NYUMBA ZENYE VICHAKA KUTOZWA FAINI PAPO KWA HAPO



Wakazi ya Afya na Ustawi wa Jamii kwa kushirikiana na manispaa za Dar es Salaam, zitaanza kampeni ya kukagua maeneo ya makazi ya watu yenye vichaka.
Vichaka hivyo ni vile vinavyofanya mbu wa kueneza ugonjwa wa homa ya dengue, kuzaliana.
Watu hao watatozwa faini za papo hapo  na nyumba zao zitafanyiwa usafi.
Akizungumza na mwandishi jana, Ofisa Ufuatiliaji wa Magonjwa wa Mkoa wa Dar es Salaam, Alex Mkamba alisema kampeni hiyo inatarajia kuanza hivi karibuni.
Alisema watafanya ukaguzi katika makazi ya watu na shule na lengo ni kukabiliana na homa ya dengue, inayozidi kushika kasi.
“Tunaanza kampeni ya kukagua maeneo ya watu, ambayo hayajafanyiwa usafi yanayosababisha mbu kuzaliana na tutashirikiana na Manispaa zote za jiji,” alisema Mkamba.
Alisema watatoza faini shule ambazo hazijatoa elimu kwa wanafunzi wao juu ya  homa ya dengue, ambayo imekuwa tishio katika jiji la Dar es Salaam.
Akielezea hali ya ugonjwa huo, alisema jana wagonjwa wapya 39 walikutwa na ugonjwa huo, ambapo waliolazwa ni 20 na wako katika Hospitali za Temeke, Amana na Mwananyamala.
“Hivi karibuni hakuna mtu aliyekufa kutokana na ugonjwa wa dengue na hiyo ni kutokana na kwamba wanafika hospitali mapema kabla ya kufikia katika hatua ya pili ambayo mgonjwa anakuwa ameshaharibika ini na figo na hivyo kutokwa damu nyingi, kukojoa na kuharisha damu, tunajitahidi kutoa elimu,” alisema Mkamba.
Alisema tangu ugonjwa huo ulipuke katika jiji la Dar es Salaam, watu 2,247 walipimwa ambapo 1,014 walikutwa wamepata homa ya ugonjwa huo. Wilaya ya Kinondoni inaongoza kwa kuwa na  wagonjwa  wengi.
Mpaka sasa ugonjwa huo, hauna tiba maalumu wala chanjo. Njia pekee ya kukabiliana nao ni kutambua dalili zake kama vile homa, kupungukiwa maji au damu, kuumwa kichwa, maumivu ya viungo na uchovu.
Mgonjwa anaweza kupoteza maisha, endapo atachelewa kupatiwa matibabu. Wananchi wanatakiwa kuchukua hadhari juu ya ugonjwa wa dengue, ambao dalili zake ziko sawa na zile za malaria.

No comments: