KAMBI YA UPINZANI WASUSIA KUJADILI BAJETI YA NISHATI NA MADINI



Habari zilizopatikana hivi punde zinasema, wabunge wanaounda kambi ya rasmi ya upinzani Bungeni wamesusia mjadala unaoendelea jioni hii kwa kile walichodai kuwa mkakati uliopangwa na wenzao wa CCM kujaribu kufunika madudu yaliyogubika ufujaji wa fedha za IPTL.
Akizungumza muda mfupi kabla ya kutoka nje ya Bunge, Kiongozi wa kambi hiyo, Freeman Mbowe alisema kuna kila dalili kwamba wabunge wa CCM walishakaa kikao kabla ya kuanza kujadili Bajeti ya Wizara ya Nishati na Madini kwamba wahakikishe wanasambaratisha kila hoja inayohusiana na suala zima la kampuni ya ufuaji umeme ya IPTL.
Mbowe alimshutumu Spika na wabunge wa CCM kujaribu kufifisha hoja za wapinzani waliosisitiza kutaka suala hilo lijadiliwe kwa kina na bila kutanguliza misimamo ya vyama vyao.
“Mheshimiwa Spika, humu ndani ni dhahiri kuna wabunge tayari wameingia na misimamo ya vyama vyao bila kujali suala hili ni zito sana kwa mustakabali wa taifa letu. Najua humu ndani mpo wengi kuweza kupitisha msimamo wenu kuhusu suala hili, lakini najua mtahukumiwa huko nje siku moja mbeleni,” alisema Mbowe.
Akahitimisha kwa kusema, “Ili tuwe na amani, naomba tuwaache muendelee kujadili wenyewe (CCM) suala hili kwa amani kabisa.”
Kauli hiyo ikazusha kelele kutoka kwa wabunge wanaomanika kuwa wa chama tawala cha CCM wakirusha maneno ya kejeli wakati  wabunge wa kambi ya upinzani wakitoka nje ya bunge majira ya Saa 10:30 jioni hii.
Mapema kabla, Waziri Kivuli wa wizara hiyo, John Mnyika akisoma Bajeti Mbadala ya kambi hiyo alielekeza shutumu nzito dhidi ya ufisadi uliokithiri kwenye suala zima la fedha ilizolipwa IPTL, ambapo alimwomba Spika wa Bunge, Anne Makinda kuunda kamati maalum ya Bunge kuchunguza suala hilo.
Wabunge wa kambi rasmi ya upinzani wanatoka katika vyama vya Chadema, CUF na NCCR-Mageuzi.

No comments: