Wananchi wa Jimbo la Monduli wilayani
Monduli mkoani Arusha wametakiwa kuwang’oa madarakani viongozi wa vijiji
wanaoshiriki kinyume na utaratibu kuuza ardhi bila ya kufuata utaratibu kwa
kuendekeza zawadi ya bia na nyama choma.
Kauli hiyo ilitolewa juzi na Mbunge wa
Jimbo la Monduli, Edward Lowassa mara baada ya kuzindua bwawa la maji la Leken
lililopo Kijiji cha Selela, Kata ya Selela wilayani Monduli lililobomoka
kutokana na mafuriko ya Novemba mwaka 2011 na ukarabati wake kugharimu zaidi ya
Sh bilioni 1.1.
Alisema viongozi wa vijiji wanaongoza
kwa kuuza ardhi katika Wilaya ya Monduli na kibaya zaidi ardhi hiyo huuzwa kwa
wageni kutoka nje ya nchi, wakati mwingine kwa kuhongwa bia na nyama choma.
Alisema wakati umefika kwa wananchi
kuwang'oa viongozi wa namna hiyo kwani wanaweza kuingiza jamii ya Monduli
katika matatizo makubwa kwa uroho wao binafsi kwani ni aibu kiongozi kwa kijiji
kuhongwa bia na nyama choma halafu unatoa ardhi kubwa bila ya kuangalia athari
ya baadaye.
Lowassa alisema mkutano mkuu wa kijiji
tu ndio wenye mamlaka ya kuuza ardhi kupitia kikao halali na sio kiongozi
binafsi hivyo aliwataka wananchi kuwapigia kura ya hapana viongozi wenye
kushiriki kuuza ardhi kiholela kwa maslahi yao binafsi.
Alisema kasi ya kuuza ardhi ni kubwa
sana hivyo ni lazima kwa kila mkazi wa Wilaya ya Monduli kuwa macho na hilo
kwani hali hiyo ikiendelea kutafanya watoto wa Monduli kuwa wakimbizi katika
maeneo mengine kitu ambacho ni hatari.
Lowassa ambaye pia amewahi kuwa Waziri
Mkuu alisema watu wanaongezeka, lakini ardhi haiongezeki hivyo aliwaasa
viongozi wa vijiji jimboni mwake kuacha kuuza ardhi kwa bakshishi ndogo kwani
vizazi vijavyo vinaweza kutaabika.
Akizungumzia maji,Lowassa aliwataka
wakazi wa Kijiji cha Selela kulilinda bwawa hilo kama mboni ya jicho kwani
bwawa hilo lenye uwezo wa kuhifadhi maji
yenye lita za ujazo 392,040,000 lina uwezo wa kuhifadhi maji kwa zaidi
ya miaka mitatu hivyo ni jukumu la kila mtu kufuata utaratibu wa kulilinda.
Lowassa alisema alipopata ubunge mwaka
1995 tatizo kubwa katika Jimbo la Monduli lilikuwa maji pale Monduli mjini na
vijijini ilikuwa tatizo kubwa na wazee wa kijiji cha Selela ndio waliokuwa
wakimpa nguvu ya kuwa Mungu atamsaidia na tatizo hilo litafika mwisho na ndio
maana kwa sasa Monduli ina maji hadi Kijiji cha Selela chenye wakazi 26,671.
Alimshukuru Rais Jakaya Kikwete kwa
kupeleka fedha za ukarabati mabwawa 6 katika Jimbo la Monduli kiasi cha Sh
bilioni 3 likiwemo bwawa la Leken na aliwataka wakazi wa mabwawa hayo kumuenzi
Rais kwa kuyatunza kwa faida yao na mifugo.
Alisema bajeti ya Wizara ya Maji kwa
nchi nzima inaonesha kuwa maji yamefika katika maeneo kwa asilimia 50 lakini
katika Wilaya ya Monduli kwa sasa peke yake maji yameshafika kwa asilimia 60
hiyo ni jitihada nzuri na inapaswa kupongezwa.
No comments:
Post a Comment