AJALI YAUA WATUMISHI 7 MANYARA, WAMO MUME NA MKE

Watu saba ambao ni watumishi katika Wilaya ya Kiteto mkoani Manyara wamekufa baada ya gari walilokuwa wamepanda kugongana na gari lingine katika eneo la Pori Mamba Moja, Kata ya Partimbo Kiteto mkoani humo.
Katika ajali hiyo jana watu wengine watano walijeruhiwa na kukimbizwa katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Dodoma na wengine wanatibiwa Kiteto.
Akizungumza kuhusu ajali hiyo, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Manyara, George Katabazi alisema ilihusisha gari la wagonjwa ya Kituo cha Afya Sunya lililokuwa limepeleka mgonjwa hospitali ya Wilaya ya Kiteto kwa ajili ya matibabu.
Kamanda Katabazi alisema wakati likirudi likiwa limebeba watumishi kurejea eneo la kazi Sunya liligongana uso kwa uso na gari dogo aina ya Prado.
Alitaja majina ya waliopoteza maisha kuwa ni muuguzi, Joseph Bizuku (36), daktari Edward Makundi (47), Mkuu wa Shule ya Esamatwa, Agapiti Kimaro (32),
muuguzi Kadidi Saidi (36), mtumishi wa maabara, Celina Nyimbo 31, muuguzi Katherine Mathei (31) na daktari Nickson Mhongwa.
Waliopelekwa hospitalini Dodoma ni dereva wa Prado, Method Malick (55) na dereva wa gari ya wagonjwa ya Kiteto, Juma Mbaruku (45). Waliolazwa katika hospitali ya Kiteto ni Ibrahim Selemani (71) na Mbaraka Shabani (44).
Mapema Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Kiteto, Pascal Mbota alithibitisha kupokea miili ya watu wawili waliopoteza maisha na majeruhi 11.

No comments: