HOTUBA YA
MAKADIRIO YA MAPATO NA MATUMIZI
YA OFISI YA
MAKAMU WA PILI WA RAIS
KWA MWAKA WA
FEDHA
2014/2015
UTANGULIZI
1.0
Mheshimiwa Spika, naomba kutoa
Hoja kwamba Baraza lako Tukufu likae kama Kamati ya Mapato na Matumizi ili
lipokee, lijadili na hatimae liidhinishe Makadirio ya Mapato na Matumizi ya
Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais kwa kipindi cha mwaka wa
fedha 2014/2015.
2.0
Mheshimiwa Spika,
tumekutana
tena katika kikao hiki cha nne cha Bajeti ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar
yenye Muundo wa Umoja wa Kitaifa kwa mwaka wa fedha 2014/2015 kwa ajili ya
kuzungumzia mipango na masuala muhimu ya nchi yetu kwa nia ya kuleta maendeleo
ya nchi na wananchi wake. Namshukuru
Mwenyezi Mungu kwa kutupa uwezo huu wa kukutana tena na ninamuomba aendelee
kutupa afya njema na kutuwezesha kuendesha kikao chetu hiki kwa hekima, busara
na uadilifu mkubwa. Ni imani yangu kuwa tutamaliza kikao hiki tukiwa tunaendelea
kubakia wamoja na wenye mshikamano mkubwa katika kuendeleza nchi yetu.
3.0
Mheshimiwa Spika, nachukua nafasi hii
kumshukuru kwa dhati Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.
Dkt. Ali Mohamed Shein kwa kuiongoza nchi yetu kwa umahiri na umakini mkubwa. Sote
ni mashahidi kuwa chini ya uongozi wa Dkt.
Ali Mohamed Shein, nchi yetu imeendelea kupata mafanikio makubwa katika nyanja
zote za kiuchumi, kijamii na kisiasa. Aidha, nchi yetu imeendelea kuwa katika
hali ya amani na utulivu mkubwa hali ambayo imetoa nafasi kwa wananchi
kuendelea na shughuli zao za maisha za kila siku bila bughudha wala usumbufu wowote.
Namuomba Mwenyezi Mungu aendelee kumpa afya njema na umri mrefu yeye na familia
yake, amzidishie hekima na busara ili aendelee kutuongoza katika hatua za
kuiletea nchi yetu maendeleo zaidi.
4.0
Mheshimiwa Spika, vilevile,
nachukua nafasi hii kumshukuru kwa dhati Mheshimiwa Makamu wa Kwanza wa Rais,
Maalim Seif Sharif Hamad kwa kuendelea kumsaidia na kumshauri vyema Mheshimiwa
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapindunzi na kwa mashirikiano yake mazuri kwa Ofisi yangu.
5.0
Mheshimiwa Spika,
pongezi
za pekee nazitoa kwako wewe mwenyewe binafsi Mheshimiwa Spika kwa jinsi
unavyoliendesha Baraza letu hili kwa umahiri na umakini mkubwa kwa kufuata
sheria na kanuni za Baraza. Uongozi wako wa busara kwa hakika umeimarisha demokrasia
ndani ya Baraza na kulipa Baraza letu mafanikio makubwa katika kutekeleza
majukumu yake. Tunakuombea kwa Mwenyezi Mungu akuzidishie uwezo na hekima katika
kutekeleza majukumu yako makubwa katika Taifa letu. Pia napenda kuwapongeza kwa dhati Naibu Spika
Mhe. Ali Abdalla Ali Mwakilishi wa Jimbo la Mfenesini na Wenyeviti wa Baraza Mhe. Mgeni Hassan Juma, Mwakilishi wa Viti Maalumu
na Mhe. Mahmoud Mohamed Mussa, Mwakilishi wa Jimbo la Kikwajuni kwa namna
wanavyokusaidia katika kuliendesha Baraza letu hili.
6.0
Mheshimiwa Spika, naomba nitumie
fursa hii pia kuwashukuru Wenyeviti na Wajumbe wa Kamati za Kudumu za Baraza la
Wawakilishi kwa kufuatilia kwa karibu utekelezaji wa malengo na maagizo mbalimbali
wanayoyatoa kwa Wizara wanazozisimamia. Aidha, natoa shukrani maalum kwa Mwenyekiti
wa Kamati ya Kudumu ya Kusimamia Ofisi za Viongozi Wakuu wa Kitaifa Mhe. Hamza
Hassan Juma, Mwakilishi wa Jimbo la Kwamtipura, Makamu Mwenyekiti Mhe. Saleh
Nassor Juma Mwakilishi wa Jimbo la Wawi na Wajumbe wote wa Kamati hiyo kwa
kuyapitia Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais na
kutupa ushauri unaotuongoza na kutusaidia katika utekelezaji wa malengo na
majukumu ya Ofisi yetu.
7.0
Mheshimiwa Spika,
pia
nawapongeza wajumbe wote wa Baraza hili Tukufu kwa kuipitisha Bajeti ya
Serikali iliyowasilishwa na Mheshimiwa Waziri wa Fedha. Bajeti hiyo ndiyo
itakayotuwezesha kuendesha kazi za Serikali katika kipindi cha mwaka wa fedha
2014/2015.
HALI YA SIASA
8.0
Mheshimiwa Spika,
tunamshukuru
Mwenyezi Mungu kwa kuendelea kuijaalia nchi yetu amani na utulivu. Katika
kipindi cha mwaka wa fedha 2013/2014 hakukua na matukio makubwa ya uvunjifu wa
amani yaliyotokea katika nchi yetu. Hali hii inatokana na wananchi wengi kuzidi
kuelewa umuhimu wa amani na kushirikiana na Serikali yao kudumisha amani na
utulivu kwa maendeleo ya Taifa letu na Ustawi wa jamii.
9.0
Mheshimiwa Spika,
kwa
kipindi cha mwaka wa fedha 2013/2014, nchi yetu imefanya chaguzi ndogo mbili
(2) ambazo zilihusisha Uchaguzi wa Mwakilishi wa Jimbo la Kiembesamaki Wilaya
ya Magharibi Unguja na Uchaguzi wa Diwani Wadi ya Kiboje Wilaya ya Kati Unguja. Tunavishukuru vyama vyote vya siasa
vilivyoshiriki katika chaguzi hizo ambazo ziliendeshwa kwa haki, uwazi, amani
na utulivu mkubwa. Aidha, tunawapongeza sana viongozi walioshinda katika
chaguzi hizo na tunawatakia mafanikio katika kuwatumikia wananchi waliowachagua
na nchi yetu kwa ujumla. Vilevile, nachukua nafasi hii kuwashukuru na
kuwapongeza sana wananchi wa Jimbo la Kiembesamaki na wananchi wa Wadi ya Kiboje kwa kuweza
kutumia demokrasia yao vizuri kuwachagua viongozi wao kwa imani ya kuwaletea
maendeleo katika maeneo yao.
MAADHIMISHO YA
SHEREHE ZA MIAKA 50 YA MAPINDUZI YA ZANZIBAR
10.0
Mheshimiwa Spika,
katika
mwaka huu wa fedha, nchi yetu
imeadhimisha Miaka 50 ya Mapinduzi Matukufu ya Zanzibar. Maadhimisho ya Sherehe
hizo yalizinduliwa rasmi tarehe 15 Agosti, 2013 na Mheshimiwa Rais wa Zanzibar
na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dkt. Ali Mohamed Shein na kufikia kilele
chake tarehe 12 Januari, 2014, Uwanja wa Amani, Zanzibar.
11.0
Mheshimiwa Spika,
kwa
muda wote wa maadhimisho haya hadi siku ya kilele tumeshuhudia shughuli na
matukio mbalimbali ambayo wananchi na viongozi walishiriki kikamilifu katika
maeneo yote ya Unguja na Pemba. Miongoni mwa matukio hayo ni Maonesho ya Miaka
50 ya Mapinduzi yaliyofanyika katika
viwanja vya Chuo Kikuu cha Taifa (SUZA), Kampasi ya Beit el Ras kuanzia tarehe
2 – 5 Januari, 2014; Maonesho ya Fensi; Maonesho ya Biashara yaliyofanyika
katika viwanja vya Maisara; Utoaji wa Nishani kwa viongozi na wananchi
mbalimbali waliotoa mchango wao katika Mapinduzi ya Januari 12, 1964 pamoja na
waliochangia katika maendeleo ya Zanzibar kwa jumla; Matamasha ya Michezo na
Burudani, Ujenzi wa Mnara wa Kumbukumbu ya Miaka 50 ya Mapinduzi ya Zanzibar
hapo Michenzani, Uwekaji wa jiwe la msingi na uzinduzi wa miradi ya maendeleo
na maonesho mbalimbali yaliyofanywa siku ya kilele katika Uwanja wa Amani.
12.0
Mheshimiwa Spika, sote ni
mashahidi wa namna sherehe zetu hizi zilivyokuwa zimefana sana na kuleta haiba
kubwa kwa nchi yetu. Hii imeonesha jinsi gani wananchi wetu wanavyothamini
Mapinduzi yetu ya Januari 1964 pamoja na maendeleo wanayoyaona kutokana na
Mapinduzi hayo.
13.0
Mheshimiwa Spika, kwa ruhusa yako
napenda kutoa pongezi na shukurani zangu za dhati kwa wananchi na viongozi wote
walioshiriki kwa njia moja au nyengine katika kufanikisha Maadhimisho ya
Sherehe hizo. Ni matumaini yangu kuwa sote kwa umoja wetu tutaendelea kudumisha
Mapinduzi haya ili kuendeleza amani na maendeleo katika nchi yetu.
14.0
Mheshimiwa Spika,
pamoja
na kutoa pongezi hizo, naomba kutoa masikitiko yangu
kuona kwamba hadi leo hii wapo watu wachache miongoni mwetu ambao wanauliza
uhalali wa Mapinduzi Matukufu ya Mwaka 1964. Ni dhahiri kwamba hata hawa
wanaohoji uhalali wa Mapinduzi kwa kiasi kikubwa wamefaidika na Mapinduzi haya.
Mwenye macho haambiwi tazama kwani baada
ya Mapinduzi ya 1964 ndio nchi hii imeshuhudia mafanikio makubwa ya maendeleo katika
nyanja zote. Hivyo hatuna budi kuyalinda na kuyaendeleza Mapinduzi yetu kwa
manufaa yetu na vizazi vijavyo.
15.0
Mheshimiwa
Spika, dhana ya Mapinduzi ilikuwa ni kuleta maisha bora kwa kila
Mzanzibari na kuondoa ubaguzi wa aina zote na kuleta umoja na maendeleo na
ndio kilichofanyika. Haya mengi ambayo leo tunayaona hayakuwepo kabla ya Mapinduzi
ambayo ni pamoja na kuwepo kwa nyumba bora za kuishi, kuimarika kwa huduma za
elimu, afya na kupatikana kwa maendeleo makubwa katika Sekta ya Miundombinu,
Kilimo, Maji na Umeme, Uchumi na Biashara, na kuwepo kwa uhuru wa kushiriki
shughuli za siasa.
16.0
Mheshimiwa
Spika, naomba tuelewe kwa nini tunatoa kipaumbele katika
kuweka kumbukumbu za Mapinduzi hasa katika maadhimisho yake. Kwa kweli ni jambo
la ajabu kuona miongoni mwetu bado wapo watu wanaohoji umuhimu wa Sherehe za
Mapinduzi au kuweka vielelezo vya Mapinduzi. Tunasema tutaendelea kuenzi na
kuheshimu kazi nzuri iliyofanywa na Wazee wetu ya kutukomboa na kutupatia
Uhuru wa nchi yetu.
17.0
Mheshimiwa
Spika, kwa ajili ya kuweka kumbukumbu ya kutimiza miaka 50 ya Mapinduzi,
Serikali kwa makusudi imefanya uamuzi wa kujenga Mnara katika eneo la
Michenzani. Hii inatokana na historia ya eneo hilo katika harakati za kuikomboa
nchi yetu. Aidha, Serikali ina dhamira ya dhati ya kuendeleza azma ya Marehemu
Mzee Abeid Amani Karume ya kuendeleza eneo hilo na kulifanya kuwa eneo la
biashara na kuwa kivutio kwa wageni, watalii na wananchi kwa ujumla.
18.0
Mheshimiwa
Spika, mnara unaoendelea kujengwa utakuwa pia ni kituo kwa
wananchi na wageni kusoma historia ya Mapinduzi na waanzilishi wake kwani kutakuwa
na maktaba maalum. Katika eneo hilo kutakuwa na mkahawa na bustani ya
mapumziko ambayo itasaidia sana kupunguza msongamano katika maeneo ya Forodhani
hasa wakati wa sikukuu. Naomba wananchi waelewe kuwa mnara huo unajengwa kwa
Fedha za Mfuko wa Hifadhi ya Jamii (ZSSF) na utaendeshwa kibiashara na kwa
faida.
MASUALA YA MUUNGANO
19.0
Mheshimiwa Spika,
Muungano
wa Tanganyika na Zanzibar hivi sasa umetimiza miaka 50 (Nusu Karne) tangu
ulipoasisiwa tarehe 26 Aprili, 1964. Sherehe za kutimiza Miaka 50 ya Muungano
wetu zilizinduliwa rasmi hapa Zanzibar na Mhe. Dkt. Ali Mohamed Shein, Rais wa
Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi tarehe 01 Machi, 2014 katika Ukumbi
wa Salama, Hoteli ya Bwawani na kilele chake kilifanyika Dar es salaam tarehe
26 Aprili, 2014. Kipindi cha miaka 50 ni kirefu na nchi yetu ina kila sababu za
kujivunia kutokana na kuudumisha Muungano wetu kwa kipindi chote hicho. Yapo
mafanikio mengi yanayotokana na Muungano, lakini makubwa kati ya mafanikio hayo ni kuwa na amani na utulivu katika
nchi yetu. Aidha, Muungano huu umeweza kutoa fursa ya kuendeleza na kuimarisha
mahusiano ya kidugu yaliyopo kati ya wananchi wa Tanzania Bara na Zanzibar.
20.0
Mheshimiwa Spika,
licha
ya kuwa na mafanikio hayo, Muungano wetu huu umekuwa na changamoto katika
baadhi ya maeneo ambazo zimekuwa zikipigiwa kelele na wananchi wa pande zote
mbili za Muungano. Juhudi kubwa tayari zimechukuliwa na viongozi wetu katika
kuzitafutia ufumbuzi changamoto hizo ili kuimarisha Muungano wetu huu wa
kihistoria. Mambo ambayo mpaka sasa yameshapatiwa ufumbuzi kupitia Kamati Maalumu
inayoongozwa na Mhe, Makamu wa Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania ni kama
yafuatayo:-
· Utekelezaji wa
Sheria ya Haki za Binaadamu.
· Utekelezaji wa “Merchant
Shipping Act” katika Jamhuri ya Muungano na uwezo wa Zanzibar kujiunga na
Shirika la Kimataifa la Usafiri Baharini [International Maritime Organisation
(IMO)].
· Misamaha ya
mikopo ya fedha kutoka IMF.
· Uwezo wa Zanzibar
kukopa ndani na nje nchi.
· Mfuko wa
Maendeleo ya Jimbo wa SMT.
· Kodi ya Mapato (Mgao
wa Mapato yatokanayo na PAYE).
21.0
Mheshimiwa Spika,
pamoja
na mambo ambayo yameshapatiwa ufumbuzi kuna mambo ambayo yapo katika hatua nzuri ya
kupatiwa ufumbuzi, mambo hayo ni kama
yafuatayo:-
· Mgawanyo wa
mapato yatokanayo na faida ya Benki Kuu.
· Utafutaji na
uchimbaji mafuta na gesi asili.
· Ushirikiano na
Zanzibar na Taasisi za nje.
· Ajira kwa
watumishi wa Zanzibar katika Taasisi za Muungano.
· Usajili wa vyombo
vya moto.
· Tume ya pamoja ya
fedha.
· Ushiriki wa
Zanzibar katika Jumuiya ya Afrika Mashariki.
HALI YA UCHUMI NA MIPANGO YA SERIKALI YA KUIMARISHA UCHUMI
22.0
Mheshimiwa Spika, Uchumi wa
Zanzibar umeendelea kuonesha mwenendo mzuri na umeendelea kukua kwa asilimia
7.4 mwaka 2013 kutoka asilimia 7.1 mwaka 2012. Uchumi huu umekua kwa kipindi cha miaka minne (4) kutoka asilimia
6.4 mwaka 2010 hadi kufikia asilimia 7.4 mwaka 2013. Pato la Taifa kwa bei za
miaka husika limefikia jumla ya Sh. 1,442.8 bilioni kwa mwaka 2013 kutoka Sh.
1,342.6 bilioni kwa mwaka 2012.
23.0
Mheshimiwa Spika,
mwaka
2013 pato la kila mtu limeongezeka kufikia wastani wa Sh. 1,077,000 (USD 667)
kutoka wastani wa Sh. 1,030,000 (USD 656) kwa mwaka 2012 sawa na ongezeko la
asilimia 4.3. Ukuaji huu mkubwa wa Uchumi umechangiwa na mambo yafuatayo:-
i. Kuimarika kwa
Sekta ya Kilimo, Misitu na Uvuvi ambayo imekua kutoka asilimia 2.0 mwaka 2012
hadi asilimia 3.6 mwaka 2013.
ii. Kuimarika kwa baadhi
ya Sekta ya Viwanda kulikochangiwa na ongezeko la ukuaji wa Sekta ndogo ya
uzalishaji viwandani kutoka asilimia 0.1 kwa mwaka 2012 hadi asilimia 3.2 mwaka
2013.
iii. Kuimarika kwa
Sekta ya huduma kulikochangiwa na ongezeko la ukuaji wa Sekta ndogo za Hoteli
na Mikahawa kutoka asilimia 0.2 mwaka 2012 hadi asilimia 6.5 mwaka 2013, Sekta
ya Utawala wa Umma kutoka asilimia 0.3 mwaka 2012 hadi asilimia 3.4, mwaka 2013
na Sekta ya Elimu kutoka asilimia 1.2 mwaka 2012 hadi asilimia 3.5 mwaka 2013.
iv. Kuongezeka kwa
idadi ya Watalii wanaoingia nchini kutoka Watalii 169,223 mwaka 2012 hadi
kufikia Watalii 181,301 mwaka 2013 sawa na ongezeko la asilimia 7.1.
24.0
Mheshimiwa Spika, mafanikio ya
kukua kwa Uchumi yanatokana pamoja na sababu zilizotajwa hapo juu,
na hali ya utulivu, amani na
mshikamano wa wananchi ambayo imejenga mazingira mazuri ya kuwekeza na kufanyakazi
kunakoleta tija kwa nchi.
UWEZESHAJI WANANCHI KIUCHUMI
25.0
Mheshimiwa Spika,
katika
jitihada za kuwainua wananchi kiuchumi, Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar
imeshazindua Mfuko wa Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi. Mfuko huo wenye thamani ya shilingi 1.1
bilioni utatoa mikopo kwa wananchi wa makundi mbalimbali yakiwemo kundi la
vituo vya kutotolea wajasiriamali, kundi la watu wenye ulemavu, kundi la
wanawake na kundi la vijana waliomaliza masomo katika vyuo na Skuli za
Sekondari. Pamoja na uzinduzi wa Mfuko huu juhudi nyengine za Serikali katika
kuwawezesha wananchi kiuchumi ni kuanzisha kituo cha kulelea na kutotoa
wajasiriamali (Incubator Centre), kuendeleza Kongano (Clusters) sita (6)
zilizopo na kuanzisha Kongano nyengine tofauti.
26.0
Mheshimiwa Spika, natoa wito kwa
wananchi waache ile taabia ya kuona kuwa ajira ni ile ya serikalini. Hivyo basi
tunawaomba watumie fursa zilizopo ili kuweza kujiajiri wenyewe na kuendeleza
maisha yao ya kila siku.
SEKTA YA HUDUMA ZA
KIUCHUMI
27.0
Mheshimiwa Spika,
katika
kuimarisha huduma za kiuchumi Serikali inaendelea na utekelezaji wa miradi
mbalimbali ya uimarishaji wa miundombinu ya usafiri ikiwemo miundombinu ya barabara,
Bandari na Viwanja vya Ndege. Kwa upande wa barabara, Serikali inaendeleza
ujenzi wa barabara mbalimbali Unguja na Pemba pamoja na kutafuta rasilimali kwa
ajili ya ujenzi na ukarabati wa barabara zinazoingia ndani ya mji wa Zanzibar.
28.0
Mheshimiwa Spika,
kuhusu
kuimarisha usafiri wa anga Serikali inaendelea na kukiimarisha Kiwanja cha
Ndege cha Kimataifa cha Abeid Amani
Karume Unguja na Uwanja wa Ndege wa Pemba kwa upanuzi wa njia za kurukia na
kuegeshea ndege na ujenzi wa majengo mapya ya abiria pamoja na uwekaji wa taa
katika kiwanja cha Pemba. Kwa upande wa Sekta ya Mawasiliano, Serikali
imekamilisha kuandaa Sera ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano Zanzibar
(TEHAMA) ambayo itatoa muongozo wa matumizi mazuri ya TEHAMA kwa Zanzibar.
Aidha, Serikali inaendelea kuziunganisha Wizara na Taasisi za Serikali katika Mkonga wa Mawasiliano na hadi sasa
jumla ya Wizara na Taasisi 56 kati ya 83 zimeshaunganishwa na Mkonga huo.
29.0
Mheshimiwa Spika, kukamilika kwa
Mradi wa kulaza waya mpya wa umeme wenye uwezo wa kuchukua “MegaWatts” 100 na
mradi wa uimarishaji wa miundombinu ya ndani ya umeme imeimarisha upatikanaji wa huduma za umeme nchini na
kutoa muelekeo kwa kuendelea kukua kwa uchumi wa Zanzibar kwani uwekezaji hasa
katika maeneo ya Viwanda, Utalii na Biashara utaongezeka kwa kuwepo umeme wa
uhakika. Pamoja na hatua hii iliyofikiwa ya kupatikana kwa umeme, Serikali kwa
kushirikiana na Washirika wa Maendeleo inafanya uchambuzi yakinifu (Feasibility
Study) katika masuala ya nishati mbadala ikiwemo umeme. Pia, hivi sasa Serikali imo katika kuandaa
wataalam wa gesi na mafuta ili kuweza kukabiliana na upungufu wa wataalam wa
fani ya nishati ikiwemo utafutaji na uchimbaji wa mafuta hapa nchini.
SEKTA YA HUDUMA ZA JAMII
30.0
Mheshimiwa Spika,
maji
ni rasilimali ya kimaumbile na ya msingi ambayo ni muhimu kwa kuendeleza
maisha. Umuhimu wa matumizi yake
unaonekana kwenye mahitaji ya majumbani, viwandani na matumizi mengine mbalimbali
ya kijamii. Serikali inaendelea na
mipango ya kuwapatia wananchi maji safi na salama. Mipango hiyo ni pamoja na
uhuishaji, upanuzi na usambazaji wa maji mijini na vijijini inayohusisha
uchimbaji wa visima zaidi ya 50, ujenzi wa matangi ya maji, ununuzi na uwekaji
wa pampu mpya, ulazaji wa mabomba, ujenzi wa vibanda vya kuwekea pampu za maji
na ufungaji wa mita kwa wateja.
31.0
Mheshimiwa Spika,
katika
kuendeleza upatikanaji na utoaji wa huduma ya maji kwa wananchi, Serikali
inaendelea na mipango yake ya kulinda na kuhifadhi vyanzo vya maji kwa kujenga
uzio katika vyanzo mbalimbali vya maji na kusogeza karibu huduma za malipo ya
maji kwa wananchi kwa kujenga vituo vya kulipia maji katika sehemu mbalimbali
nchini.
32.0
Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea kuwaomba wananchi kuthamini mipango
mbalimbali ya kuimarisha upatikanaji wa maji kwa kuongeza ulinzi kwenye
miundombinu ya maji na uhifadhi wa vyanzo vya maji kwa kupanda miti.
33.0
Mheshimiwa Spika, kwa upande wa
sekta ya Elimu, Serikali inaendelea na juhudi zake za kuwapatia elimu bora
wananchi wa Zanzibar. Juhudi hizo ni pamoja na kujenga majengo ya kisasa kwa
skuli za Sekondari na Msingi katika Wilaya za Unguja na Pemba, kuajiri walimu
zaidi ya 700 walio na Shahada na Stashahada katika masomo ya Sayansi kwa mwaka
2014/2015. Aidha, Serikali inaendelea kutoa mafunzo kazini kwa Walimu yakiwemo
ya matumizi ya Lugha ya Kiingereza kwa kufundishia na mafunzo ya matumizi ya
Kompyuta. Vilevile Serikali itanunua Vifaa vya Maabara kwa Skuli 100 za
Sekondari na Kompyuta kwa Skuli mbili zenye Mchepuo wa Sayansi ya Kompyuta.
Pia, juhudi hizo za kuimarisha ubora wa elimu ni pamoja na kuandika na
kuchapisha Vitabu vya kiada na Miongozo ya Walimu wa Madarasa ya Tano hadi
Darasa la Saba. Serikali vilevile imepanga kuimarisha matumizi ya Teknolojia ya
Habari na Mawasiliano (TEHAMA) katika elimu kwa kuziunganisha Taasisi za elimu
na Mkonga wa Taifa na kuendelea na juhudi za kutumia Teknolojia hii kama nyenzo
ya kufundishia na kujifunza.
