MEMBE AOTESHWA KUGOMBEA URAIS UCHAGUZI MKUU 2015...


Bernard Membe.

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe, amesema atakuwa tayari kuwania urais mwaka 2015, iwapo wananchi wataona anafaa na kumtaka afanye hivyo.

Alisema hayo juzi wakati akijibu maswali ya mwandishi  wa habari hii mjini hapa, baada ya kumalizika kwa kongamano la vyuo vya elimu ya juu mkoani hapa, lililofanyika katika ukumbi wa St. Dominic.
Membe aliyekuwa mgeni rasmi katika kongamano hilo, alisema ingawa muda wa kufanya uamuzi kuhusu mwaka 2015 bado na chama hakijatoa utaratibu, lakini atasubiri ushauri wa Watanzania.
"Naomba  kurudia,  mimi  nilishapata  kuueleza umma kuwa muda haujafika wa kutangaza kugombea urais ...ila nasema  hivi natarajia sana ushauri  wa  Watanzania.
“Iwapo Watanzania wataniona nafaa na kunitaka nigombee, nitapima mawazo yao na iwapo ni wananchi wengi watakaoniunga mkono kutaka nigombee, basi nitachukua fomu na kuijaza ili nigombee nafasi hiyo kwani sauti ya wengi ni sauti ya Mungu," alisema Waziri Membe.
Membe alisema hali ya kisiasa nchini inakwenda vibaya kutokana na kila mtu kuzungumza mambo bila kujitathmini.
Alisema mbaya zaidi hata baadhi ya wabunge wa CCM, nao wamekuwa si msaada kwa chama, kutokana na kuzungumza mambo dhidi ya Serikali na chama.
Membe alisema amepata kukaa bungeni kwa zaidi ya miaka 15 tangu Bunge la Spika Pius Msekwa, hadi sasa chini ya Spika Anne Makinda, ila anachokiona ni baadhi ya wabunge kukosa maadili na kuzungumza mambo bila kuzingatia kanuni za Bunge, jambo ambalo ni hatari zaidi.
Alisema Bunge linalotazamwa na Watanzania, ni lazima liwe la mfano wa kuigwa na lenye kuzingatia maadili katika kuzungumza, lakini sasa hali siyo hiyo, ndio maana Bunge linaendelea kupoteza mwelekeo.
"Bunge linapoteza mwelekeo kutokana na mawazo ya baadhi ya  wabunge  wanaofikiri  wakisema ovyo na  kutumia  lugha kali katika  kuzungumza, wao ndio wanaonekana ni  wabunge  bora  kitu ambacho hakipo.
“Mbunge ni pamoja na kujiheshimu na kutumia lugha nzuri katika kuwakilisha wapiga kura  wako bungeni," alisema.
Membe alisema kutotumia busara katika kujadili mambo bungeni, si ubunge mzuri na bora watambue wazi kuwa wananchi wao wanawatazama na hukumu yao itatolewa mwaka 2015 katika uchaguzi mkuu kama hicho wanachokifanya, ni kuwakilisha wananchi au kujiwakilisha.
"Nawaomba wabunge wawe wazalendo, wawakilishe wananchi waliowatuma badala ya kuligeuza Bunge kama sehemu ya kuonesha ujuzi wa kuzungumza ovyo.
“Nasema tuogope wananchi, mwaka 2015 watatoa adhabu kwa kila mbunge na kwa sasa wananchi wanasikiliza na kutazama ila muda ukifika watakuacha," alisema.
Alisema wabunge  wengi ni vijana na wanafikiri kusema vibaya juu ya CCM ndio ubunge bora, ila watu watafanya uchunguzi wa kutembelea jimbo la mbunge husika na  kuangalia amefanya  nini katika  jimbo lake na watampima kwa kazi  aliyofanya na si ukali bungeni.
Alisifu baadhi ya wabunge wa CCM, kwamba wamekuwa  msaada mkubwa kwa wananchi katika majimbo yao, kwa chama na Serikali chini ya Rais Jakaya  Kikwete, kwa kusukuma mbele maendeleo ya Taifa,  ila baadhi yao wapo kwa ajili ya kuonesha uwezo wa kusema ovyo.

No comments: