ndani, alisema yamekuwepo matukio mengi ya watoto
kupelekwa maeneo ya mijini kwa ajili ya kufanya kazi za ndani na kusababisha
kuishi katika mazingira magumu.
“Watoto
kama hao wanapopelekwa mijini hujikuta wakiishi katika mazingira magumu sana na
kuanza kufanyiwa ukatili wa kimwili, kiakili na hata kingono,” alisema
Sungusia.
Pia
matukio ya watoto kubakwa na kulawitiwa ni vitendo vya ukatili ambavyo
kituo hicho cha wanasheria, kimesema vinaendelea kufanywa na wazazi, walezi na
jamaa wa karibu.
Sungusia
alisema ukatili huo unaendelea licha ya kuwepo sheria ya kumlinda mtoto.
Alisema kutokana na kukithiri kwa matukio yasiyojali haki ya mtoto, ni wakati
wa jamii kuthamini na kuheshimu nafasi ya watoto.
Katika
Maadhimisho ya Siku ya Mtoto wa Afrika mkoani Dar es Salam, wanafunzi wameomba
Serikali kudhibiti nyumba za wageni na madanguro yaliyojengwa karibu na
shule zao.
Katika
risala yao, walisema moja ya changamoto kubwa wanazokutana nazo, uwepo wa
nyumba hizo hufanya wanafunzi wengi kuacha maadili yao na kufuata vitendo
ambavyo havina maadili.
Maadhimisho
hayo huadhimishwa kila Juni 16, kila mwaka na nchi za Afrika
51 kutokana na vifo vya watoto vilivyotokea Soweto Afrika Kusini mwaka 1976 na
kauli mbiu ya mwaka huu ni “Kupata elimu iliyobora na isiyo na vikwazo ni haki
ya kila mtoto.”
Mkuu
wa Wilaya ya Ilala, Raymond Mushi aliyekuwa mgeni rasmi kwenye maadhimisho
hayo, alisema serikali imejipanga vyema kukomesha vitendo vya
ukatili kwa watoto. Alisema pia inajipanga kudhibiti ujenzi holela wa nyumba za
muziki karibu na shule.
Katika hatua nyingine, Halmashauri ya
Wilaya ya Hai, mkoani Kilimanjaro ikishirikiana na viongozi wa serikali,
Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuhudumia Watoto (UNICEF) na Shirika la Save the
Children, imezindua kituo cha huduma jumuishi, kitakachosaidia wanawake na
watoto walioathiriwa na ukatili.
Katibu
Mkuu wa Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii, Charles Pallangyo, alisema
kituo kitatoa msaada wa kisaikolojia, ulinzi, usalama na msaada wa
kisheria.
Kwa
upande wake, Mwakilishi wa Unicef Tanzania, Dk Jama Gulaid, alisema
anaamini wadau wakishirikiana na serikali, watapata suluhu katika kumaliza
ukatili dhidi ya watoto.
Kwa
mujibu wa Utafiti juu ya Ukatili Dhidi ya Watoto, uliozinduliwa na Wizara ya
Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto mwaka 2011, wastani wa msichana kati
ya watatu na mvulana kati ya wavulana saba, wamefanyiwa vitendo vya ukatili wa
kingono.
Utafiti
unaonesha, zaidi ya asilimia 70 ya wasichana na wavulana wamefanyiwa vitendo
vya ukatili wa kimwili kabla hawajafikia umri wa miaka 18. Hata hivyo,
waathirika wengi hawajamwambia mtu yeyote ukatili waliofanyiwa na ni kesi
chache zimefikishwa polisi.
No comments:
Post a Comment