34.0
Mheshimiwa Spika, kwa upande wa
Sekta ya Afya, Serikali inaendelea na azma yake ya kuhakikisha wananchi wa
Zanzibar wanapata huduma bora ya afya ili kufikia malengo ya Dira ya mwaka
2020. Katika kufikia azma hiyo, Serikali imeweka mikakati mbalimbali ikiwa ni
pamoja na kuimarisha mifumo ya utoaji wa huduma za afya kwa kuzingatia makundi
maalum, kutumia mfumo mpya wa ununuzi wa dawa kupitia Mfumo wa Ununuzi wa Dawa
kwa Awamu (Framework Contract). Aidha,
Serikali imepanga kuongeza juhudi za kupata madaktari bingwa katika magonjwa
mbalimbali na kuwa na vifaa tiba vya kutosha ili kuweza kutoa huduma
zinazohitajika.
MIGOGORO YA ARDHI
35.0
Mheshimiwa Spika,
Serikali
bado inaendelea kulitafutia ufumbuzi wa kudumu suala la migogoro ya ardhi. Kwa
kiasi kikubwa hali hii inatokana na tabia ya wananchi na baadhi ya viongozi
kuuza au kukodisha ardhi bila kufuata sheria na taratibu ziliopo nchini. Mhe.
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi tayari amelitolea maagizo
mara kadhaa suala hili kwa kuwataka viongozi na wananchi kutojihusisha na mambo
yoyote yanayopelekea kuwa na migogoro ya ardhi.
36.0
Mheshimiwa Spika, hata hivyo,
Serikali inaendelea kuchukua juhudi mbalimbali ili kuhakikisha kuwa migogoro ya
ardhi inapatiwa ufumbuzi wa kudumu kupitia vyombo vyake mbalimbali ikiwemo
Mahakama ya Ardhi pamoja na Ofisi ya Mrajis wa Ardhi inayoshughulikia usajili
wa ardhi na kuwatambua wenye haki ya matumizi ya ardhi husika. Naomba
kusisitiza kwa kuwasihi viongozi katika ngazi zote na wananchi kwa ujumla
kuacha kujiingiza katika mambo ambayo yanasababisha kutokea kwa migogoro ya
ardhi.
MASUALA MTAMBUKA
UKIMWI
37.0 Mheshimiwa
Spika, Serikali inaendelea na juhudi
za kupambana na maradhi ya UKIMWI. Kwa kupitia Mipango na Programu mbalimbali
juhudi zinaelekezwa katika kutoa elimu na kudhibiti maambukizi mapya. Aidha, Serikali
inaendelea kuwaelimisha wananchi kuacha kuwanyanyapaa wale wote ambao kwa
bahati mbaya tayari wameshapata maambukizi ya virusi vinavyosababisha UKIMWI.
Watu Wenye
Ulemavu
38.0
Mheshimiwa Spika,
Serikali
inasimamia utekelezaji wa Mkakati wa kuwapatia haki watu wenye ulemavu na
kuwajumuisha katika masuala mbalimbali ya kiuchumi, kijamii na kisiasa. Kwa
sasa kumezuka wimbi kubwa la ubakaji wa watu wenye ulemavu. Serikali
itahakikisha kuwa wale wote wanaohusika na vitendo hivi vya udhalilishaji
wanapatikana na kuchukuliwa hatua kali kwa mujibu wa sheria. Watu wenye ulemavu
ni binaadamu kama binaadamu wengine hivyo wanastahiki haki na usawa katika jamii kwa nyanja zote.
Tusisahau kuwa na sisi pia ni walemavu watarajiwa.
Mapambano Dhidi ya Dawa za Kulevya
39.0
Mheshimiwa Spika, madawa ya
kulevya ni moja ya matatizo makubwa ya kiuchumi na kijamii duniani kwa sasa
kutokana na athari wanazozipata watumiaji wa dawa hizo ambao wengi wao ni
vijana. Zanzibar nayo inakabiliwa na tatizo kubwa la uingizwaji na matumizi ya
dawa za kulevya. Janga hili limewakumba vijana wengi ambao ni tegemeo la nchi
katika maendeleo ya kiuchumi na kijamii. Serikali itasimamia utekelezaji wa
Sheria ya Dawa za Kulevya na kudhibiti njia zote za uingizwaji wa dawa hizo na
kuwachukulia hatua kali za kisheria wale wote wanaohusika na uingizaji na utumiaji
wa dawa hizo. Aidha, Serikali itaendelea kutoa elimu kwa wananchi wote juu ya
madhara ya matumizi ya dawa za kulevya na kuwasaidia wale wote walioacha
matumizi ya dawa hizo. Serikali inazidi kutoa wito kwa wananchi kuachana na
tabia ya kuingiza na kutumia dawa za kulevya ili kuinusuru nchi na janga hili.
Mazingira
40.0
Mheshimiwa Spika,
suala
la kutunza mazingira lina umuhimu mkubwa sana katika kuleta maendeleo ya
kiuchumi na kijamii na kupunguza umasikini wa wananchi. Suala la mabadiliko ya
tabianchi pia limeendelea kuleta athari mbalimbali za kimazingira katika maeneo
yetu. Katika kuendeleza juhudi ya kukabiliana na hali ya uharibifu wa mazingira
na mabadiliko ya tabianchi, Serikali itasimamia sheria na kanuni za utunzaji wa
maliasili zisizorejesheka, kutoa elimu juu ya utunzaji wa mazingira na
kusimamia utekelezaji wa mkakati wa mabadiliko ya tabianchi ikiwa ni pamoja na
masuala ya mabadiliko ya tabianchi kuingizwa katika mipango ya maendeleo ya sekta mbalimbali nchini.
41.0
Mheshimiwa Spika,
Serikali
itaendelea kusimamia utekelezaji wa Programu ya upandaji miti katika maeneo
mbalimbali ikiwemo katika vyanzo vya maji, misitu ambayo imeathirika na ukataji
miti na maeneo ya wazi yaliyoathirika na ukataji wa miti ovyo. Ni vyema
wananchi wakazingatia suala zima la utunzaji wa mazingira kwani athari zake kwa nchi ya kisiwa kama Zanzibar ni kubwa.
SEKTA YA UTUMISHI
NA MASLAHI YA WAFANYAKAZI
42.0
Mheshimiwa Spika, Moja ya
vipaumbele vya Serikali ya Awamu ya
Saba (7) ni kuimarisha sekta ya utumishi wa umma na maslahi ya wafanyakazi
ikiwa na lengo la kuwepo kwa ufanisi na uwajibikaji katika utendaji wa shughuli
za utumishi, uadilifu na usimamizi mzuri wa rasilimali za umma. Ili kufikia
lengo hili serikali imetekeleza mageuzi makuu ya msingi yakiwemo mageuzi ya
utumishi wa umma na kuimarisha serikali katika masuala ya uwajibikaji na
uongozi.
43.0
Mheshimiwa Spika,
mageuzi
haya yamejumuisha mambo yafuatayo:
i. Kufanya tathmini
na ufuatiliaji wa utekelezaji wa Miundo ya Utumishi wa Wizara, Idara na Taasisi
zote za Serikali.
ii. Kuimarisha
utendaji wa taasisi za umma ikiwemo miundombinu, mifumo ya utoaji huduma,
kusimamia na kuendeleza watumishi wa umma pamoja na mageuzi ya Serikali za
mitaa.
iii. Kufanya Tathmini
ya Uchambuzi wa Kazi na Madaraja (Job Evaluation and Grading).
iv. Kufanya tathmini
ya idadi ya watumishi wa umma na majukumu yaliyopo.
v. Kuandaa Mpango
Mkakati wa Sera ya Malipo na Sera ya Uhifadhi Kumbukumbu na Nyaraka.
44.0
Mheshimiwa Spika,
pamoja
na mipango hiyo Serikali itaendelea kutoa umuhimu kwa mafunzo kwa Watumishi wa
Umma kwa kuwapatia mafunzo ya muda mrefu, muda mfupi na semina elekezi ili
kuwajengea uwezo wafanyakazi katika kutekeleza majukumu yao. Aidha, Serikali
imefanya marekebisho makubwa ya mishahara, kwa kuongeza mishahara ya
wafanyakazi kwa mujibu wa viwango vya elimu na uzoefu kazini.
MWELEKEO WA VIPAUMBELE VYA OFISI YA MAKAMU WA PILI WA RAIS KWA MWAKA
WA FEDHA 2014/2015
45.0
Mheshimiwa Spika Ofisi ya Makamu
wa Pili wa Rais katika kutekeleza majukumu yake katika mwaka wa fedha 2014/2015
imejipangia kutekeleza vipaumbele vifuatavyo:
i.
Kuimarisha huduma za usafiri na makaazi ya Mheshimiwa
Makamu wa Pili wa Rais.
ii.
Kuongeza hadhi katika Sherehe na Maadhimisho ya Kitaifa.
iii.
Kujenga uwezo wa kiutendaji kwa wafanyakazi wa Ofisi ya
Makamu wa Pili wa Rais kwa kuwapatia mafunzo na vitendea kazi.
iv.
Kujenga uwezo wa jamii katika kujikinga, kukabiliana na
kuhimili majanga na maafa.
v.
Kushughulikia malalamiko na migogoro ya wananchi kwa
kushirikiana na Sekta husika.
vi.
Kusimamia masuala ya utafiti kwa kuzingatia vipaumbele vya
Taifa vya Utafiti (National Research Agenda).
vii.
Kuweka Muundo mpya wa Kitaasisi na Kiutumishi wa Ofisi ya
Uratibu wa Shughuli za Serikali Dar es Salaam utakaoongeza ufanisi na tija.
viii.
Kuongeza mapato yatokanayo na kuongezeka kwa huduma za
upigaji chapa.
ix.
Kuandaa mazingira bora kwa ajili ya kufanikisha Uchaguzi
Mkuu wa 2015, ikiwemo kutoa elimu ya Wapiga Kura, kufanya uchunguzi wa idadi, majina
na mipaka ya majimbo na kufanya mapitio ya Daftari la Kudumu la Wapiga Kura.
x.
Kuendesha mikutano ya Baraza la Wawakilishi na kusimamia
kazi za Kamati za Kudumu za Baraza.
UTEKELEZAJI WA
MALENGO KWA MWAKA WA FEDHA 2013/2014 NA MALENGO YALIYOPANGWA KWA MWAKA WA FEDHA
2014/2015
46.0
Mheshimiwa Spika,
katika
mwaka wa fedha 2013/2014, Ofisi ya Makamu wa Pili
wa Rais na Taasisi zake ilikadiriwa kutumia jumla ya Sh. 30,066,506,000. Kati ya hizo Sh. 22,094,970,000
ni kwa kazi za kawaida na Sh. 7,971,536,000 ni kwa kazi za maendeleo. Hadi
kufikia mwezi Machi 2014, Ofisi iliingiziwa Sh. 19,416,893,755 (sawa na
asilimia 65). Kati ya hizo Sh. 15,837,895,300 ni kwa kazi za kawaida (sawa na
asilimia 72) na Sh. 3,578,998,455 kwa kazi za maendeleo (sawa na asilimia 45). [Kiambatanisho Nam. 1A na 1B].
47.0
Mheshimiwa Spika, baada ya kutoa
taarifa za jumla za utekelezaji kifedha kwa mwaka 2013/2014, sasa naomba kutoa
taarifa za utekelezaji kwa kila idara na taasisi zilizo chini ya Ofisi ya
Makamu wa Pili wa Rais.
OFISI YA FARAGHA YA
MAKAMU WA PILI WA RAIS
48.0
Mheshimiwa Spika, Ofisi ya Faragha ina jukumu la
kutoa huduma zote muhimu kwa Mhe. Makamu
wa Pili wa Rais na familia yake pamoja na kutunza makaazi ya Makamu wa Pili wa
Rais yaliyoko Mazizini Unguja, Dar es Salaam na Dodoma.
49.0
Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa
fedha 2013/2014 Baraza lako Tukufu liliidhinisha jumla ya Sh. 780,034,000 kwa
Idara ya Faragha. Hadi kufikia mwezi
Machi, 2014 Idara iliingiziwa jumla ya Sh. 317,824,974 kwa ajili ya kazi za
kawaida ambazo ni sawa na asilimia 41.
50.0
Mheshimiwa Spika, katika mwaka
2013/2014 Ofisi ya Faragha imetekeleza kazi zifuatazo:-
i. Ofisi imefanya
ununuzi wa vifaa muhimu vya kuendeshea ofisi, matengenezo ya magari na vifaa na
kulipia huduma ya simu na faksi.
ii. Matengenezo
madogo madogo yamefanywa kwa makaazi ya Mhe. Makamu wa Pili wa Rais ya Dar es
Salaam na kulipia huduma muhimu kwa makaazi ya Unguja, Dares-Salaam na Dodoma.
iii. Ofisi imeratibu
mikutano ya Mheshimiwa Makamu wa Pili wa Rais na Mabalozi na Wanadiplomasia 11
ikiwemo Marekani, Kenya, Israel, Malaysia, Nigeria, India, China waliopo nchini
Tanzania na ujumbe wa Serikali ya Oman.
iv. Ofisi imeratibu
ziara 15 za ndani ya nchi [Pemba saba (7), Dar-es-Salaam tano (5), Dodoma moja
(1) na Arusha mbili (2)] na ziara mbili (2) za nje (Marekani na Falme za Nchi
za Kiarabu) za Mheshimiwa Makamu wa Pili wa Rais.
v. Ofisi imeratibu
mazungumzo ya upatanishi wa migogoro ya wananchi ambapo mgogoro wa mpaka wa
wananchi wa Donge Muwanda tayari umetatuliwa.
