MALAWI WAKESHA WAKISUBIRIA MATOKEO UCHAGUZI MKUU



Tume ya Uchaguzi nchini Malawi  (MEC) imesema Uchaguzi Mkuu wa Rais, ulikuwa huru na wa haki, ingawa Rais    alifuta uchaguzi huo.
Hayo yamesemwa na Mwenyekiti wa Tume hiyo, Maxon Mbendera.
“Uchaguzi Mkuu wa Urais nchini Malawi ulifanyika kwa uhuru, haki na namna ya uaminifu ingawa kulikuwa na makosa,” alitangaza wakati Wamalawi katika maeneo mbalimbali, wakikesha ili kupokea matokeo ya uchaguzi huo.
"Kwa raha naweza kusema uchaguzi ulikuwa wa uhuru na wa haki…pia ulikuwa wazi, kwa tathmini yangu, ulikuwa wa kuaminika,” alisema Mbendera.
Uchaguzi Mkuu huo ulileta utata na maswali, baada kugundulika mambo yasiyokuwa ya kawaida katika kwenye vituo vya kupigia kura 4,000.
Mwenyekiti huyo wa Tume alisema asilimia 99 ya upigaji kura, ulikuwa hauna matatizo na kuwa watu walionesha mapenzi yao.
Matatizo na mivutano hiyo, imesambaa hadi mahakamani, ambapo mgombea urais wa Chama cha upinzani cha Malawi Congress Party (MCP), Lazarus Chakwera alitaka kura hizo zirudiwe.
Lakini, Chama cha Democratic Progressive (DPP) kinachoongozwa na Profesa Peter Mutharika, aliyekuwa akiongoza katika matokeo ya awali, kiliungana na mawakili wa Tume ya Uchaguzi, kuzuia kuongezwa siku 30 za kuhesabu kura.
Tume hiyo ilisema inaendelea kujiandaa kutangaza matokeo ya Urais. Iliahidi kuwa ingetangaza matokeo hayo ya urais jana na hiyo ni kwa mujibu wa Sheria, labda kama kungetokea zuio la mahakama.
“Chochote kitakachoelekezwa na mahakama, tutafanya,” alisema Mbendera. Kwa mujibu wa Sheria, tume hiyo inalazimika kutangaza matokeo katika kipindi cha siku nane za uchaguzi na mwisho wa siku hizo, ilikuwa ni  mchana wa siku ya jana (Ijumaa).
Juzi Alhamisi, kesi iliyokuwa imefunguliwa mahakamani, ilikwama baada ya jaji aliyekuwa amechaguliwa kusikiliza, Healy Potani,  alijitoa kwa sababu kaka yake ni mjumbe wa tume ya uchaguzi.  Jaji mwingine, Kenyatta Nyirenda, alichaguliwa kuchukua nafasi hiyo na alitarajiwa angetoa uamuzi wake jana.
Mahakama Kuu ilitarajiwa itoe uamuzi Ijumaa, ambao ungewezesha Tume ya Uchaguzi, kutangaza matokeo uchaguzi huo uliopigwa Mei 20, mwaka huu au kuna haja ya kurudia kuhesabu kura zote zilizopigwa, hatua ambayo itachukua miezi miwili.
Kwa upande wake,  Rais wa Malawi, Joyce Banda alisema siku ya Alhamisi, kuwa angekuwa tayari kuondoka madarakani,  kama Mahakama Kuu ingetoa uamuzi wake kumaliza mgogoro huo wa uchaguzi.
Rais Banda alisema bado anaamini kuwa uchaguzi huo, ulifanyika katika mazingira ya ulaghai. Rais alidai uchaguzi huo, ulikuwa ‘batili na haukuwa wa uwazi’, kwani ulikuwa umegubikwa na mambo mengi yaliyokuwa sio ya kawaida. Aliagiza uchaguzi huo urudiwe upya ndani ya siku 90.
Hata hivyo, juzi, Rais Banda alisisitiza kuwa  "Nimeiambia MEC na wadau husika, kuwa nitakubali maamuzi ya Tume hiyo na uamuzi wa mahakama,”
Matokeo ya awali yalionesha kuwa mpinzani wa Banda, ambaye ni Profesa Mutharika, alikuwa anaongoza. Rais Joyce Banda alikuwa anafuatia.
Wapo wagombea wengine katika uchaguzi huo ni pamoja na Atupele Muluzi, ambaye ni mtoto wa Rais wa zamani, Bakili Muluzi.

No comments: