Josephat Mwingira. |
Mlinzi wa shamba la mifugo la Shirika la Efatha Ministry linaloongozwa na Joseph Mwingira, ameuawa na wengine wawili kujeruhiwa baada ya wananchi kuwavamia wilayani Sumbawanga.
Wakazi zaidi ya 200 wa Kijiji cha Sikaunga wilayani Sumbawanga mkoani Rukwa walivamia shamba hilo la Malonje, wakawashambulia walinzi 10 na kumuua mmoja na wengine wawili walijeruhiwa vibaya.
Kaimu Kamanda wa Polisi Mkoa wa Rukwa , Peter Ngusa ambaye pia ni Ofisa Upelelezi wa Mkoa amethibitisha kuwepo tukio hilo jana.
Kwa mujibu wa Ngusa mwili wa mlinzi huyo umehifadhiwa katika chumba cha kuhifadhia maiti cha Hospitali ya Mkoa wa Rukwa mjini Sumbawanga kusubiri uchunguzi wa kitabibu ambapo majeruhi wawili wamelazwa katika hospitali hiyo kwa matibabu huku hali zao zikielezwa kuwa tete.
Jina la marehemu halikuweza kufahamika mara moja . Mmoja wa majeruhi ni Briton Ngimili. Kaimu Kamanda alisema hakuna mtu aliyekamatwa kuhusiana na kisa hicho. Polisi inasaka wahusika wa vurugu hizo.
Akisimulia mkasa huo Ngusa alisema uvamizi huo unatokana na kuwepo mgogoro wa ardhi wa muda mrefu kati ya mwekezaji, Efatha Ministry na wanakijiji wa Sikaunga.
“Tulipata taarifa za vurugu hizo jana na tulipofika huko tulikuta tayari walinzi wawili wa shamba hilo wakiwa wamejeruhiwa na kuhifadhiwa ndani ya ofisi kijijini hapo hivyo walikimbizwa haraka katika Hospitali ya Mkoa mjini hapa ambako wamelazwa kwa matibabu,” alisema.
Alisema baada ya msako wa muda mrefu ndipo polisi waligundua mwili wa mlinzi anayedaiwa kuuawa kikatili na wanakijiji hao.
Mlinzi wa shamba hilo, Ngilimi aliyelazwa kwa matibabu alidai kuwa kabla ya kutokea vurugu hizo kundi dogo la wakazi wa kijini hapo walivamia eneo la shamba hilo.
Alisema walipohojiwa na walinzi wa shamba hilo, wanakijiji hao walianza kuwasiliana kwa simu na wenzao huku wakipuliza filimbi. Kundi kubwa la watu wakitokea kijijini walivamia shamba na walinzi kwa silaha.
Meneja wa Shamba hilo , Peter Kibona alidai kikundi cha watu hao wanaokadiriwa kufikia 200 kutoka Kijiji hicho cha Sikaunga wakiwa na silaha mbalimbali za jadi zikiwemo marungu , mapanga na fimbo waliwashambulia walinzi hao 10 waliojaribu kuwatoa wanakijiji kwa kuingia shambani bila kuwa na vitambulisho.
Kibona alisema walinzi hao walipewa maagizo ya kuwatishia wakazi hao kwa kupiga risasi juu ndipo walipoanza kushambuliwa kwa silaha hizo za jadi na kusababisha kifo cha mmoja wao .
“ Tuliwakataza kabisa walinzi wetu wasiwafyatulie risasi wanakijiji hao waliovamia shambani bali wafyatue hewani na ndivyo walivyofanya,” alisema.
Shamba hilo la Efatha linadaiwa kuwa na ukubwa wa hekta 10,000. Mgogoro baina ya wanakijiji na mwekezaji ni wa muda mrefu.
No comments:
Post a Comment