KALALA JUNIOR HUYOOO TWANGA PEPETA...

Mwimbaji mashuhuri wa muziki wa dansi hapa nchini, Kalala Junior ambaye hivi majuzi ametangaza rasmi kuachana na bendi aliyoshiriki kuianzisha na kuizindua kwa mbwembwe ya Mapacha Watatu, anasemekana kuwa katika mpango kamambe wa kurejea kwenye bendi yake ya zamani ya African Stars "Twanga Pepeta".
Habari ambazo hazijathibitishwa rasmi zimedai kuwa mwimbaji huyo ambaye ni mtoto wa mkongwe wa ucharazaji gitaa la solo, Komandoo Hamza Kalala, yuko kwenye mazungumzo ambayo ni siri kubwa licha ya taarifa kwamba kila kilichojadiliwa kitawekwa hadharani hivi karibuni.
"Kalala atatangazwa rasmi kuwa kujiunga na Twanga Pepeta wakati wowote kuanzia sasa na kwamba tayari mipango inafanywa kumkabidhi kuliongoza jahazi la bendi hiyo ambayo ilitetereka katika siku za hivi karibuni baada ya kuondokewa na baadhi ya wanamuziki wake mahiri waliojiunga na bendi ya Mashujaa Musica "Wana Kibega".
Kwa mujibu wa mtoa habari huyo, inasemekana Kalala ameahidiwa donge nono ambalo linaweza kuwa rekodi katika historia ya muziki wa dansi nchini mara atakapotia wino kujiunga na Twanga Pepeta inayomilikiwa na Asha Baraka.
Aliendelea kusema kwamba hatua hiyo inachochewa na ukweli kwamba Kalala amekuwa akikubalika na wanamuziki walioko kwenye bendi hiyo kiasi cha kushinikiza chinichini kukamilishwa kwa mpango huo.
Juhudi za kumpata Kalala mwenyewe wala Asha Baraka kufafanua hili bado zinaendelea.

No comments: