Babu
aliyefunga ndoa mwaka 2011 akiwa na umri wa miaka 94, Mathias Kisokota mkazi wa
Kitongoji cha Isunta, Namanyere wilayani Nkasi ambaye kwa sasa ana umri wa miaka 97,
amehamia na mkewe katika Mji wa Mpulungu
mwambao wa Ziwa Tanganyika nchi
jirani ya Zambia miezi
sita iliyopita kwa lengo la kufanya tambiko la kumwezesha mkewe mwenye
umri wa miaka 83 kupata mtoto wa uzeeni.
Mke wa
mzee huyo, Uria Mwamanzi ni
mwenyeji wa nchi jirani ya Zambia alizaliwa na kukulia
katika Mji wa Mpulungu
mwambao mwa Ziwa Tanganyika ambapo
kwa mujibu wa wajukuu zao
ndiko babu yao alipokutana
naye na kuwa na
mahusiano hadi walipofunga
ndoa miaka mitatu iliyopita.
Wanandoa
hao ambao waliacha gumzo kubwa baada ya kufunga pingu za maisha katika Kanisa
Katoliki la Mtakatifu Anthony, alasiri ya Juni 18, 2011 mjini Namanyere Makao
Makuu ya Wilaya ya Nkasi.
Akizungumza
na mwandishi wa
habari kwa njia ya simu kutoka
katika Mji wa Namanyere jana, Salvatory Adolf (19), mjukuu wa wazee hao kutoka kwa mtoto wao kitindamimba
mwenye umri wa miaka 40 sasa, alisema babu yake
amemsindikiza mkewe huyo ili kwenda kutambikia mizimu
ya kwao.
“Bibi hakuwa
na raha mara kwa mara alikuwa akitamani
kurudi nchini kwao
Zambia kuwasalimia nduguze pia akiwa
huku alikuwa akiugua mara kwa
mara hivyo babu aliona
bora amsindikize bibi
akatambike kwa mizimu ya babu
zake nchini humo,” alisema.
Hata
hivyo, hakutaka kueleza kwa undani juu ya kiu ya babu yake ya kutaka kupata
mtoto, habari ambazo zinazungumzwa na watu wa karibu waliopo ndani ya familia ya wanandoa hao.
Miongoni
mwao, Agnes ambaye ni mtoto wa mwisho wa Mzee Kisokota akizungumza na mwandishi
wa habari hizi kwa njia ya simu kutoka mjini
Namanyere, Nkasi alisema baba yake amekuwa na hamu
hadi sasa ya kupata mtoto katika ndoa yake changa.
“Anasali sana akiomba kila siku
apate mtoto katika ndoa yake. Bado ana matumaini makubwa ….. nikianza
kukusimulia tutakesha, tena anasema siku akijaliwa
mtoto katika ndoa yake hiyo atajawa na
furaha kubwa na kufanya sherehe ya aina yake… amemsindikiza
bibi (mkewe) Zambia kusalimia ndugu zake pia kutambika
kwa kuwa baba ana hamu ya mtoto atatumia
fursa hii nae kutambikia kwa wakwe zake ili
mkewe huyo ashike mimba,“ alieleza Agnes.
Hali
hiyo inakuja licha ya ukweli kwamba, umri wa mke wa Mzee Kisokoto kuzaa
umeshapitiliza, lakini kwa pamoja wamedaiwa kuamini kwa Mungu hakuna
kisichowezekana hivyo anaweza kutenda miujiza kwa kuwapa baraka ya mtoto wa
ndoa yao ya uzeeni.
Mjukuu huyo alipoulizwa juu ya ziara hiyo kuhusisha
pia kusaka mtoto kutoka kwa `mizimu’ ya ukoo
wa mke wa babu yake, hakuwa na majibu ya moja kwa moja.
“Bibi alipoondoka
alikuwa akisumbuliwa na
maumivu ya mwili lakini tangu
atambike nchini Zambia inadaiwa amepona kabisa na
sasa wanaishi raha mustarehe na
babu… ila watarudi huku
kwetu baadae mwaka huu …”, alisema.
Katika
safari ya wazee hao, Adolf anasema bibi na babu yake walisindikizwa na Claudio
Mathias (21), kaka wa mjukuu huyo na kwamba kaka huyo amesharejea nchini.
Wanandoa hao
kwa mujibu wa wajukuu
zao kabla ya kufunga ndoa katika Kanisa Katoliki Jimbo
la Sumbawanga mjini
Namanyere miaka mitatu iliyopita walikuwa
wakiishi ‘kinyumba’ kila mmoja wao akibahatika
kuwa na watoto katika mahusiano yake ya awali.
Kwa
pamoja wana wajukuu zaidi ya 30
na vitukuu zaidi ya 40 wengi wao wakiishi
nchi jirani ya Zambia. Mzee
Kisokoto alifiwa na mke wa kwanza zaidi ya miaka 39 iliyopita.
No comments:
Post a Comment