UTURUKI, TANZANIA KUJENGA KIJIJI CHA ALBINO 500



Ubalozi wa Uturuki kwa kushirikiana na Serikali ya Tanzania, wana mpango wa kujenga kijiji nchini  kwa ajili ya kutunza albino wapatao  500.
Ujenzi wa kijiji hicho unakadiriwa kugharimu  dola za kimarekani milioni tano sawa na Sh bilioni 8.2.
Mke wa Balozi wa Uturuki, Yesim Meco alisema hayo jana Dar es Salaam kwenye mkutano na waandishi wa habari, ambao mumewe, Ali Davutoglu alikuwa akizungumzia ujio wa meli  ya jeshi la nchi yake wiki ijayo. 
Yesim alisema lengo kubwa la kujenga kijiji hicho ni kusaidia watu hao wenye albinism.
Alisema kabla ya kuanza mchakato wa ujenzi wa kijiji hicho alifika mkoani Shinyanga iliko kambi yao na kukuta watu hao wakiwa na hofu kuu.
Alisema aliomba Serikali ya Tanzania kuhamishia kambi hiyo jijini Dar es Salaam , ambapo ndipo ofisi za Ubalozi huo zilipo ili kuweza kuwasaidia zaidi.
“Tunamshukuru Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa kutusaidia eneo la Bagamoyo ambapo tutajenga kijiji kwa ajili ya kuwasaidia watu hao kuweza kuyafurahia maisha na uhai wao pia,” alisema Yesim na kuongeza kuwa ujenzi huo unaratibiwa na Taasisi ya  Msaada ya Uturuki na Tanzania (TTAF).
Alisema katika kijiji hicho, kutakuwa na sehemu ya ufundi wa cherehani, bustani ya wanyama na shule ya ufundi ambapo watawafundisha wahusika jinsi ya kujipatia kipato katika maeneo mbalimbali.
Yesim alisema lengo ni kuwezesha kundi hilo kuishi sehemu salama ambayo itakuwa ya kisasa na eneo hilo litakabidhiwa kwa chama cha  watu wenye albinisim kwa ajili ya kuliendesha.
Kuhusu ziara ya meli, Balozi Ali alisema watakaofuatana nayo, watakuwa na shughuli mbalimbali nchini, kama vile kutembelea kituo cha watoto yatima na shule ya watu wenye mahitaji maalum.
Alisema ziara ya meli hiyo,  inaanzia Magharibi mwa Afrika ikitoa mafunzo katika bandari 29 za nchi za Afrika. Inapinga  uharamia na kuchangia katika usalama wa ukanda wa Bahari ya Hindi.

No comments: