VODAFONE 875 YENYE MFUMO WA ADROID YAINGIA MITAANI



Kampuni ya simu za mkononi ya Vodacom, Tanzania, imezindua ofa ya simu ya mkononi aina ya Vodafone 875 yenye mfumo Adroid kuwezesha matumizi zaidi ya intaneti katika jamii. Imesema simu hiyo itauzwa kwa Sh 100, 000.
Mkuu wa Idara ya Masoko na Mawasiliano wa Vodacom Tanzania, Kelvin Twissa, alisema hayo hivi karibuni, alipozungumzia utafiti uliofanywa kuhusu idadi ya watumiaji wa simu za mkononi na intaneti kwa Afrika ya Mashariki.
“Simu hii aina ya Vodafone 875 yenye mfumo Adroid inapatikana kwa Sh 100, 000 taslimu katika maduka yote ya Vodacom. Ni ya kisasa imeunganishwa na 3G na inampatia mteja uwezo wa kuperuzi mitandao ya Facebook, Whatsap, Twitter, Viber, Instagram na mingineyo,” alisema Twissa.
Aliongeza; “Mbali na uwezo wa simu hiyo inayopatikana kwa bei nafuu, mteja anunuapo simu hiyo atapatiwa MB 500 na SMS 200 bure kwa kila mwezi ndani ya miezi sita mfululizo. Ili kupata ofa hiyo, mteja atatakiwa kutuma neno CIMEI kisha kuacha nafasi ikifuatiwa na namba ya CIMEI ya simu kwenda namba 15300”.
Akizungumzia utafiti huo, alisema takwimu zinaonesha kwamba, Kenya inaongoza kwa maendeleo ya mawasiliano ya simu na intaneti kwa nchi za Kusini mwa Jangwa la Sahara ikifuatiwa na Tanzania, Uganda, Rwanda na Burundi.
Kwa mujibu wa Twissa, takwimu za Julai mwaka jana,  zinaonesha Kenya yenye wakazi milioni 44, ina watumiaji wa simu za mkononi milioni 30.4 huku wa intaneti wakiwa milioni  16.2 sawa na asilimia 41. 
Tanzania inafuata kwa kuwa na wakazi   milioni 48.3 na watumiaji wa simu za mkononi ni milioni 27.4 na wanaotumia intaneti ni milioni 5.31 sawa na asilimia 11 tu. 

No comments: