YANGA YAANZA KWA KISHINDO, YAICHAPA BDF XI MABAO 2-0

Yanga imeanza vema michuano ya Kombe la Shirikisho Afrika baada ya kuifunga BDF X1 ya Botswana mabao 2-0 katika mechi ya kwanza ya raundi ya awali ya michuano hiyo.

Matokeo hayo yanaifanya Yanga ijiweke kwenye mazingira mazuri ya kusonga mbele katika mechi ya marudiano itakayofanyika baada ya wiki mbili mjini Gaborone, Botswana.
Mchezaji wa zamani wa Simba, Amis Tambwe ndiye aliyekuwa shujaa wa Yanga baada ya kuifungia mabao yote mawili.
Tambwe alifunga bao la kwanza katika dakika kwanza ya mchezo huo kwa kichwa baada ya kuruka juu na kuuwahi mpira wa kona katikati ya mabeki wa BDF.
Katika kipindi hicho cha kwanza, BDF walionekana kucheza kwa kujilinda zaidi hali iliyomaanisha kwamba walikusudia kupata sare.
Tambwe aliipatia Yanga bao la pili katika dakika ya 56 akifunga tena kwa kichwa hatua tatu kutoka lango la BDF. Alifunga bao hilo baada ya kuunganisha pasi safi ya Mrisho Ngassa aliyewachanganya mabeki wa BDF.
Kwa ujumla Yanga ilianza mechi hiyo kwa kasi kiasi cha kuipoteza BDF XI  katika dakika 20 za kwanza kabla haijakaa sawa na kujaribu kufanya mashambulizi.
Washambuliaji wa Yanga mara kadhaa walifika langoni mwa BDF  lakini walikosa umakini na kujikuta wakipiga juu ama kupiga michomo dhaifu iliyodakwa na kipa wa wapinzani wao.
Katika dakika 20 za mwanzo BDF XI ilifanya shambulizi moja la nguvu wakati Master Mastara alipoingia eneo la hatari, lakini alipiga shuti lililopaa juu. 
Kipindi cha pili kilianza kwa Yanga kushambulia kwa kasi, huku BDF XI wakionekana kupoteza muda zaidi kwa kuhitaji matokeo yabaki kama yalivyo na hapo ndipo Tambwe alipowapachika bao la pili.
Dakika ya 64, 65 na 67 lango la BDF XI lilikuwa katika hekaheka, lakini Nadir Haroub, Andrey Coutinho na Haruna Niyonzima kwa nyakati tofauti walishindwa kutumbukiza mpira wavuni. 
Kikosi cha Yanga kilipangwa hivi: Ally Mustapha, Mbuyu Twite, Oscar Joshua, Kelvin Yondani, Nadir Haroub, Salum Telela, Simon Msuva, Haruna Niyonzima, Amissi Tambwe/Jerry Tegete, Mrisho Ngassa na Andrey  Coutinho/Kpah Sherman.

No comments: