Baadhi ya wafanyabiashara ndogo wa Dar es Salaam
ambao wamegoma kuondoka katika maeneo yasiyoruhusiwa, wamesema suluhisho pekee
ni wao kutafutiwa maeneo mazuri ya kufanyia shughuli zao.
Wafanyabiashara hao ambao awali waliondolewa kufanya
biashara zao katika maeneo yasiyoruhusiwa na askari waliokuwa wakisafisha jiji,
wameonekana kurudi katika maeneo hayo na kuendelea na shughuli zao.
Wakizungumza na mwandishi, baadhi yao wamedai kuwa
maeneo yaliyotengwa kwa ajili ya wafanyabiashara ni machache hivyo yanachukua
wafanyabiashara wachache, jambo linalowafanya wao waendelee kutafuta riziki
katika maeneo hayo.
Mfanyabiashara Said Kudra anayefanya shughuli zake
katika eneo la Ilala alisema, kitendo cha wao kuondolewa katika maeneo ya
shughuli zao bila kuoneshwa maeneo yanayoruhusiwa si sahihi.
"Unajua
ndugu mwandishi nikuhakikishie tu, kwamba hakuna mtu anayependa usumbufu wa
aina hii wa kufukuzwa na kurudi, lakini hii inatokea kwa sababu tunafukuzwa
lakini hakuna maeneo tunayoelekezwa twende," alisema Kudra.
Alisema hata inapotokea wanaelekezwa maeneo ya
kwenda, tayari maeneo hayo yanakuwa yameshajaa na hayana nafasi jambo
linalowalazimu wao kurudi walipoondolewa.
Naye Ester Julius wa Buguruni alisema kwa kiasi
kikubwa baadhi yao wamekuwa wakitegemea maeneo hayo kupata riziki, hivyo
serikali ione umuhimu wa kuongeza maeneo zaidi ambayo wanaweza kufanya biashara
zao.
Aidha, mfanyabiashara mwingine aliyejitambulisha kwa
jina la Mama Dora wa Kinondoni Mkwajuni alisema, kikubwa ni serikali iweze
kuangalia namna ya kuwasaidia badala ya kuwatimua maeneo hayo na kusababisha
mitaji yao kupotea.
Alisema baadhi yao wako tayari kuondoka katika
maeneo hayo endapo wataelekezwa maeneo sahihi ya kufanyia biashara zao.
Ofisa habari wa Manispaa ya Temeke, Joyce Msumba
alisema manispaa hiyo inatarajia kujenga soko jipya la kisasa na lenye hadhi ya
wilaya ambalo litatumiwa na
wafanyabiashara ndogo.
"Hii iko kwenye mpango wa DMDP (Dar es Salaam
Metropolitan Development Project) na tayari utafiti wa awali umeshafanyika na
kuangalia linaweza kuchukua watu wa ngapi na ubora wake kwa ujumla,"
alisema Joyce.
Aidha kwa Manispaa ya Kinondoni, wafanyabiashara hao
walishatangaziwa masoko wanayotakiwa kwenda kufanya biashara zao. Aidha Ofisa
Uhusiano wa Manispaa ya Ilala tabu Shaibu, mapema mwaka huu alisema manispaa
hiyo imebaini kuwa wafanyabiashara 21,500 hawana maeneo ya kufanyia biashara
jambo linalosababisha wavamie hifadhi za barabara.
Alisema manispaa hiyo imerenga Sh milioni 240 kwa
ajili ya ujenzi wa mabanda ya masoko ili wafanyabiashara hao waweze kupata
sehemu za kufanyia shughuli zao.
No comments:
Post a Comment