Aidha, mgogoro wa wananchi wa Kiombamvua na muwekezaji wa hoteli ya Sea
Cliff iliyopo Kama Wilaya ya Kaskazini “B” umefikia katika hatua nzuri ambapo
bado Serikali inaendelea kuufanyia kazi kutokana na matatizo mapya yaliyojitokeza
kwa utaratibu maalum.
vi. Ofisi imeratibu
na kufuatilia ahadi 11 zilizotolewa na Mheshimiwa Makamu wa Pili wa Rais kati
ya hizo ahadi saba (7) zimetekelezwa
51.0
Mheshimiwa Spika katika mwaka wa
fedha 2014/2015 Ofisi ya Faragha imepanga kutekeleza malengo yafuatayo:-
i.
Kuimarisha Ofisi ya Faragha ya Makamu wa Pili wa Rais kwa
ununuzi wa gari moja, samani na vifaa vya ofisi.
ii.
Kuratibu ziara 20 za ndani ya nchi na mbili za nje ya nchi
za Mheshimiwa Makamu wa Pili wa Rais.
iii.
Kuwajengea uwezo wafanyakazi wawili (2) wa Idara kwa
kuwapatia mafunzo ya muda mfupi na muda mrefu pamoja na kulipa stahiki za
likizo kwa wafanyakazi wanne (4).
iv.
Kuimarisha makaazi ya Mheshimiwa Makamu wa Pili wa Rais
kwa kuzifanyia matengenezo nyumba za Mazizini, Dar es Salaam na Dodoma.
v.
Kuimarisha uhusiano na ushirikiano na nchi na taasisi
mbalimbali za ndani, kikanda na kimataifa.
52.0
Mheshimiwa Spika, ili Ofisi ya
Faragha iweze kutekeleza malengo yake kwa mwaka wa fedha 2014/2015 naliomba
Baraza lako Tukufu liidhinishe jumla ya Sh 483,116,224 kwa matumizi ya Ofisi.
Kati ya hizo Sh 330,616,224 kwa malipo ya mishahara, posho za wafanyakazi na
michango ya Mfuko wa Hifadhi ya Jamii na Sh 152,500,000 kwa matumizi mengineyo.
IDARA YA UENDESHAJI
NA UTUMISHI
53.0
Mheshimiwa Spika,
Idara
ya Uendeshaji na Utumishi ina wajibu wa kusimamia stahiki za watumishi wa Ofisi
ya Makamu wa Pili wa Rais na kusimamia mafunzo kwa wafanyakazi. Aidha, Idara
ina jukumu la kusimamia usalama na mazingira bora ya kazi pamoja na uendeshaji
wa kazi za kila siku za Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais.
54.0
Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa
fedha 2013/2014 Baraza lako Tukufu liliidhinisha jumla ya Sh. 1,004,880,000 kwa
Idara ya Uendeshaji na Utumishi. Hadi kufikia mwezi Machi, 2014 Idara iliingiziwa
jumla ya Sh. 577,298,515 kwa kazi za
kawaida ambazo ni sawa na asilimia 57.
55.0
Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa
fedha 2013/2014 Idara ya Uendeshaji na Utumishi imetekeleza kazi zifuatazo:-
i. Idara imeendelea
kuratibu na kuwalipia ada na gharama nyengine za masomo kwa wafanyakazi 66 wanaoendelea
na masomo ndani na nje ya nchi. (Kiambatanisho Nam. 2)
ii. Kulipia stahiki
za wafanyakazi zikiwemo likizo kwa wafanyakazi saba (7), malipo baada ya saa za
kazi na kutayarisha mafao kwa watumishi sita (6) waliostaafu.
iii. Idara imefanya
semina elekezi kuhusu Sheria ya Utumishi wa Umma ya mwaka 2011 na elimu ya
kujikinga na maambukizi mapya ya UKIMWI.
iv. Idara imenunua
vifaa vya kufanyia kazi ikiwemo mashine ya kurudufia (photocopy) na “projector”
moja kwa lengo la kujenga mazingira bora ya kazi.
v. Idara imeweza
kudhamini wafanyakazi 46 kupata mikopo
ya kifedha yenye thamani ya Sh. 202,137,540 katika taasisi mbali mbali za
kifedha.
56.0
Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa
fedha 2014/2015 Idara ya Uendeshaji na Utumishi imepanga kutekeleza malengo
yafuatayo:-
i.
Kuweka mazingira mazuri ya kazi za idara kwa ununuzi wa
vifaa vya ofisi, samani pamoja na kulipia gharama za umeme na mawasiliano na
utunzaji wa majengo.
ii.
Kuwajengea uwezo wafanyakazi kumi (10) wa idara kwa
kuwapatia mafunzo ya muda mfupi na muda mrefu pamoja na kulipa stahiki za
likizo kwa wafanyakazi tisa (9).
iii.
Kuufanyia mapitio Mpango wa Mafunzo kwa wafanyakazi pamoja
na kuandaa utaratibu wa kutathmini utendaji kazi (Staff Appraisal System) na
upandishaji vyeo wafanyakazi kwa kufuata muundo wa utumishi (Scheme of Service).
iv.
Kusimamia matumizi bora ya fedha na vifaa vya ofisi kwa
kuandaa vikao vinne (4) vya Kamati ya Uongozi, vikao vinne (4) vya Bodi ya
Zabuni, Vikao vinne (4) vya Kamati ya Ukaguzi wa ndani na kulifanyia mapitio
Daftari la Mali za Serikali (Asset Registry).
57.0
Mheshimiwa Spika, ili idara ya
Uendeshaji na Utumishi iweze kutekeleza malengo yake kwa mwaka wa fedha 2014/2015 naliomba
Baraza lako tukufu liidhinishe jumla ya Sh. 704,166,316. Kati ya hizo Sh. 514,166,316
ni kwa malipo ya mishahara, posho na mchango
wa Mfuko wa Hifadhi ya Jamii na Sh. 190,000,000 ni kwa matumizi mengineyo.
IDARA YA MIPANGO, SERA NA UTAFITI
58.0
Mheshimiwa Spika, Idara ya Mipango, Sera na
Utafiti inaendelea na jukumu la kusimamia masuala ya mipango, bajeti, sera na
utafiti. Pia Idara hii ina jukumu la
kufuatilia na kutathmini utekelezaji wa miradi ya maendeleo pamoja na
kutayarisha ripoti za utekelezaji wa shughuli za kawaida na miradi ya maendeleo
kwa kipindi cha miezi mitatu, miezi sita, miezi tisa na mwaka mzima.
59.0
Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa
fedha 2013/2014 Baraza lako Tukufu liliidhinisha jumla ya Sh. 295,240,000 kwa
Idara ya Mipango, Sera na Utafiti. Hadi kufikia mwezi Machi, 2014 Idara
iliingiziwa jumla ya Sh. 125,771,732 kwa kazi za kawaida ambazo ni sawa na asilimia
43.
60.0
Mheshimiwa Spika, Idara ya Mipango, Sera na Utafiti
katika mwaka wa fedha wa 2013/2014 imetekeleza kazi zifuatazo:-
i.
Idara imelipa stahiki za wafanyakazi wanne (4) waliokwenda
likizo.
ii.
Idara imefanya semina ya siku mbili kwa wafanyakazi juu ya
Sheria ya Utumishi wa Umma.
iii.
Idara imenunua vifaa vya kufanyia kazi ikiwemo Projekta
moja (1), Printa moja (1) na vifaa vya kuandikia.
iv.
Idara imefanya ziara ya ukaguzi wa miradi ya maendeleo
iliyo chini ya Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais.
v.
Idara imeratibu utekelezaji wa Miradi ya Mfuko wa Dunia
(Global Fund) ya Kupambana na UKIMWI, Kifua Kikuu na Malaria.
vi.
Idara imeandaa Mpango Mkakati wa Ofisi ya Makamu wa Pili
wa Rais.
vii.
Idara imeandaa Bajeti na Hotuba ya Bajeti ya Ofisi ya
Makamu wa Pili wa Rais kwa mwaka wa fedha 2014/2015.
viii.
Idara imeandaa ripoti za utekelezaji kwa shughuli za
kawaida na Miradi ya maendeleo kwa robo mwaka, nusu mwaka na miezi tisa. Pia
imefanya vikao vya kupitia na kutathmini ripoti hizo.
ix.
Idara imetoa vibali 110 vya kufanya utafiti katika sekta za
mazingira, historia, kilimo, maliasili, misitu na elimu. Aidha, Idara imeratibu
vikao vinne; viwili vya Kamati ya Taifa ya Utafiti na viwili kwa Kamati ya
Wataalamu ya Kutafiti Rasilimali za Asili.
x.
Idara kwa kushirikiana na COSTECH imetekeleza kazi zifuatazo:-
§ Imeratibu kikao
cha Kamati ya Taifa ya Wataalamu ya Rasilimali za Asili juu ya kupitia vipaumbele
vya utafiti (National Research Agenda).
§ Imeratibu mkutano
wa siku tatu wa mashirikiano baina ya Afrika ya Kusini na Tanzania juu ya masuala
ya Utafiti.
§ Idara kwa
kushirikiana na COSTECH, SUZA na Chuo Cha Sayansi ya Afya imeratibu na
kushiriki Siku ya Utafiti na Ugunduzi ikiwa ni moja ya shughuli za maadhimisho
ya sherehe za Miaka 50 ya Mapinduzi ya Zanzibar.
61.0
Mheshimiwa Spika, Kwa mwaka wa fedha wa 2014/2015
Idara ya Mipango, Sera na Utafiti
imepanga kutekeleza malengo yafuatayo:-
i.
Kuweka mazingira mazuri ya kazi za idara kwa ununuzi wa
vifaa vya ofisi na samani.
ii.
Kuwajengea uwezo wafanyakazi 11 wa idara kwa kuwapatia mafunzo
ya muda mfupi na wafanyakazi watatu (3) kwa mafunzo ya muda mrefu na kulipa
stahiki za likizo kwa wafanyakazi watatu (3)
iii.
Kuufanyia mapitio Mpango Mkakati wa Ofisi ya Makamu wa
Pili wa Rais na kutayarisha Miradi mitatu ya Maendeleo
iv.
Kuandaa Bajeti kwa
Mwaka wa Fedha 2015/2016 na kufanya ziara nne (4) za ufuatiliaji wa kazi za
Wizara na utekelezaji wa Miradi ya
Maendeleo ya Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais
v.
Kuandaa vikao 12 vya Kamati ya Kisekta ya kuidhinisha Tafiti mbalimbali na Vikao vinne vya Kamati ya Taifa ya Kutafiti Rasilimali za
Asili
vi.
Kwa kushirikiana na COSTECH kuwajengea uwezo watafiti wa wizara za SMZ
kwa kuandaa warsha mbili pamoja na
kuweka utaratibu mzuri wa utoaji wa
vibali vya Utafiti
vii.
Kuratibu utekelezaji wa Miradi ya Mfuko wa Dunia (Global
Fund) ya Kupambana na UKIMWI, Kifua Kikuu na Malaria
62.0
Mheshimiwa
Spika, Ili Idara ya Mipango, Sera na Utafiti iweze kutekeleza malengo yake
katika mwaka wa fedha 2014/2015 naliomba Baraza lako Tukufu kuidhinisha jumla
ya Sh 184,007,400 kwa matumizi ya Idara.
Kati ya hizo Sh. 100,718,400 kwa ajili ya malipo ya mishahara, posho za
wafanyakazi na mchango wa Mfuko wa Hifadhi ya Jamii na Sh. 83,289,000 kwa
matumizi mengineyo.
IDARA YA URATIBU WA
SHUGHULI ZA SERIKALI
63.0
Mheshimiwa Spika, Idara ya Uratibu wa Shughuli za
Serikali ina jukumu la kuratibu Shughuli za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar
na Shughuli za Muungano ndani ya Zanzibar.
64.0
Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2013/2014
Baraza lako Tukufu liliidhinisha jumla ya Sh. 397,530,000 kwa Idara ya Uratibu
wa Shughuli za Serikali. Hadi kufikia mwezi Machi, 2014 Idara iliingiziwa jumla
ya Sh. 223,282,110 kwa kazi za kawaida ambazo ni sawa na asilimia 56. Aidha,
Idara iliidhinishiwa Sh. 840,000,000 kwa kazi za maendeleo ikiwa ni mchango wa
SMZ. Kati ya hizo Sh. 80,000,0000 ni kwa Mradi wa TASAF na Sh. 760,000,000 kwa
Mfuko wa Maendeleo ya Jimbo. Hadi kufikia Machi, 2014, Idara imeingiziwa Sh. 25,
000,000 kwa mradi wa TASAF, sawa na asilimia 31.
65.0
Mheshimiwa Spika, katika mwaka
2013/2014 Idara imetekeleza kazi zifuatazo:-
i.
Idara imefuatilia utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya
Chama Cha Mapinduzi ya mwaka 2010 – 2015 katika Wizara za SMZ na Mikoa yote ya
Unguja na Pemba na kuandaa taarifa ya utekelezaji kwa kipindi cha mwaka mmoja (Oktoba
2012 – Septemba 2013).
ii.
Idara imetoa mafunzo ya kuwajengea uwezo wa kukusanya na
kuandaa taarifa za utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi kwa Maafisa
viungo wa Wizara, Maafisa Mipango wa Mikoa pamoja na Waratibu wa Ofisi ya
Makamu wa Pili wa Rais.
iii.
Idara imepokea na inaendelea kuyafuatilia malalamiko 15
(10 yanayohusiana na ardhi na 5 mambo mengine) yaliyowasilishwa na wananchi.
iv.
Idara imeendelea kufuatilia utekelezaji wa ahadi nane (8) za
Viongozi Wakuu wa Kitaifa zilizotolewa katika maeneo mbalimbali ya Unguja na
Pemba wakati wa ziara zilizofanywa na viongozi hao.
v.
Idara imefuatilia
vikao vitatu (3) vya Baraza la Wawakilishi vilivyofanyika katika mwezi wa Oktoba Mkutano wa 14, Disemba Mkutano wa 15 na
Januari Mkutano wa 16, Katika Mikutano
hiyo jumla ya masuali 221 ya msingi yaliulizwa na kujibiwa. Pia, miswada Saba
(7), Ripoti moja ya Kamati Teule na hoja binafsi moja ziwasilishwa.
vi.
Idara imeratibu vikao saba (7) vya mashirikiano baina ya
Wizara za SMZ na SMT ambapo vikao vitatu (3) vimefanyika baina ya Wizara ya
Elimu na Mafunzo ya Amali SMZ na Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi SMT,
vikao vitatu (3) baina ya Wizara ya Kilimo na Maliasili SMZ na Wizara ya
Kilimo, Chakula na Ushirika SMT, kikao kimoja (1) baina ya Ofisi ya Mwanasheria
Mkuu SMZ na SMT.
vii.
Idara imeendelea kulipia ada na gharama nyengine za masomo
ya muda mrefu kwa wafanyakazi sita (6) na masomo ya muda mfupi kwa wafanyakazi
watatu (3) ndani na nje ya nchi.
viii.
Idara imesimamia utekelezaji wa mradi wa TASAF Awamu ya
Tatu (Mpango wa Kunusuru Kaya Masikini) na kaya masikini 2,675 kwa Unguja na
Kaya 4,084 kwa Pemba zimepatiwa malipo
kwa awamu mbili (Januari na Machi 2014). Jumla ya Sh. 432,259,000 zimelipwa kwa
Unguja na Pemba. (Kiambatanisho Nam. 3A-3F)
ix.
Idara iliandaa semina kwa Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi
kwa lengo la kuwapatia uwelewa wajumbe hao kuhusu utekelezaji wa Mradi wa TASAF
awamu ya Tatu.
x.
Idara imeratibu ziara za mafunzo kwa Wakuu wa Mikoa na Wakuu wa Wilaya zote wa
Unguja na Pemba pamoja na Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Baraza la Wawakilishi
ya Kusimamia Ofisi za Viongozi Wakuu wa Kitaifa waliotembelea eneo la mfano la
utekelezaji wa Mradi wa TASAF awamu ya Tatu huko Bagamoyo - Tanzania Bara.
xi.
Idara imetoa mafunzo maalumu kwa wawezeshaji 120 kutoka
Wilaya zote za Unguja na Pemba (Unguja 60 na Pemba 60) wa kuibua kaya masikini.
xii.
Idara imeandaa Rasimu ya Kanuni ya Sheria ya Mfuko wa
Maendeleo ya Jimbo.
xiii.
Idara imefuatilia utekelezaji wa miradi ya Mfuko wa
Maendeleo ya Jimbo kwa Majimbo yote 50 ya Unguja na Pemba. Katika ufuatiliaji huo Kamati za kusimamia
miradi hiyo zimehimizwa kufanya marejesho ya utekelezaji wa miradi hiyo.
xiv.
Idara imetoa mafunzo kuhusu utekelezaji wa Sheria ya Mfuko
wa Maendeleo ya Jimbo ya mwaka 2012 kwa Makatibu wa Kamati za Mfuko wa
Maendeleo ya Jimbo kwa majimbo yote 18
ya Pemba pamoja na Maafisa Mipango wa Mikoa na Wilaya za Pemba.
xv.
Idara inaendelea kukiimarisha Kitengo cha Habari,
Mawasiliano na Elimu (ICE) kwa kununua vifaa na kutoa mafunzo kwa watendaji wa
Kitengo hicho.
xvi.
Tovuti ya Serikali imeimarishwa kwa kuwekwa taarifa mbali
mbali za Mawizara na matukio muhimu ikiwemo maadhimisho ya Sherehe mbali mbali
za kitaifa na hotuba za Viongozi Wakuu.
66.0
Mheshimiwa
Spika, katika mwaka wa fedha 2014/2015 Idara imepanga kutekeleza malengo yafuatayo:-
i. Kuweka mazingira
mazuri ya kazi za Idara kwa ununuzi wa vifaa vya ofisi na samani.
ii. Kuwajengea uwezo
wafanyakazi wanne (4) wa Idara kwa kuwapatia mafunzo ya muda mfupi na muda
mrefu pamoja na kulipa stahiki za likizo kwa wafanyakazi saba (7).
iii. Kufuatilia utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM na kuandaa
Taarifa ya utekelezaji kwa kipindi cha Miaka miwili kuanzia Oktoba 2012 –
Septemba 2014
iv. Kufuatilia
utekelezaji wa Ahadi za Viongozi Wakuu wa Kitaifa kwa kila robo mwaka
v. Kupokea na
kufuatilia malalamiko ya wananchi na kusimamia utatuzi wa migogoro katika
jamii.
vi. Kufuatilia na
kutathmini utekelezaji wa Miradi ya Mfuko wa Maendeleo ya Jimbo katika majimbo
50 ya Unguja na Pemba ambayo yamepatiwa fedha.
vii. Kufuatilia
mijadala na utekelezaji wa Ahadi za Serikali zinazotolewa katika vikao vya Baraza
la Wawakilishi.
viii. Kuratibu
vikao saba (7) vya mashirikiano kati ya
Wizara za SMZ na SMT
ix. Kuratibu vikao
vinne (4) vya Mawaziri na Makatibu wakuu wa SMZ na SMT na vikao vinne (4) vya
Sekretarieti ya Kamati ya Pamoja ya Mambo ya Muungano
x. Kusimamia utoaji
wa fedha (Cash Transfer) kwa Kaya masikini za Unguja na Pemba zinazotolewa
kupitia Mpango wa TASAF awamu ya Tatu.
xi. Kuimarisha
kitengo cha ICE kwa ununuzi wa vifaa vipya na kutoa mafunzo kwa watendaji sita
wa Kitengo.
67.0
Mheshimiwa Spika, Ili Idara iweze kutekeleza
majukumu yake kwa mwaka 2014/2015 naliomba Baraza lako Tukufu liidhinishe jumla
ya Sh. 344,638,000. Kati ya fedha hizo Sh. 247,053,000 kwa malipo ya mishahara,
posho za wafanyakazi na mchango wa Mfuko wa Hifadhi ya Jamii na Sh. 97,585,000 kwa
matumizi mengineyo. Kwa upande wa Miradi ya Maendeleo naliomba Baraza lako
Tukufu kuidhinisha jumla ya Sh. 1,060,000,000. Kati ya hizo Sh. 1,010,000,000 kwa
ajili ya Mfuko wa Maendeleo ya Jimbo na Sh. 50,000,000 mchango wa Serikali kwa ajili ya
Miradi ya Mfuko wa Maendeleo ya Jamii – TASAF awamu ya Tatu.
IDARA YA URATIBU WA SHUGHULI
ZA SMZ- DAR ES SALAAM.
68.0
Mheshimiwa Spika, Idara ya Uratibu
wa Shughuli za SMZ Dar es Salaam imehamishiwa rasmi katika Ofisi ya Makamu wa
Pili wa Rais tangu mwezi wa Septemba 2013. Kabla ya hapo Idara hii ilikuwa
chini ya Iliyokuwa Wizara ya Fedha, Uchumi na Mipango ya Maendeleo.
69.0
Mheshimiwa Spika, Idara hii inajukumu
la kuratibu kazi za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar huko Tanzania Bara. Aidha, Idara inaratibu masuala ya SMZ na Ofisi
za Balozi mbalimbali zilizopo Tanzania, Wadau wa Maendeleo pamoja na Mashirika
ya Kimataifa yenye ofisi zao Dar es Salaam.
70.0
Mheshimiwa Spika,
kwa
mwaka wa fedha 2013/2014 Baraza lako Tukufu liliidhinisha jumla ya Sh. 326,970,000
kwa Idara ya Uratibu wa Shughuli za SMZ Dar es Salaam. Hadi kufikia mwezi
Machi, 2014 Idara iliingiziwa jumla ya Sh. 119,053,550 kwa kazi za kawaida ambazo
ni sawa na asilimia 36.
71.0
Mheshimiwa Spika, Idara ya Uratibu
wa Shughuli za SMZ - Dar es Salaam katika mwaka wa fedha 2013/2014 imetekeleza
kazi zifuatazo:-
i. Idara ilishiriki
kwenye Mkutano wa Nane wa Tume ya pamoja ya Ushirikiano wa kiuchumi, kiufundi
na Sayansi baina ya Tanzania na India.
Ambapo India iliahidi kuipatia msaada SMZ katika kuimarisha huduma za
Afya.
ii. Idara ilishiriki
katika kikao cha mashauriano baina ya Tanzania na Japan, ambapo Zanzibar
iliwasilisha mapendekezo ya miradi saba kupitia Tume ya Mipango Tanzania Bara
kwa ajili ya kuombewa misaada kutoka Serikali ya Japan (TICAD V).
iii. Idara imeshiriki
katika kikao cha wadau kuhusiana na mpango mpya wa ushirikiano baina ya Tanzania
na Saudi Arabia, lengo likiwa ni kujenga ushirikiano baina ya nchi hizo mbili.
iv. Idara ilishiriki
katika vikao vya maandalizi ya Mkutano wa Wakuu wa nchi za Afrika na Ufaransa,
lengo ilikuwa ni kujadili mabadiliko ya tabianchi, ulinzi na usalama pamoja na
mashirikiano ya kiuchumi.
v. Idara ilishiriki
katika kikao cha wadau kuhusu mpango mpya wa ushirikiano kati ya Tanzania na
Uingereza, lengo kuu ni kujadili sera iliyotolewa na Serikali ya Uingereza na
kupendekezwa kuundwa kwa ubia wenye ustawi kati yake na Tanzania “Tanzania –
United Kingdom Partnership in Prosperity” kwenye maeneo ya: Nishati Jadilifu
(renewable enegy), kilimo na mazingira ya biashara.
vi. Idara ilishiriki
katika matayarisho ya Mkutano Mkuu wa Mawaziri unaojadili masuala ya kiuchumi
ambao ulifanyika nchini Kenya.
72.0
Mheshimiwa Spika,
kwa
mwaka wa fedha wa 2014/2015 Idara ya Uratibu wa shughuli za SMZ Dar es Salaam
imepanga kutekeleza malengo yafuatayo:-
i. Kuweka mazingira
mazuri ya kazi za Idara kwa ununuzi wa vifaa vya ofisi na samani
ii. Kuwajengea uwezo wafanyakazi
watatu (3) wa Idara kwa kuwapatia mafunzo ya muda mfupi na muda mrefu pamoja na
kulipa stahiki za likizo kwa wafanyakazi tisa (9).
iii. Kuandaa Muundo
mpya wa Kitaasisi na Kiutumishi wa Idara utakaoleta ufanisi zaidi na tija.
iv. Kuimarisha
mashirikiano baina ya Idara na Taasisi za SMZ na Taasisi za Serikali ya Jamhuri
ya Muungano, Ofisi za Kibalozi na Taasisi za Kimataifa.
73.0
Mheshiwa Spika, ili Idara ya
Uratibu wa Shughuli za SMZ Dar es Salaam iweze kutekeleza malengo yake katika
mwaka wa fedha 2014/2015 naliomba Baraza lako Tukufu kuidhinisha jumla ya Sh. 353,178,160. Kati
ya hizo Sh. 208,178,160 kwa ajili ya malipo ya mishahara, Posho za wafanyakazi
na mchango wa Mfuko wa Hifadhi ya Jamii na Sh. 145,000,000 kwa matumizi
mengineyo.
IDARA YA KUKABILIANA
NA MAAFA
74.0
Mheshimiwa Spika, Idara ya kukabiliana
na Maafa ina jukumu la kuratibu masuala ya maafa hapa Zanzibar, kama
ilivyoelezwa katika Sheria ya Kukabiliana na Maafa Nam. 2 ya mwaka 2003.
75.0
Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2013/2014
Baraza lako Tukufu liliidhinisha jumla ya Sh. 262,528,000 kwa Idara ya
Kukabiliana na Maafa kwa kazi za kawaida. Hadi kufikia mwezi Machi, 2014 Idara
iliingiziwa jumla ya Sh. 112,283,620 kwa kazi za kawaida ambazo ni sawa na
asilimia 43. Kwa upande wa miradi ya maendeleo Idara iliidhinishiwa Sh.
340,000,000. Kati ya hizo Sh. 70,000,000 ni mchango wa Serikali na Sh.
270,000,000 ni mchango kutoka kwa Washirika wa Maendeleo na hadi kufikia mwezi
wa Machi 2014, Idara imeingiziwa Sh.10,000,000 kutoka mchango wa Serikali sawa
na asilimia 14. na Sh. 175,176,000 kutoka kwa Washirika wa Maendeleo sawa na asilimia 65.
76.0
Mheshimiwa Spika, Idara ya
Kukabiliana na Maafa katika mwaka fedha wa 2013/2014 imetekeleza kazi kama ifuatavyo:
-
i. Idara imepatiwa
na Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP) gari moja, redio za
mawasiliano 10, pikipiki tatu (3) na kompyuta (laptop) nne (4).
ii. Idara
imetayarisha na kurusha vipindi 18 vya kukabiliana na maafa kwa lengo la
kuelimisha jamii kupitia ZBC Radio.
iii. Idara imetoa mafunzo
ya kukabiliana na maafa kwa Shehia 36 zilizofanyiwa tathmini ya kujua uwezo wa
kukabiliana na maafa katika Wilaya za Magharibi, Mjini na Kaskazini ‘A’.
Mafunzo hayo ni muendelezo wa mafunzo kwa Wilaya zilizopata fursa ya kutengeneza
Mpango wa Dharura wa Kukabiliana na Maafa ambapo wilaya za Micheweni na Wete
Pemba tayari zimeshatengeneza Mipango na kupatiwa mafunzo. (Kiambatanisho Nam. 4A & 4 B)
iv. Idara
imekamilisha Mipango ya Kujiandaa na Kukabiliana na Maafa kwa Wilaya za Mjini,
Magharibi na Kaskazini ‘A’. Mipango kama
hii imeshakamilika kwa Wilaya za Wete na Micheweni Pemba.
v. Idara imetoa
huduma ya operesheni za uokozi kwa abiria waliopata ajali ya kudondoka katika meli
ya MV. Kilimanjaro II iliyotokea katika bahari ya Nungwi tarehe 5 Januari 2014.
vi. Idara imeendesha
makongamano mawili (2) ya kukabiliana na maafa kwa wadau wa maafa nchini.
vii. Idara imeandaa Mwongozo
wa Mafunzo kwa Wafanyakazi wa Idara ya Kukabiliana na Maafa pamoja na Mkakati
wa Kutafuta Nyenzo za Kukabiliana na Maafa wa Zanzibar.
viii. Idara imetoa elimu
ya kukabiliana na maafa kwa watu wenye ulemavu 100 na wanafunzi wa skuli za
msingi na Sekondari (1,200) katika Wilaya za Mjini na Kaskazini ‘A’ Unguja na
Chakechake na Mkoani Pemba.
ix. Idara imefanya
mikutano miwili (2) Unguja na Pemba ya kuelimisha wadau juu ya Mwongozo wa
Kukabiliana na Maafa Zanzibar pamoja na Mwongozo wa Ufuatiliaji na Tathmini wa
Sera ya Kukabiliana na Maafa ya Zanzibar.
x. Idara imelipia
gharama za mafunzo ya muda mrefu (Shahada ya Pili) kwa wafanyakazi watatu (3)
wa Idara. Wafanyakazi hawa wote wanasomea kada ya kukabiliana na maafa.
77.0
Mheshimiwa Spika,
katika
mwaka 2014/2015, Idara imepanga kutekeleza malengo yafuatayo: -
i. Kuweka mazingira
mazuri ya kazi za Idara kwa ununuzi wa vifaa vya ofisi na samani.
ii. Idara kwa
kushirikiana na Washirikia wa Maendeleo (USAFRICOM, Benki ya Dunia na Kamisheni
ya Bahari ya Hindi) itaendesha mafunzo mbalimbali ya kukabiliana na maafa kwa
watendaji na wadau wa kukabiliana na maafa pamoja na kuendesha mazoezi mawili
(2) ya kukabiliana na maafa.
iii. Kuwajengea uwezo
wafanyakazi wanne (4) wa Idara kwa kuwapatia mafunzo ya muda mfupi na muda
mrefu pamoja na kulipa stahiki za likizo kwa wafanyakazi sita (6).
iv. Kuyafanyia
matengenezo maghala mawili (2) na kununua vifaa vya kukabiliana na maafa kwa Unguja
na Pemba.
v. Kujenga uwezo kwa
jamii katika kukabiliana na majanga na maafa kwa Shehia 10.
vi. Kukamilisha
sheria mpya ya kukabiliana na maafa.
78.0
Mheshimiwa Spika, ili Idara ya
Kukabiliana na Maafa iweze kutekeleza malengo yake katika mwaka wa fedha
2014/2015, naliomba Baraza lako Tukufu kuidhinisha jumla ya Sh. 298,447,800 kwa
matumizi ya Idara. Kati ya hizo Sh. 128,875,500 kwa ajili ya malipo ya
mishahara, posho za wafanyakazi na mchango wa Mfuko wa Hifadhi ya Jamii na Sh. 169,572,300
kwa matumizi mengineyo. Aidha, naliomba Baraza lako Tukufu kuidhinisha jumla ya
Sh. 1,322,880,000 kwa ajili ya Miradi ya maendeleo, Sh. 40,000,000 ikiwa ni
mchango wa Serikali na Sh. 1,282,880,000 ni mchango kutoka washirika wa
Maendeleo.
IDARA YA SHEREHE NA
MAADHIMISHO YA KITAIFA
79.0
Mheshimiwa Spika, Idara ya
Sherehe na Maadhimisho ya Kitaifa ina jukumu la kuratibu Sherehe na Maadhimisho
ya Kitaifa pamoja na shughuli za kuwaenzi Viongozi wa Kitaifa. Sherehe na
Maadhimisho ya Kitaifa yanayoratibiwa na Idara ni Sherehe za Mapinduzi Matukufu
ya Zanzibar, Sherehe za Muungano wa Tanganyika na Zanzibar pamoja na ushiriki
wa Viongozi na wananchi wa Zanzibar katika Sherehe za Uhuru wa Tanganyika.
Aidha, kwa upande wa shughuli za kuwaenzi Viongozi wa Kitaifa, Idara inaratibu
mazishi ya Viongozi kama ilivyoainishwa kwenye Sheria ya Kuwaenzi Viongozi Nam.
10 ya Mwaka 2002, Hitma na Dua ya Marehemu Sheikh Abeid Amani Karume pamoja na
kutunza kumbukumbu za viongozi hao.
80.0
Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa
fedha 2013/2014 Baraza lako Tukufu liliidhinisha jumla ya Sh. 2,189,103,000 kwa
Idara ya Sherehe na Maadhimisho ya Kitaifa. Hadi kufikia mwezi Machi, 2014
Idara iliingiziwa jumla ya Sh. 2,480,329,652 kwa kazi za kawaida ambazo ni sawa
na asilimia 113.
81.0
Mheshimiwa Spika, Katika kipindi
cha mwaka wa fedha 2013/2014, Idara ya Sherehe na Maadhimisho ya Kitaifa
imetekeleza malengo yafuatavyo:-
i.
Kuratibu kwa mafanikio makubwa maadhimisho ya Sherehe za
Miaka 50 ya Mapinduzi Matukufu ya Zanzibar ambazo zilikuwa za kipekee na za
aina yake zilizofikia kilele tarehe 12 Januari 2014.
ii.
Idara imeratibu kwa mafanikio makubwa Sherehe za Miaka 50
ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar zilizofanyika katika uwanja wa Uhuru, Dar
es Salaam tarehe tarehe 26 Aprili 2014. Aidha, Idara imeratibu ushiriki wa viongozi
na wananchi wa Zanzibar katika Sherehe za miaka 52 ya Uhuru wa Tanganyika
zilizofanyika tarehe 09 Disemba, 2013. Kazi hii imefanywa kwa kushirikiana na
Ofisi ya Waziri Mkuu.
iii.
Idara imeratibu Hitma na Dua ya Marehemu Sheikh Abeid
Amani Karume iliyofanyika Afisi Kuu ya CCM, Kisiwandui tarehe 7 Aprili, 2014.
iv.
Idara imeendelea kukusanya taarifa na kumbukumbu za
Marehemu Sheikh Abeid Amaan Karume.
v.
Idara imenunua vifaa vya sherehe ikiwemo zulia jekundu na
bendera pamoja na kuendelea kulifanyia matengenezo Ghala la Idara lililopo
Mwanakwerekwe Unguja.
vi.
Idara imewapatia mafunzo ya muda mrefu wafanyakazi wawili
(2) wa Idara pamoja na kulipia stahiki za
wafanyakazi wawili (2) waliokwenda likizo.
82.0
Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa
fedha 2014/2015, Idara ya Sherehe na Maadhimisho ya Kitaifa imepanga kutekeleza
malengo yafuatayo:-
i.
Kuweka mazingira mazuri ya kazi za idara kwa ununuzi wa
vifaa vya ofisi na samani.
ii.
Kuwajengea uwezo wafanyakazi wawili (2) wa idara kwa kutoa
mafunzo ya muda mfupi na muda mrefu pamoja na kulipa stahiki za likizo kwa
wafanyakazi wawili (2).
iii.
Kuratibu na kusimamia sherehe za Miaka 51 ya Mapinduzi
Matukufu ya Zanzibar.
iv.
Kuratibu sherehe za Miaka 51 ya Muungano wa Tanganyika na
Zanzibar na ushiriki wa viongozi na wananchi wa Zanzibar katika Sherehe za miaka
53 ya Uhuru wa Tanganyika kwa kushirikiana na Ofisi ya Waziri Mkuu.
v.
Kuratibu Hitma na Dua ya Marehemu Sheikh Abeid Amani
Karume (Siku ya Mashujaa).
vi.
Kuifanyia mapitio Sheria Namba 10 ya 2002 ya Kuwaenzi Viongozi
pamoja na mambo yanayohusiana nayo.
vii.
Kuendelea kukusanya na kutunza kumbukumbu za Marehemu
Sheikh Abeid Amani Karume.
83.0
Mheshimiwa Spika, ili Idara ya
Sherehe na Maadhimisho ya Kitaifa iweze kutekeleza malengo yake iliyojipangia kwa
mwaka wa fedha 2014/2015, naliomba Baraza lako Tukufu kuidhinisha jumla ya Sh. 871,615,500
kwa matumizi ya Idara. Kati ya hizo Sh. 87,259,800 kwa malipo ya mishahara,
posho za wafanyakazi na mchango wa mfuko wa Hifadhi ya Jamii na Sh. 784,355,700
ni kwa matumizi mengineyo.
IDARA YA UPIGAJI
CHAPA NA MPIGA CHAPA MKUU WA SERIKALI
84.0
Mheshimiwa Spika,
Idara
ya Upigaji Chapa na Mpiga Chapa Mkuu wa Serikali ina majukumu ya kuchapisha Miswaada
ya Sheria, Gazeti Rasmi, risiti, hotuba za bajeti na nyaraka zote za Serikali
pamoja na kuuza vifaa vya kuandikia kwa Taasisi zote za Serikali na watu
binafsi. Vile vile, Idara ina jukumu kuu
la kuchapisha na kuhifadhi nyaraka za siri za Serikali.
85.0
Mheshimiwa Spika, Kwa mwaka wa
fedha 2013/2014 Baraza lako Tukufu liliidhinisha jumla ya Sh. 546,868,000 kwa
Idara ya Upigaji Chapa na Mpiga Chapa Mkuu wa Serikali. Hadi kufikia mwezi
Machi, 2014 Idara iliingiziwa jumla ya Sh. 288,754,082 kwa kazi za kawaida
ambazo ni sawa na asilimia 53. Aidha, Idara iliidhinishiwa jumla ya Sh. 2,500,000,000
kwa kazi za maendeleo ikiwa ni mchango wa SMZ na hadi kufikia mwezi Machi, 2014
Idara iliingiziwa jumla ya Sh. 2,050,000,000 sawa na asilimia 82.
86.0
Mheshimiwa Spika, Idara
ilipangiwa kuchangia jumla ya Sh.500,000,000 kwa mwaka wa fedha 2013/2014 katika
Mfuko Mkuu wa Serikali. Hadi kufikia tarehe 31 Machi, 2014, Idara imechangia Sh.
14,623,400 sawa na asilimia 4. Mchango huu mdogo umetokana na kiwanda kupunguza
uzalishaji kutokana na kuharibika kwa mashine pamoja na kuanza kwa zoezi la
kuhamisha mashine na kufunga mashine mpya. Aidha, Idara inazidai baadhi ya
taasisi za Serikali jumla sh. 42,480,000 za mapato ambazo ni sehemu ya mapato
yanayotarajiwa kukusanywa katika kipindi cha Julai 2013 - Machi 2014.
87.0
Mheshimiwa Spika, Idara kwa Mwaka
wa Fedha 2013/2014 imeweza kutekeleza kazi zifuatazo:
i.
Jumla ya wafanyakazi saba (7) wamepatiwa mafunzo ya muda
mrefu na mfupi katika ngazi za cheti, diploma na shahada ya pili.
ii.
Idara inaendelea kutoa huduma ya machapisho mbali mbali
zikiwemo kazi za uchapishaji wa sheria, Gazeti Rasmi ya Serikali, Katiba,
madaftari ya mishahara, kalenda, na kazi nyengine za taasisi za umma na
binafsi.
iii.
Idara imekamilisha matengenezo ya jengo jipya la kiwanda
cha uchapishaji huko Maruhubi na tayari jengo hilo limeanza kutumika.
iv.
Idara imechapisha miswada ya sheria 11 na matoleo 1,400 ya
Gazeti Rasmi la Serikali.
v.
Idara imenunua pamoja na kufunga kwa awamu ya kwanza mashine
mpya nne (4) za aina ya dijitali.
88.0
Mheshimiwa Spika, katika Mwaka wa
Fedha wa 2014/2015, Idara ya Upigaji Chapa na Mpiga Chapa Mkuu wa Serikali
imejipangia malengo yafuatayo:-
i.
Kuweka mazingira mazuri ya kazi za Idara kwa ununuzi wa
vifaa vya ofisi na samani.
ii.
Kuwajengea uwezo wafanyakazi watano (5) wa Idara kwa kutoa
mafunzo ya muda mfupi na muda mrefu pamoja na kulipa stahiki za likizo kwa
wafanyakazi saba (7).
iii.
Kutoa huduma za Uchapishaji wa nyaraka na Sheria za
Serikali
iv.
Kutangaza huduma za Kiwanda kwa ajili ya kuongeza idadi ya
wateja na mapato.
v.
Kukamilisha utaratibu wa kuanzisha Bohari Kuu ya Serikali
ya vifaa vya Ofisi.
89.0
Mheshimiwa Spika, katika Mwaka wa
Fedha 2014/2015, Idara ya Upigaji Chapa na Mpiga Chapa Mkuu wa Serikali
imekadiriwa kutumia jumla ya Sh. 482,066,600. Kati ya hizo Sh. 347,066,600 kwa
matumizi ya mishahara ya wafanyakazi, michango ya ZSSF na Sh. 135,000,000 kwa
matumizi mengineyo.
90.0
Mheshimiwa Spika, kwa upande wa
mapato Idara imepangiwa kukusanya Sh. 600,000,000 kwa mwaka wa fedha 2014/2015.
OFISI KUU PEMBA
91.0
Mheshimiwa Spika,
Ofisi ya Makamu wa
Pili wa Rais Pemba
ina jukumu la kusimamia utekelezaji wa kazi za Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais kwa upande wa Pemba.
92.0
Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa
fedha 2013/2014 Baraza lako Tukufu liliidhinisha jumla ya Sh. 452,817,000 kwa
Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais Pemba. Hadi kufikia mwezi Machi, 2014 Idara
iliingiziwa jumla ya Sh. 254,014,050 kwa kazi za kawaida ambazo ni sawa na
asilimia 56.
93.0
Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa
fedha 2013/2014 Ofisi Kuu Pemba ilikuwa
na lengo la kusimamia shughuli
za Idara zilizo chini ya Ofisi ya
Makamu wa Pili wa Rais Kisiwani Pemba na imetekeleza kazi zifuatazo:
i.
Ofisi iliratibu na kufuatilia utekelezaji wa ziara 23 za
Viongozi Wakuu wa Kitaifa.
ii.
Ofisi ilifanya Semina ya siku moja (1) kwa Maafisa Mipango
wa Mawizara, Mikoa na Wilaya juu ya uandishi wa taarifa ya utekelezaji wa Ilani
ya Uchaguzi ya Chama Tawala. (CCM)
iii.
Ofisi iliratibu
na ilisimamia utekelezaji wa miradi ya TASAF Pemba
iv.
Ofisi iliendelea kutoa mafunzo, kusimamia na kuratibu
shughuli za kukabiliana na Maafa.
v.
Ofisi iliwapatia mafunzo wafanyakazi wanane (8) katika kada mbali mbali.
94.0
Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa
fedha 2014/2015 Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais Pemba itatekeleza malengo ya
idara na taasisi zilizo chini ya Ofisi ya Makamu wa Rais.
95.0
Mhesimiwa spika, ili Ofisi ya
Makamu wa Pili wa Rais Pemba iweze kutekeleza malengo yake iliyopanga naliomba
Baraza lako Tukufu liidhinishe jumla ya Sh. 388,964,000 kwa matumizi ya Ofisi. Kati
ya hizo Sh. 241,266,000 ni kwa malipo ya mishahara na posho za wafanyakazi na
mchango wa Mfuko wa Hifadhi ya Jamii, na
Sh. 147,698,000 ni kwa matumizi mengineyo.
TUME YA UCHAGUZI YA
ZANZIBAR
96.0
Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa
fedha 2013/2014 Baraza lako tukufu liliidhinisha jumla ya. Sh. 987,000,000 kwa
Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar, Hadi kufikia mwezi Machi, 2014 Tume iliingiziwa
jumla ya Sh. 827,303,454 kwa kazi za kawaida ambazo ni sawa na asilimia 84.
Aidha, Tume iliidhinishiwa Sh. 3,594,000,000 kutoka kwa Washirika wa Maendeleo
na hadi kufikia mwezi Machi, 2014 Tume ya Uchaguzi iliingiziwa jumla ya Sh. 768,165,455
sawa na asilimia 21.
97.0 Mheshimiwa Spika,
kwa mwaka wa fedha 2013/2014 Tume ya Uchaguzi
imetekeleza malengo yafuatayo:-
i. Katika mwaka wa Fedha wa 2013/2014, Tume ya Uchaguzi
ya Zanzibar iliendesha chaguzi ndogo mbili. Chaguzi hizo ni Uchaguzi Mdogo wa
Jimbo la Kiembesamaki Wilaya ya Magharibi kujaza nafasi iliyoachwa wazi na
Ndugu Mansour Yusuf Himid aliyekuwa mwakilishi wa Jimbo hilo na uchaguzi Mdogo
wa Wadi ya Kiboje Wilaya ya Kati iliyoachwa wazi kufuatia kifo cha Diwani wa
Wadi hiyo Ndugu Mayunga Maftah Mayunga. Chaguzi zote mbili ziliendeshwa kwa salama
na utulivu mkubwa.
ii. Tume imetoa elimu ya Wapiga Kura kupitia
vyombo mbali mbali vya habari vya Redio na Televisheni, semina za Wanafunzi wa
Skuli za Sekondari na kupitia vikundi vya Sanaa za Maonesho kwa Unguja na Pemba.
Aidha, imeendelea kutoa elimu ya uandikishaji wa Wapiga Kura katika Shehia
mbalimbali ikiwa ni sehemu ya maandalizi ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015.
iii. Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar imeanza maandalizi ya
awali ya kuchunguza idadi, majina na mipaka ya majimbo ya Uchaguzi kwa
kuwapatia Wajumbe wa Tume ya Uchaguzi na Watendaji wake mafunzo kuhusu
uchunguzi wa majimbo. Mafunzo hayo
yamefanyika kwa awamu mbili ambapo awamu ya kwanza iliwahusisha Maafisa Uchaguzi wa Wilaya za Unguja na Pemba
na awamu ya pili iliwahusisha Wajumbe wa
Tume na Sekretarieti.
iv. Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar imeendesha kazi za uandikishaji
wa Wapiga Kura wapya na uendelezaji wa Daftari la Kudumu la Wapiga kura. Kazi
hiyo ilianza katika mwezi wa Juni 2013 Mkoa wa Kaskazini Unguja na ilimalizika
katika mwezi wa Novemba 2013, Mkoa wa Kusini Pemba. Zoezi hilo lilifanyika kwa
kuwaandikisha wananchi wote waliojitokeza ambao wana sifa za kupiga kura kwa
Uchaguzi Mkuu wa Zanzibar. Jumla la
wananchi 41,261 waliandikishwa (Kiambatisho
Nam 5).
98.0 Mheshimiwa Spika,
kwa mwaka wa fedha 2014/2015 Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar imepanga kutekeleza malengo yafuatayo:-
i. Kuweka mazingira
mazuri ya kazi za Tume kwa ununuzi wa vifaa vya ofisi na samani.
ii. Kuwajengea uwezo
wafanyakazi watatu (3) kwa kuwapatia mafunzo ya muda mrefu na wafanyakazi (15) mafunzo
ya muda mfupi pamoja na kulipa stahiki za likizo kwa wafanyakazi sita (6).
iii. Kuendeleza
Daftari la Kudumu la Wapiga Kura.
iv. Kufanya uchunguzi
wa idadi, majina na mipaka kwa majimbo yote 50 ya uchaguzi.
v. Kusimamia na
kuendesha kura ya Maoni ya kuthibitisha Katiba iliyopendekezwa.
vi. Kufanya
matayarisho ya jumla ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015.
99.0 Mheshimiwa Spika,
ili Tume ya Uchaguzi iweze kutekeleza majukumu
yake kwa mwaka wa fedha 2014/2015, naliomba Baraza lako Tukufu liidhinishe
jumla ya Sh. 1,314,100,000 kwa matumizi
ya kawaida. Kati ya hizo Sh. 971,500,000 ni kwa
malipo ya mishahara, posho na
stahiki za wafanyakazi na Sh. 342,600,000 kwa matumizi mengineyo. Aidha, naliomba Baraza lako Tukufu kuidhinisha jumla ya Sh. 1,750,000,000
kwa ajili ya utekelezaji wa kazi za maendeleo kupitia mchango wa Washirika wa
Maendeleo.
100.0 Mheshimiwa Spika,
Tume ya Uchaguzi kupitia Mfuko
Mkuu wa Serikali imepangiwa kutumia jumla ya Sh. 3,000,000,000 kwa ajili ya
maandalizi ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015, kufanya uchunguzi wa idadi, majina
na mipaka ya majimbo ya uchaguzi pamoja na kuendeleza Daftari la Kudumu la
Wapiga Kura.
BARAZA LA
WAWAKILISHI
101.0
Mheshimiwa Spika, Baraza la Wawakilishi Zanzibar
limeundwa chini ya Kifungu cha 63 cha Katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984 na majukumu
ya msingi yanatajwa kwenye Kifungu cha 88 cha Katiba ambayo ni kama yafuatayo:-
i. Kutunga Sheria
pale ambapo utekelezaji wa jambo unahitaji kuwepo kwa sheria hiyo.
ii. Kujadili shughuli
za kila Wizara wakati wa kikao cha mwaka wa Bajeti katika Baraza la
Wawakilishi.
iii. Kuuliza maswali
mbalimbali kwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika Baraza la Wawakililshi.
iv. Kuidhinisha na
kusimamia Mipango ya Maendeleo ya Serikali katika njia ile ile ambayo Bajeti ya
mwaka inaidhinishwa.
102.0
Mheshimiwa Spika, katika
kutekeleza majukumu hayo kwa mwaka wa fedha wa 2013/2014 Ofisi ya Baraza la
Wawakilishi iliidhinishiwa jumla ya Sh. 14,852,000,000. Hadi kufikia mwezi wa
Machi 2014 Baraza limeingiziwa Sh. 10,501,979,561 kwa kazi za kawaida sawa na
asilimia 71. Kwa upande wa fedha za
Miradi ya Maendeleo Baraza la Wawakilishi liliidhinishiwa jumla ya Sh. 697,536,000
na hadi kufikia mwezi Machi 2014 Baraza limeiingiziwa Sh. 544,658,000 Sawa na
asilimia 78.
103.0
Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa
fedha 2013/2014 Baraza la Wawakilishi limetekeleza kazi zifuatazo:-
i. Baraza limefanya Mikutano
minne ya kawaida ambapo kwenye Mikutano hiyo jumla ya Miswada kumi (10) ya
Sheria ilijadiliwa na kupitishwa na maswali 250 yameulizwa na kujibiwa. Mgawanyo
wa Miswada na Maswali hayo ni kama ifuatavyo:-
§ Mkutano wa Kumi
na mbili wa Bajeti ya mwaka wa fedha wa 2013/2014 ulikuwa na Miswada miwili ya
Sheria na jumla ya Maswali 75 ya msingi yaliulizwa na kujibiwa.
§ Mkutano wa Kumi
na Tatu uliofanyika mwezi wa Oktoba, 2013 ulipitisha Miswada minne ya Sheria na
jumla ya maswali 71 ya msingi yaliulizwa na kupatiwa majibu.
§ Mkutano wa Kumi
na Nne uliofanyika mwezi wa Disemba 2013 ulipitisha Miswada Mitatu ya Sheria
wakati jumla ya maswali 61 ya msingi yaliulizwa na kujibiwa. Aidha, kwenye
Mkutano huo Baraza lilipokea na kuijadili Ripoti ya Kamati Teule ya Kuchunguza
Migogoro ya Ardhi. Pia, kulikuwa na Hoja mbili za Wajumbe. Moja ni Hoja ya
Mjumbe kuomba Ridhaa ya Baraza kwa ajili ya kuwasilisha Mswada wa Sheria ya
Utawala wa Baraza, iliyowasilishwa na Mhe. Hamza Hassan Juma na Pili ni Hoja ya
Mjumbe ya kuliomba Baraza kutoa Azimio Dhidi ya Vitendo vya Udhalilishaji wa
Watoto, Zanzibar. Hoja ambayo iliwasilishwa kwenye Baraza na Mhe. Mgeni Hassan
Juma
§ Mkutano wa Kumi
na Tano uliofanyika mwezi wa Februari, 2014 nao ulipitisha Miswada miwili ya
Sheria na jumla ya maswali 50 yaliulizwa na kujibiwa. Wakati huohuo, Baraza
lilipokea Taarifa za Utekelezaji wa Maagizo ya Kamati za Baraza yaliyotolewa
mwaka 2012/2013 na Kamati za Kudumu za Baraza ziliwasilisha Ripoti za Kazi kwa
mwaka 2013/2014. Katika Mkutano huo pamoja na mambo mengine yaliyojadiliwa na
kufikiwa maamuzi, Baraza liliunda Kamati Teule ya Kuchunguza Upotevu wa Nyaraka
za Serikali katika Jengo la Nyaraka na Makumbusho. Kamati hiyo iliundwa ikiwa
na Wajumbe watano. Hili liliibuka wakati wa kuwasilisha Ripoti za Kamati na
lilitokana na Ripoti ya Kamati ya Katiba, Sheria na Utawala. (Kiambatanisho Nam. 6)
ii. Kamati za Kudumu
za Baraza zilifanya kazi zake za Kawaida za kufuatilia utekelezaji wa majukumu
ya Serikali kupitia Wizara na Idara mbali mbali za Serikali. Aidha, Kamati Teule
ya Baraza iliyopewa kazi ya kuchunguza Migogoro ya Ardhi nayo ilimaliza kazi
yake na kuwasilisha Ripoti yake kwenye Baraza.
iii. Ofisi imewapatia
mafunzo Wafanyakazi 16 katika fani za Sheria, Uchumi, Uhusiano wa Kimataifa,
Utawala wa Biashara, Utawala wa Raslimali Watu, Ufundi, Teknolojia, Ununuzi na
Ugavi, Ukutubi na Elimu, hii ni kwenye ngazi za Vyeti, Stashahada, Shahada,
Shahada ya Uzamili na Shahada ya Uzamivu.
iv. Baraza
limeshiriki katika Mkutano wa Jumuiya ya Makatibu Mezani (SOCAT) Dar-es-Salaam kwa
lengo la kuendeleza uhusiano wa
Kimataifa wa kikanda baina ya Baraza na vyombo vyengine vya Kutunga Sheria na
Umoja wa Mabunge ya Jumuiya ya Madola.
v. Ofisi ya Baraza
la Wawakilishi bado inaendeleza vipindi vyake vya kutoa elimu kwa Umma kupitia
Shirika la Utangazaji la Zanzibar (ZBC) kwa upande wa Redio na Televisheni. Kwa
kipindi cha mwaka 2013/2014 jumla ya vipindi 24 vya LIJUE BARAZA LA WAWAKILISHI
vilirushwa hewani.
vi. Ofisi imefanya matengenezo
makubwa ya majengo kwa Ofisi za Baraza Unguja na Pemba hasa yanayohusu miundo
mbinu ya maji, tatizo ambalo sasa limepungua kwa kiasi kikubwa. Aidha, katika
kupunguza matumizi ya umeme hasa kwa kuendesha vipoza hewa muda wote, mfumo wa
muundo wa madirisha nao umeanza kubadilishwa ambapo badala ya kuwa na madirisha
yasiyofunguka sasa yamewekwa yale yanayofunguka.
vii.
Ofisi imefanya tathmini ya athari zinazotokana na nyufa
ili kuweza kutafuta ufumbuzi wa kuziba nyufa hizo.
104.0
Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha
2014/2015 Baraza la Wawakilishi limepanga kutekeleza malengo yafuatayo:-
i. Kujenga Mazingira
mazuri kwa kuwezesha kufanyika kwa Mikutano minne (4) ya Baraza la Wawakilishi pamoja na
kazi za Kamati katika kufuatilia Shughuli za Serikali na Kusimamia uwajibikaji
wake
ii. Kutoa mafunzo ya
kuongeza uwezo wa kitaalamu kwa Wajumbe na Wafanyakazi wa Baraza
iii. Kuweka majengo yote ya Ofisi katika hali nzuri
iv. Kutoa taaluma kwa
wananchi kuhusu utendaji wa Shughuli za Baraza kupitia vyombo vya Habari
v. Kuimarisha
mahusiano kati ya Baraza na Mabunge mengine ya Umoja wa Mabunge ya Jumuiya ya
Madola.
105.0
Mheshimiwa Spika,
ili
Ofisi ya Baraza la Wawakilishi iweze kutekeleza malengo yake kwa mwaka wa fedha
2014/2015, naliomba Baraza lako Tukufu liidhinishe jumla ya Sh. 14,564,000,000
kwa matumizi ya Ofisi. Kati ya hizo Sh. 7,664,000,000 ni kwa malipo ya
mishahara, posho za wafanyakazi, Stahiki nyengine na mchango wa Mfuko wa
Hifadhi ya Jamii na jumla ya Sh. 6,900,000,000 kwa matumizi mengineyo. Kwa
upande wa fedha za maendeleo naliomba Baraza lako Tukufu liidhinishe jumla ya Sh.
710, 615,000 ikiwa ni mchango wa Washirika wa Maendeleo.
UKUSANYAJI MAPATO
106.0
Mheshimiwa Spika,
kwa mwaka wa fedha 2013/2014, Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais ilipanga kukusanya
mapato ya jumla ya Sh. 544,400,000 kwa mchanganuo ufuatao:-
i. Idara ya Upigaji
Chapa na Mpiga Chapa Mkuu wa Serikali
Sh. 500,000,000
ii.
Idara ya Uendeshaji na Utumishi
(Kodi ya Ukumbi
wa Mikutano wa BLW wa zamani)
Sh.
38,000,000
iii.
Idara ya Sherehe na Maadhimisho ya Kitaifa
(Kodi ya milango
ya duka na mashamiana)
Sh. 6,000,000
Jumla Sh. 544,000,000
107.0
Mheshimiwa Spika, hadi kufikia
mwezi Machi 2014 ukusanyaji halisi wa mapato ulikua ni jumla ya Sh. 16,519,200
Sawa na asilimia 4 kama ifuatavyo:-
i. Idara ya Upigaji
Chapa na Mpiga Chapa Mkuu wa Serikali
Sh. 14,899,200
ii.
Idara ya Uendeshaji na Utumishi
(Kodi ya Ukumbi
wa Mikutano wa BLW wa zamani) __
iii. Idara ya Sherehe
na Maadhimisho ya Kitaifa
(Kodi ya Milango ya duka na mashamiana)
Sh. 1,620,000
Jumla
Sh. 16,519,200
108.0
Mheshimiwa Spika,
kwa mwaka wa fedha 2014/2015, Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais imepanga
kukusanya mapato ya jumla ya Sh. 608,000,000 kwa mchanganuo ufuatao:-
i.
Idara ya Upigaji Chapa na Mpiga Chapa Mkuu wa Serikali
Sh. 600,000,000
ii.
Idara ya Uendeshaji na Utumishi
(Kodi ya Ukumbi
wa Mikutano wa BLW wa zamani)
Sh. 5,000,000
iii.
Idara ya Sherehe na Maadhimisho ya Kitaifa
(Kodi ya mashamiana) Sh. 3,000,000
Jumla Sh. 608,000,000
109.0
Mheshimiwa Spika,
muhtasari
wa makadirio ya fedha kwa kazi za kawaida na za Maendeleo kwa mwaka wa
fedha 2014/2015 ni kama unavyoonekana katika (Kiambatanisho Nam. 7A na 7B).
HITIMISHO
110.0
Mheshimiwa Spika,
napenda
kuchukua fursa hii kumshukuru kwa dhati Mheshimiwa Mohamed Aboud Mohamed,
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais kwa kunisaidia kutekeleza
majukumu ya Ofisi yangu kwa ufanisi mkubwa. Aidha, nawashukuru kwa dhati watendaji wote wa Ofisi ya Makamu wa Pili wa
Rais wakiongozwa na Katibu Mkuu, Dkt. Khalid Salum Mohamed kwa juhudi zao
katika kutekeleza majukumu yao.
111.0
Mheshimiwa Spika,
natoa
shukrani zangu za dhati kwa Wajumbe wote wa Baraza la Wawakilishi na shukurani za pekee kwa Mwenyekiti
na wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Kusimamia Ofisi za Viongozi Wakuu wa Kitaifa
kwa mashirikiano, maelekezo, ushauri na michango wanayotupa ambayo ilisaidia
katika utayarishaji wa hotuba hii.
Aidha, napenda kuwashukuru sana Washirika wa Maendeleo (Development Partners)
na nchi marafiki ambazo zinaendelea kuchangia katika kufanikisha utekelezaji wa
malengo ya Ofisi yetu na ya nchi kwa jumla katika mwaka wa fedha 2013/2014.
Miongoni mwao ni: AL-Yousef Foundation, Benki ya Dunia, Clinton Foundation,
China, FAO, Finland, Norway, Jumuiya ya Afrika ya Mashariki, India, Japan,
Marekani, Mfuko wa Dunia wa Kupambana na Kifua Kikuu, Malaria na UKIMWI (Global
Fund), Oman, UNAIDS, USAID, UNDP, UNICEF, UNFPA, WHO, WFP na WIPO. Vile vile,
naishukuru sana Ofisi ya Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na
Ofisi ya Waziri Mkuu kwa ushirikiano wao wa karibu sana na Ofisi yetu. Pia nazishukuru Taasisi zisizo za Kiserikali
kama ZAYEDESA, Jumuiya ya Wafanya Biashara, Wenye Viwanda na Wakulima kwa
kuendelea kuisaidia Serikali katika kutoa huduma za jamii na kuiletea maendeleo
nchi yetu. Pia, nawashukuru wananchi wote ambao wamefuatilia na kusikiliza
Hotuba yetu hii.
112.0
Mheshimiwa Spika,
Baada
ya maelezo hayo, sasa naliomba Baraza lako
Tukufu liidhinishe Jumla ya Sh. 19,988,300,000 kwa Ofisi ya Makamu wa
Pili wa Rais na Taasisi zake (Tume ya Uchaguzi na Baraza la Wawakilishi) kwa
matumizi ya kazi za kawaida na Sh. 6,343,495,000 kwa
kazi za maendeleo (Kiambatanisho Nam. 7A na 7B). Mchanganuo halisi wa
fedha hizo ni kama ifuatavyo:-
Kazi za Kawaida
i
|
Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais
|
Sh. 4,110,200,000
|
ii
|
Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar
|
Sh. 1,314,100,000
|
iii
|
Ofisi ya Baraza la Wawakilishi
|
Sh. 14,564,000,000
|
|
Jumla
Kuu
|
Sh. 19,988,300,000
|
Kazi za Maendeleo
i
|
Ofisi ya Makamu
wa Pili wa Rais
|
|
a
|
Kujenga Uwezo wa Kukabiliana na Maafa
|
Sh. 1,322,880,000
|
b
|
Mradi wa TASAF III
|
Sh. 1,550,000,000
|
c
|
Mfuko wa Maendeleo ya Jimbo (CDF)
|
Sh. 1,010,000,000
|
|
Jumla
Ndogo (OMPR)
|
Sh. 3,882,880,000
|
ii
|
Tume ya
Uchaguzi ya Zanzibar
|
|
|
Mradi wa kuwezesha Demokrasia (DEP)
|
Sh. 1,750,000,000
|
iii
|
Ofisi ya Baraza
la Wawakilishi
|
|
|
Mradi wa Kuwezesha BLW (LSP)
|
Sh. 710,615,000
|
|
Jumla Kuu (Miradi)
|
Sh. 6,343,495,000
|
113.0
Mheshimiwa Spika,
naomba kutoa hoja,
MHE. BALOZI SEIF ALI IDDI
MAKAMU WA PILI WA RAIS,
OFISI YA MAKAMU WA PILI WA RAIS,
ZANZIBAR.
No comments:
Post a Comment