WALIMU WANNE SEKONDARI YA KINDAI WATIMULIWA KWA UDHALILISHAJI



Walimu wanne wa shule ya Sekondari Kindai, Manispaa ya Singida wametakiwa kuhama mara moja.
Wamepewa agizo hilo baada ya kukiri kuwa walitoa adhabu ya udhalilishaji kwa wasichana wote wa shule hiyo, kwa madai kuwa mmoja wao alitupa chooni taulo ya kike  iliyotumika.
Walimu waliohusika na mkasa huo na kukumbwa na tamko hilo ni Hadija Mussa, Sara Kabogo, Evodia Zablon na Elina Mathias ambao walikiri kutenda kosa hilo na kuahidi kutorudia tena.
Walimu hao walikiri kutenda makosa hayo mbele ya mkutano wa dharura wa wazazi,  ambao pia ulihudhuriwa na Ofisa Elimu Sekondari wa Manispaa ya Singida, Omari Kisuda.
Wazazi hao walifikia uamuzi huo, baada ya walimu hao kukiri kuwa kitendo walichokuwa wamekifanya kwa wasichana wa kidato cha kwanza hadi cha nne, kilikuwa ni kinyume cha sheria na ilikuwa ni udhalilishaji wa watoto wa kiwango cha juu.
Kwa mujibu wa walimu hao, walilazimika kutoa adhabu hiyo baada ya kukuta mmoja wa wanafunzi wa kike wa shule hiyo, akiwa ametupa taulo hilo  ovyo chooni. Tukio hilo ni la Mei 22, mwaka huu.
Ilidaiwa kwenye kikao hicho kuwa baada ya kuikuta taulo hiyo ndani ya choo, walimu hao waliamuru wanafunzi wailoweke kwenye ndoo ya maji ya lita 20 hadi maji yote, yaenee rangi ya damu iliyokuwa kwenye taulo hilo.
Hapo ndipo, wanafunzi  walipopangwa mstari na kuanza kuchapwa viboko 16 kila mmoja kwenye viganja vya mikono yao, kisha kunawishwa kwa nguvu maji hayo yaliyokuwa na uchafu wa damu ya taulo hiyo iliyotumika, iliyochanganyikana na uchafu wa chooni.
Inadaiwa kuwa baada ya kitendo hicho kufanyika, wanafunzi hao waliagizwa kurudi kwao na kwamba wakale chakula bila kunawa mikono yao.

No comments: