SIMBA NA AZAM ZABANWA MBAVU, YANGA NA MTIBWA HAPATOSHI KESHO


Simba jioni ya leo ilirudia ugonjwa wake wa sare baada ya kutoka 0-0 na Coastal Union kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Mchezo wa duru la kwanza baina ya timu hizo uliofanyika Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam mwaka jana timu hizo zilifungana mabao 2-2.
Mabao ya Simba yalifungwa na Shaaban Kisiga na Amis Tambwe kipindi cha kwanza, huku yale ya Coastal Union yakifungwa na Rama Salim na Yayo Lutimba yote kipindi cha pili.
Msimu huu umekuwa si mzuri kwa Simba, ambapo imekuwa ikipata matokeo yasiyoridhisha, ingawa mchezo wa wiki iliyopita ilishinda mabao 2-1 dhidi ya JKT Ruvu Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam, hivyo kuwapa imani mashabiki kwamba wangeibuka na ushindi leo.
Kutokana na matokeo hayo Simba imefikisha pointi 17 ikiendelea kuwa nafasi ya nane, huku Coastal ikifikisha pointi 18 na inashika nafasi ya saba.
Katika mchezo huo mashabiki walishuhudia kosakosa nyingi za kila upande kwa washambuliaji kushindwa kutulia walipokaribia lango.
Simba ilipata nafasi kadhaa za kufunga, lakini washambuliaji wake, Emmanuel Okwi, Danny Sserunkuma na Elias Maguli walikosa umakini.
Nayo Coastal Union ingeweza kupata bao kama ingetumia nafasi kadhaa ilizopata, lakini washambuliaji wake wakiongozwa na Rama Salim na Hussein Sued walishikwa kigugumizi kila walipomkaribia kipa Ivo Mapunda.
Mabeki wa Coastal jana walikuwa na kazi moja tu kuwadhibiti washambuliaji Waganda wa Simba, Okwi na Sserunkuma wasilete madhara.
Katika mchezo mwingine wa ligi hiyo jioni ya leo Uwanja wa Jamhuri Morogoro, timu ya Azam ilitoka sare ya bao 2-2 na Polisi Morogoro.
Mabao ya Azam yalifungwa na Brian Majwega na Kipre Tchetche wakati yale ya Polisi yalifungwa na Cristopher Edward na Selemani Kassim.
Kwa matokeo hayo Azam imefikisha pointi 23 sawa na Yanga, lakini yenyewe ikiwa na uwiano mzuri wa mabao ya kufunga na kufungwa, hivyo kuongoza ligi hiyo.
Kabla ya mchezo wa Azam wa jana, Yanga ilikuwa ikiongoza ligi hiyo ikiwa na pointi 23 na Azam ikiwa nafasi ya pili. Timu zote sasa zimecheza mechi 12.
Matokeo ya mechi ya Simba dhidi ya Coastal Union na Azam dhidi ya Polisi ni furaha kwa mashabiki wa Yanga, ambao kama kesho Jumapili timu yao itaifunga Mtibwa Sugar itafikisha pointi 26 na kukaa tena kileleni.
Mapema wiki hii, nahodha wa Yanga, Nadir Haroub alisema dhamira yao ni kufanya vizuri huku wakiombea Simba na Azam zifanye vibaya.
Uwanja wa Nangwanda Sijaona, timu ya Ndanda FC nayo ilitoka sare ya bao 1-1 dhidi ya Stand United, huku JKT Ruvu ikifungana bao 1-1 na Mbeya City Uwanja wa Azam Chamazi.
Bao la JKT Ruvu lilifungwa na Ally Billali wakati la Mbeya City lilifungwa na Kenny Ally.

No comments: