HUKUMU KUHUSU MWILI UNAOGOMBEWA JUMATATU


Hukumu kuhusu ni familia ipi inayostahili kuuzika mwili wa mwanamke Esther Hoseya unaogombaniwa na familia mbili, itatolewa Jumatatu.

Hii ni baada ya Mahakama ya Wilaya ya Bunda kuahirisha kesi hiyo kwa kuwa wazee wa kimila wa pande hizo mbili walioitwa kutoa ushahidi kukinzana.
Kutokana na hali hiyo, Hakimu wa Mahakama ya Wilaya ya Bunda, Said Hamadi Kasonso, ameiahirisha kesi hiyo hadi kesho, ili aweze kupitia ushahidi huo na kutoa hukumu ya kesi hiyo vizuri itakayoamua familia inayostahili kuuzika mwili wa mwanamke huyo.
Mahakama hiyo juzi ililazimika kuzuia mwili wa Esther aliyefariki dunia Februari 3, mwaka huu, jijini Dar es Salaam, usizikwe na upande wowote, baada ya kutokea mgogoro wa pande mbili wa kugombania mwili huo, akiwemo baba mzazi wa mwanamke huyo.
Familia hizo mbili ni kati ya baba yake mzazi, Samwel Obinja, mkazi wa wilayani Rorya na Benard Odila mkazi wa mjini Bunda, anayedai kuwa alikuwa tayari amekwishamuoa mwanamke huyo, baada ya mume wake wa awali, Hoseya Daud, kufariki dunia mwaka 2005, jijini Dar es Salaam.
Baada ya mwanamume huyo kufariki, Odila anayedai kuwa ni mke wake, kwa sababu alikuwa akiishi naye Dar es Salaam, alijitokeza na kuchukua mwili wa marehemu na kuusafirisha hadi wilayani Bunda kwa ajili ya mazishi.
Wakati wakiandaa shughuli za kuuaga mwili wa marehemu nyumbani kwake mjini Bunda, baba wa mwanamke huyo, Obinja alikimbilia katika Mahakama ya wilaya ya Bunda na kuwasilisha hati ya dharura yenye kiapo kwa ajili ya kupinga hatua hiyo.
Kutokana na hali hiyo Hakimu Kasonso alimtuma karani wa mahakama hiyo, Nyawaye Jogo, kupeleka hati yenye hoja kumi kuzuia mazishi hayo mpaka maamuzi ya mahakama hiyo yatakapotolewa na kwamba wakikaidi amri hiyo watachukuliwa hatua za kisheria.
Hakimu Kasonso jana aliisikiliza kesi hiyo kwa kushirikisha wazee wa kimila wa kabila la Wajaluo, kwa sababu ndoa ya awali ya mwanamke huyo ilifungwa kimila mwaka 1987.
Hata hivyo, ushahidi wa kimila wa pande zote mbili uliotolewa na wazee wa kabila hilo ulipingana na ndipo hakimu Kasonso akaiahirisha kesi hiyo namba 3 ya mwaka huu, hadi kesho, ili aweze kutoa hukumu hiyo.

No comments: