DIT WAANDAMANA KUPINGA KUZUIWA KUFANYA MITIHANI



Wanafunzi wa Taasisi ya Teknolojia Dar es Salaam (DIT) jana waliandamana kwenda Wizara ya Sayansi na Teknolojia wakidai hawajaridhishwa na uamuzi wa uongozi wa chuo kuwazuia wanafunzi 684 kufanya mtihani.
Imeelezwa kuwa wanafunzi hao hawajaruhusiwa kufanya mtihani kutokana na kushindwa kukamilisha ada na usajili wa kufanya mtihani uliotakiwa kuanza juzi.
Rais wa Serikali ya Wanafunzi DIT, Himida Elihuruma alisema hayo jana, Dar es Salaaam wakati wa maandamano hayo. Alisema utaratibu wa kujisajili uliowekwa na taasisi hiyo haujafuatwa hivyo kuleta mkanganyiko kwa wanafunzi hao kujua siku ya kukamilisha usajili.
Alisema wapo wanafunzi waliokamilisha usajili, lakini wamewekwa katika idadi ya ambao hawajakamilisha hatua hiyo, na hali hiyo imetokana na utaratibu mbovu wa kutunza kumbukumbu za wanafunzi.
“Sisi tumeandamana kupinga uamuzi wa mkuu wa chuo kwani kila mwanafunzi ana haki ya kufanya mtihani kulingana na  utaratibu wa chuo, wasiolipa ada wanapaswa kuzuiwa wasichukue matokeo kama mwaka jana, ’’alisema Elihuruma.
Naye, Ofisa Uhusiano wa DIT, Amani Kakana alisema idadi kamili ya wanafunzi wasiosajiliwa ni 180 na sio idadi iliyotajwa na serikali ya wanafunzi.
Alisema uongozi haujachukua hatua zaidi ya kuwataka kuendelea na mitihani kwa wenye vigezo.
Alisema kundi la watu wachache ndio limewachochea wanafunzi wengine kuingia katika mgomo huo na wakati wenzao wanafanya mtihani walifanya vurugu kwa kuwatoa katika chumba cha mtihani huo.
Katibu Mkuu Wizara ya Sayansi na Teknolojia, Patrick Makungu aliwasisitiza wanafunzi hao kurudi chuoni hapo kwani matatizo yao yatatatuliwa kama walivyotarajia.

No comments: