Mawakili wa aliyekuwa Mkurugenzi
wa Manispaa ya Ilala, Gabriel Fuime (61), wameiomba Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu kufuta kesi
ya mauaji ya watu 27 inayomkabili Fuime na wenzake 11.
Wakiwasilisha hoja hiyo jana mbele ya Hakimu Mkazi Devotha Kisoka,
Wakili John Mhozya na Ndurumah Majembe waliiomba Mahakama kuangalia kwa makini
hati ya mashitaka kwa kuwa madai yaliyomo ni batili, hayakidhi matakwa ya
sheria.
Wakili Mhozya alidai kuwa, sheria
inataka hati ya mashitaka iwe na viashiria vya kosa ambalo
mshitakiwa anashitakiwa nalo, aliongeza kuwa Fuime ameshitakiwa kwa mauaji lakini hati iliyopo mahakamani
haina viashiria vinavyoonesha kosa hilo.
Awali alipoanza kuwasilisha hoja,
Hakimu Kisoka alisema jalada la kesi hiyo lipo Mahakama Kuu, hata hivyo
Mhozya aliomba kuendelea kuwasilisha hoja hiyo kwa kuwa jambo lililosababisha
lipelekwe huko halimhusu Fuime.
Wakili wa Serikali Mwandamizi,
Benard Kongola alipinga kwa madai kuwa Mahakama hiyo haina
mamlaka ya kusikiliza wala kusuluhisha chochote kwa sababu kesi imefunguliwa
hapo kwa taratibu za awali tu.
Hata baada ya Mhozya kupewa
nafasi ya kusikilizwa, Wakili Kongola alizidi kupinga na kudai kuwa hata jibu
chochote na anaweza kutoka nje ya Mahakama wakati kesi hiyo ikiendelea.
Wakili Majembe aliiomba Mahakama
kuzuia uvunjifu wa sheria na kudai katika kusoma kwake na uzoefu aliokuwa
nao hajawahi kuona kitu kinachodaiwa na upande wa mashitaka.
Aliongeza kuwa Mahakama ina uwezo
wa kuangalia kwa makini kosa ili kujiridhisha kwa kuwa uhuru wa mtu ni
muhimu na jela ni mbaya; “leo Fuime ameshitakiwa kwa kosa la mauaji kesho
anaweza kubadilishiwa likawa la kutakatisha fedha na baadaye hata kubaka."
Hakimu Kisoka
aliahirisha kesi hiyo hadi Mei 19, mwaka
huu Mahakama hiyo itatoa uamuzi kama inauwezo wa kufanya hivyo.
Mbali na Fume washitakiwa wengine
katika kesi hiyo ni mfanyabiashara Laza Radha, Diwani katika Manispaa ya
Kinondoni, Ibrahim Mohamed (59), vigogo wa Manispaa ya Ilala ambao ni Mhandisi
Mkuu, Charles Ogare (48), Mhandisi wa Majengo Godluck Sylivester (35) na
Mkurugenzi Mkuu wa Mkaguzi wa Majengo, Willibrod Mugyabuso (42).
Wengine ni Mhandisi Mohamed
Abdurkarim (61), Mhandisi Mshauri, Zonazea Oushoshaodaga Hema (59), Msajili
Msaidizi AQRB, Albert Mnuo na Ofisa Mkuu Mtekelezaji OQRB, Joseph Ringo (60),
Mkadiriaji Ujenzi, Vedasto Ruhale (59), Msanifu Majengo, Michael.
Inadaiwa kuwa Machi 29 mwaka jana, katika mtaa
wa India Gandhi Ilala, Dar es salaam kwa makusudi washitakiwa waliwaua watu 27
kutokana na kuporomoka kwa jengo la ghorofa 16.
No comments:
Post a Comment