TANZANIA SASA KUONGOZWA NA MARAIS WATATU, MGOMBEA BINAFSI RUKSA...

Ikulu ya Dat es Salaam.
Rasimu ya Katiba imetolewa na Tume ya marekebisho ya katiba na miongoni mwa mambo yanayopendekezwa ni kuundwa kwa Serikali tatu pamoja na kuruhusiwa kwa mgombea binafsi.

Uzinduzi wa rasimu hiyo ya katiba umefanyika jana, Dar es Salaam na kwa uamuzi huo wa tume sasa Tanzania itakuwa na marais watatu ambao ni rais wa serikali ya shirikisho, rais wa Tanzania Bara na rais wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ).
Alisema tume yake inapendekeza serikali tatu, kwani wananchi ambao walitoa mapendekezo hayo ni wengi kuliko makundi ya waliotaka serikali moja, serikali nne, muungano wa mkataba na serikali mbili.
"Sababu zao zilikuwa nzito lakini pia kulikuwa na changamoto nyingi na nzito. Pamoja na maoni ya wananchi, tume ilirejea sababu za kupendekeza muundo huu zilizotolewa na tume zilizopita na tafiti zilizofanywa na tume kuhusu aina mbalimbali za muungano," alisema Warioba.
Alisema pamoja na maoni ya wananchi, tume ilirejea sababu za kupendekeza muundo huo zilizotolewa na tume zilizopita na tafiti zilizofanywa na tume kuhusu aina mbalimbali za muungano.
"Baada ya yote hayo tume hatukuwa na jinsi zaidi ya kufikia uamuzi wa kupendekeza mfumo wa serikali tatu, yaani serikali ya shirikisho, serikali ya Tanzania Bara na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar," alisema Warioba.
Hivyo kutakuwa na serikali ya muungano, serikali ya Tanzania Bara, Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar. Shughuli za Muungano zitatekelezwa na kusimamiwa na serikali ya muungano,  Bunge la Jamhuri ya Muungano na mahakama yake.
Kutokana na uamuzi huo wa tume, muundo, madaraka na mambo mengine ya kiuendaji yahusuyo serikali ya Bara na ile ya Zanzibar yataainishwa katika katiba za washirika hao wa muungano.
Katika rasimu hiyo serikali ya muungano itakuwa ndio chombo chenye mamlaka ya utendaji, Bunge litakuwa na mamlaka ya kutunga sheria kwa mambo ya muungano na mahakama kitakuwa chombo cha kutoa haki katika muungano huo.
Kwa mujibu wa rasimu hiyo, serikali ya Bara itakuwa na mamlaka juu ya mambo yasiyo ya muungano yanayohusu eneo hilo na SMZ, pia itakuwa na mamlaka ya juu yasiyo ya muungano yaliyoko eneo lake. “Washirika wa muungano watakuwa na hadhi na haki sawa ndani ya muungano na watatekeleza."
Washirika hao wanaruhusiwa kuanzisha mahusiano au ushirikiano na jumuiya au taasisi yoyote ya kikanda au kimataifa kwa mambo yaliyo chini yake kwa mujibu wa katiba yake. 
Katika eneo hilo inapendekezwa kuwa mshirika wa muungano anaweza wakati wa kutekeleza majukumu yake kuomba ushirikiano kutoka serikali ya muungano kwa ajili ya kufanikisha uhusiano na jumuiya au taasisi za kimataifa au kikanda na serikali ya muungano inaweza kutoa ushirikiano kwa mshirika huyo kwa namna itakavyohitajika.
Inapendekezwa  kila mshirika wa muungano atateua waziri mkazi atakayeratibu  na kusimamia uhusiano baina  ya serikali za washirika na kati ya serikali ya mshirika na serikali ya muungano, mawaziri hao wakaazi watafanya kazi zao na ofisi zao zitakuwa  makao makuu ya serikali ya muungano na watakuwa kiungo kati ya serikali ya muungano na serikali mshirika
Tume hiyo pia imepunguza mambo ya muungano kutoka 22 hadi saba ambayo ni katiba na mamlaka ya Jamhuri ya muungano wa Tanzania, ulinzi na usalama wa Jamhuri, uraia na uhamiaji, sarafu na benki kuu, mambo ya nje, usajili wa vyama vya siasa, ushuru wa bidhaa na mapato yasiyo ya kodi yatokanayo na mambo ya muungano.
Katika muundo huo serikali ya muungano itapata mamlaka yake kutoka kwa wananchi wa pande zote na serikali za serikali washirika nazo zitachaguliwa na wananchi kupitia uchaguzi wa kidemokrasia utakaosimamiwa na tume za uchaguzi za nchi zao. Viongozi wote hao wanalazimishwa na katiba hiyo kulinda na kuimarisha muungano.
Jaji Joseph Warioba alisema tume yake imezingatia maoni ya wananchi ambao walipendekeza haki zote ziimarishwe na kusiwe na vikwazo vya lazima.
Kutokana na maoni hayo, Warioba alisema tume yake inapendekeza kwamba vikwazo vilivyowekwa kuzuia mgombea huru viondolewe, kwa maana nyingine tume inapendekeza mgombea binafsi aruhusiwe.
Kwenye rasimu hiyo ya katiba, pia haki mpya zimeingizwa ambazo ni haki ya mtoto, haki za watu wenye ulemavu, haki za wanawake, haki za wazee, haki za makundi madogo katika jamii, haki ya elimu na kujifunza, haki ya kupata habari, haki na uhuru wa habari na vyombo vya habari.
Rais wa shirikisho ndiye atakayekuwa amiri jeshi mkuu na yeye atakuwa na makamu mmoja. Rais huyo atakuwa  ndiye taswira ya Muungano wa Tanzania. Pia kutakuwa na bunge la muungano, na mahakama ya Muungano.
Makamu wa Rais ndiye atakayekuwa msaidizi mkuu wa Rais.
Tume hiyo imependekeza umri wa kugombea urais uendelee kuwa miaka 40 kwa vile idadi kubwa ya watu waliotoa maoni walipendekeza umri huo.
Kwenye mapendekezo hayo, Warioba alisema mgombea wa nafasi ya rais atatangazwa kuwa mshindi iwapo atakuwa amepata kura zaidi ya asilimia 50 ya kura zote zilizopigwa.
Inapendekezwa kuwa uchaguzi wa rais itakuwa kama ilivyo sasa isipokuwa tume hiyo imependekeza mgombea urais aweza kupendekezwa na chama cha siasa au kuwa mgombea huru.
Katika rasimu hiyo tume hiyo imependekeza kuwa matokeo ya uchaguzi wa Rais yanaweza kulalamikiwa mahakamani. 'lakini sio kila mtu anaweza kufungua kesi, wanaoweza kufungua kesi ni wagombea urais.'
Pia tume hiyo imependekezwa kuundwa kwa mahakama ya juu (supreme court) ambako wagombea urais wanaweza kufungua kesi  na ni mahakama hiyo tu itakuwa na mamlaka na uwezo wa kusikiliza malalamiko kuhusu matokeo ya uchaguzi wa rais na shauri lazima liamuliwe ndani ya siku thelathini.
"Rais aliyeshinda ataapishwa siku 30 tangu alipotangazwa kuwa mshindi au kuthibitishwa na mahakama," alisema Warioba.
Warioba alisema katika eneo hilo tume imependekeza rais abaki na madaraka ya uteuzi wa viongozi wa ngazi za juu. Lakini imependekezwa rais ashirikiane na taasisi na vyombo vingine katika uteuzi huo.
Alisema uteuzi wa mawaziri na manaibu waziri Rais atateua na Bunge lithibitishe, lakini kuhusu jaji mkuu na naibu jaji mkuu ambaye tume imependekeza cheo hicho kiwepo, majina ya watu waliopendekezwa na tume ya utumishi wa mahakama na baada ya hao bunge litathibitisha. Kwa upande wa makatibu wakuu watateuliwa na rais kutokana na mapendekezo ya tume ya utumishi wa umma.
Kwa upande wa wakuu wa vyombo vya ulinzi na usalama, inapendekezwa kuwa kianzishwe chombo  kipya kitakachoitwa baraza la ulinzi na usalama wa taifa ambalo kati ya majukumu yake itakuwa ni kumshauri rais kuhusu uteuzi wa wakuu wa vyombo vya ulinzi na usalama.
Kinga ya rais imependekezwa na tume hiyo ibaki na  anaweza kushtakiwa na Bunge kama ilivyo katiba ya sasa.
Katika mapendekezo hayo imependekezwa kuwa rais aunde serikali ndogo iliyo na mawaziri wasiozidi 15 na mawaziri hao wasiwe wabunge. Mawaziri hao hawatahudhuria vikao vya Bunge  isipokuwa watahitajika kutoa ufafanuzi kwenye kamati za Bunge.
Kwa upande wa Bunge, Warioba alisema inapendekezwa wabunge wa aina mbili. Yaani kutakuwa na wabunge wa kuchaguliwa na wabunge wachache wa kuteuliwa na Rais kuwakilisha watu wenye ulemavu. Tume imependekeza mbunge akifukuzwa na chama cha siasa abaki kuwa mbunge lakini akihama chama atapoteza ubunge wake.
Katika eneo hilo pia rasimu inapendekeza kuwepo ukomo wa ubunge ambao ni vipindi vitatu vya miaka mitano mitano lakini wananchi wanaweza kumwondoa mbunge wao kabla ya mwisho wa kipindi iwapo hawaridhiki na utendaji wake wa kazi.
Pia imependekezwa kusiwepo na uchaguzi mdogo isipokuwa kama nafasi inayokuwa wazi inatokana na mbunge huru ndipo uchaguzi mdogo kujaza nafasi hiyo utafanyika, "lakini kama nafasi ikiwa wazi kutokana na mbunge wa chama cha siasa basi nafasi hiyo ijazwe na mtu kutoka chama hicho.”
Kwa upande wa spika na naibu spika, inapendekezwa wasitokane na wabunge na wasiwe viongozi wa vyama vya siasa.
Jaji Warioba alisema tume yake imefanya uchambuzi wa maoni ya wananchi katika eneo hilo na imependekeza jina la tume liwe Tume Huru ya Uchaguzi. Tume pia imependekeza sifa za wajumbe wa tume hiyo huru ziwekwe kwenye katiba na watapatikana kutokana miongoni mwa watu wenye sifa zilizoainishwa ndani ya katiba kwa kuomba.
Alisema majina ya waombaji yatachambuliwa na kamati ya uteuzi ambayo mwenyekiti wake atakuwa jaji mkuu na wajumbe wengine sita ambao ni majaji wakuu wa nchi washirika, spika wa bunge la Jamhuri ya Muungano na maspika wa mabunge ya nchi washirika na mwenyekiti wa tume ya haki za binadamu.
Alisema kamati hiyo itapendekeza majina ya watu wnaofaa kwa rais ambaye atateua mwenyekiti, makamu mwenyekiti na wajumbe wengine.
"Bunge litathibitisha uteuzi wao, wabunge na viongozi wengine wa kisiasa  hawatakuwa na sifa za kuwa wajumbe wa tume ya uchaguzi."
Katika eneo hilo imependekezwa kuwa tume huru ya uchaguzi isimamie masuala ya uchaguzi, kura ya maoni na usajili wa vyama vya siasa.
Kuhusu mahakama imependekezwa kuwa majaji wa mahakama ya juu (supreme court) na mahakama ya rufaa watateuliwa na rais baada ya kupendekezwa na tume ya utumishi wa mahakama.
Kwa kuwa tume imependekea muungano wa shirikisho, kutokana na uzito wa maoni ya wananchi, hivyo kutakuwa na benki kuu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania itakayokuwa na wajibu wa kusimamia masuala ya sarafu na fedha za kigeni na benki za washirika wa muungano.
Pia inapendekezwa kuwepo na benki zitakazokuwa na jukumu la kutunza akaunti ya fedha  za serikali za kila mshirika wa Muungano na kuzisimamia benki za biashara katika mamlaka zao.
Katiba inapendekeza makamu wa rais atatoka upande mwingine wa muungano ambako hatoki rais wa muungano.
Mgombea binafsi anaruhusiwa kumteua makamu wa rais hata kama mtu huyo alishashika wadhifa wa urais wa Zanzibar au wa Tanzania bara. Ikitokea rais wa bara au wa SMZ akateuliwa kuwa makamu wa rais atalazimika kuacha wadhifa wake wa awali ili ashike wadhifa huo wa juu katika Jamhuri.
Kwa muundo huo baraza la mawaziri sasa litaundwa na makamu wa rais wa Jamhuri ya muungano, mawaziri wa serikali ya muungano, mwanasheria mkuu wa serikali atahudhuria vikao vya baraza hilo lakini hatakuwa na haki ya kupiga kura.
Baraza hilo la mawaziri ndilo litamshauri rais na bunge na mahakama havitakuwa na uwezo wa kuchunguza jambo ambalo limepitishwa na baraza la mawaziri.
Katiba iliyopendekezwa ina ibara 20 kutoka za sasa ambazo ni 153. Misingi mikuu ya taifa iliyoko kwenye katiba hiyo ni saba kutoka minne ya awali ambayo ni uhuru, haki, udugu, usawa, umoja, amani na mshikamano.
Tunu za taifa katika katiba hiyo ni utu, uzalendo, uadilifu, umoja, uwazi, uwajibikaji, na kiswahili.
Kwenye katiba hiyo pia kuna malengo ya taifa ambayo yatakuwa ni mwongozo kwa serikali, bunge, mahakama, vyama vya siasa, taasisi na mamlaka nyingine kwa kila mwananchi katika matumizi au kutafsiri masharti ya katiba au sheria nyingine za nchi.
Kwa msingi huo, tume hiyo imependekeza malengo makuu ya taifa yapanuliwe kwa mpango wa kuonyesha malengo ya kisiasa, kiuchumi, kijamii, kiutumaduni, kimazingira, na sera ya mambo ya nje.
Vyombo vya kikatiba katika rasimu hiyo ni tume ya uhusiano na uratibu wa serikali, baraza la mawaziri, kamati maalum ya makatibu wakuu na sekretarieti ya baraza la mawaziri, baraza la ulinzi na usalama la taifa, tume huru ya uchaguzi, tume ya utumishi wa mahakama, tume ya utumishi wa umma, tume ya maadili ya viongozi na uwajibikaji na tume ya haki za binadamu na utawala bora.
Katika katiba hiyo inapendekezwa kuwa maadili ya viongozi wa umma pamoja na miiko ya uongozi yawekwe kwenye katiba na tume imependekeza sekretarieti ya maadili ibadilishwe kuw atume yenye mamlaka makubwa ya kusimamia maadili ya viongozi wanaovunja miiko ya uongozi.

1 comment:

Anonymous said...

When some οne searches for his vital thing, so he/she wishеs to be available thаt in dеtail, therefore that thing is maіntaіneԁ oveг heгe.


Аlso ѵіsіt my web page - HTTP://Hicostians.com/node/118601