SISTA ALIYEFUMANIWA NA MUME WA MTU SUMBAWANGA AAMRIWA KULIPA FIDIA...


Mahakama ya Mwanzo  mjini Sumbawanga, imemtia hatiani  aliyekuwa Sista wa Shirika la Kitawa la Kanisa Katoliki, Jimbo la Sumbawanga, Yasinta Sindani, kwa kufumaniwa na mume wa mtu.
Kutokana na kutiwa hatiani, Yasinta aliamriwa kumlipa fidia ya kimila ya Sh 700,000, malalamikaji, Asteria Mgabo. 
Katika kesi hiyo ya msingi ya madai, Asteria alikuwa  akimtaka mshitakiwa alipe Sh milioni 3 ya fidia, baada ya kumfumania na mumewe wa ndoa, Martin Msangawale (39), ambaye pia ni mkazi wa mjini hapa.
Mshitakiwa huyo ambaye ni mtumishi katika Hospitali ya Mkoa wa Rukwa mjini hapa, kwa sasa anaishi nje ya nyumba ya utawa, eneo la Kantalamba mjini hapa.
Inadaiwa mshitakiwa ambaye alikuwa mtawa wa Shirika la Masista wa Maria Mtakatifu Malkia wa Afrika (MMMA), ameachana na maisha ya kitawa miaka miwili iliyopita kwa hiyari yake mwenyewe.
Katika hati ya awali ya madai,  mshitakiwa alikuwa akidaiwa kufumaniwa na Asteria akiwa na mumewe Msangawale katika nyumba ya kulala wageni ya Chipa iliyoko eneo la Katandala mjini Sumbawanga, usiku wa Desemba 24 mwaka jana, siku ya Mkesha wa Sikukuu ya Krismasi.
Akisoma  hukumu  hiyo jana, Hakimu wa Mahakama hiyo, Jaffar Mkinga,  alisema ushahidi uliotolewa na  mlalamikaji, ulikuwa  mzito  wenye kuondoa  shaka zote kwamba mshitakiwa alitenda kosa hilo, tofauti na  utetezi uliotolewa na mdai kwamba ushahidi ulikuwa  dhaifu. 
Katika  utetezi wake,  mshitakiwa aliiambia mahakama  hiyo  kuwa  kwanza alikuwa  hajui kuwa Martin  alikuwa  mume wa mtu. Alidai kuwa pia mwanamume huyo, alimweleza kuwa hana mke na alimwomba wafunge ndoa.
Lakini Hakimu Mkinga alipinga na utetezi  huo  kwa sababu  siku hiyo ya Mkesha  wa Krismas, mwaka jana  saa  saba  na robo  usiku, mlalamikaji akiongoza na  Mwenyekiti wa Mtaa  na mashahidi  wengine watatu, walimfumania mshitakiwa akiwa na Martin.
Alisema mdai na mashahidi hao, walimfumania mshitakiwa na Martin wakitoka katika moja ya vyumba  vya kulaa katika nyumba yakulala  wageni ya Chipa,  iliyopo  katika eneo  la Katandala mjini hapa.
Kwa mujibu wa Hakimu Mkinga, baada ya kufumaniwa mshitakiwa na Martin walipokubali kusaini karatasi ya  ya fumanizi ya ugoni, iliyoaandaliwa  na  Mwenyekiti huyo wa mtaa.
“Hivyo  kama  mshitakiwa ulikuwa haufahamu kuwa Martin alikuwa hana mke, ilikuwaje ukakubali  kusaini  karatasi hiyo  ya fumanizi iliyoandaliwa na Mwenyekiti  huyo?” Alihoji.
Hata hivyo alisema kutokana na Sheria ya Ndoa na Mirathi  ya 1971, faini ya fumanizi la ugoni si adhabu,   inapaswa  itolewe kulingana na  mila na desturi  za  eneo la tukio.
Kutokana na sheria hiyo, Hakimu Mkinga alimuamuru mshitakiwa kulipa mara moja faini ya fumanizi la ugoni ya Sh 700,000  kwa mlalamikaji.
“Mlalamikaji  alimtaka  mshitakiwa alipe Sh milioni 3  kwa ajili  ya fumanizi la ugoni, kiasi hicho si tu ni kikubwa, lakini pia ni adhabu.
“Kwa mujibu wa Sheria  ya Ndoa na Mirathi ya 1971,     faini  ya fumanizi la ugoni, haipaswi kuwa  adhabu  kwani inatatozwa kulinga  na mila na desturi  za mahali  husika.
“Wafipa faini ya ugoni  ni ng’ombe wawili  ambao  thamani yake ni Sh 600,000, mshitakiwa  unaamriwa na Mahakama umlipe  mara moja  mlalamikaji Sh 700,000  ikiwa ni faini ya fumanizi la ugoni,“ alisema Hakimu Mkinga.
Akizungumza nje ya chumba  cha Mahakama  mara baada  ya  kusomwa kwa  hukumu, Asteria alikiri  kuwa  hukumu iliyotolewa, ameridhika nayo. Aidha alisema amedhamiria  kufungua  shauri lingine mahakamani hapo,   kudai talaka.
“Baada  ya  hukumu hii, kesho nitaanza mchakato wa kufungua shauri  mahakamani hapa kudai talaka kwani  siko tayari  tena kuendela kuishi na Martin,“  alisisitiza.
Wakati hayo  yakijiri ndani Mahakama  hiyo, Martin alivyokuwa akijiandaa  kuingia ndani, ghafla  alizuiwa  na kuwekwa chini ya ulinzi Mahakamani  hapo.
Mwanasheria wa  Manispaa ya Sumbawanga, Tulalemwa Mwenda  alithibitisha kukamatwa kwa Martin, akituhumiwa  kujifanya  Ofisa Ardhi wa Manispaa  hiyo na  kujipatia  fedha  kwa njia ya udanganyifu.
“Tumekuwa tukimtafuta kwa muda  mrefu, sasa  leo  tumepata.  Amekuwa  akijifanya  Ofisa  wa Manipaa,  mara mhasibu na sasa  anajifanya Ofisa Ardhi na kujipatia  fedha kwa njia ya udanganyifu,“ alidai Mwenda.
Kwa mujibu wa madai ya Mwenda, Martin awali alikuwa Ofisa Mtendaji  wa Kijiji, lakini baadaye alifukuzwa kazi na kwa muda mrefu amekuwa akitapeli  wakazi  wa  manispaa  hiyo, akijifanya  kuwa Ofisa Ardhi Mwandamizi.

No comments: