POLISI WACHUNGUZWA SAKATA LA PROFESA LIPUMBA


Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora inachunguza tukio la kupigwa kwa  viongozi  na wafuasi wa Chama cha Wananchi (CUF) katika tukio la jijini Dar es Salaam juzi, kubaini kama kulikuwa na matumizi ya nguvu ya ziada ya polisi dhidi ya raia.

Hayo yalielezwa jana na Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Mathias Chikawe ambaye alisema pia ameagiza Idara ya Malalamiko ndani ya Wizara kufanya uchunguzi kuhusu matumizi ya nguvu za ziada, zichukuliwe hatua kwa watakaobainika kuhusika.
Waziri alikuwa akitoa taarifa bungeni, kabla ya wabunge kujadili hoja iliyowasilishwa juzi na Mbunge wa Kuteuliwa, James Mbatia akitaka ijadiliwe kuhusu kupigwa kwa wanachama wa CUF na matumizi ya nguvu ya ziada yaliyofanywa na polisi katika tukio hilo la  wilayani Temeke, Dar es Salaam.
“Malalamiko haya ni mazito, na Serikali haiwezi kufumbia macho… pamoja na uchunguzi unaofanywa na Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora, nimeagiza Idara ya Malalamiko ndani ya Wizara ifanye uchunguzi kuhusu matumizi ya nguvu za ziada na ikithibitika kwamba kuna polisi walitumia nguvu nyingi zaidi dhidi ya raia, basi tutachukua hatua mwafaka dhidi ya wahusika wote. Na hii ni ahadi,” alisema Chikawe.
Alisema Jeshi la Polisi halipaswi kutumia nguvu  kuliko zinazohitajika katika kukamata wahalifu wa makosa ya jinai. 
“Serikali inaomba radhi kwa wananchi wote waliokumbana na kadhia hii bila wao kujihusisha na kuwasihi wananchi kujiweka mbali na matukio yote ya uvunjifu wa sheria,” alisisitiza.
Alisema Serikali  inaendelea kuahidi kuliongoza jeshi kwa kuzingatia sheria na maudhui yake sanjari na kukabili changamoto kuhakikisha kunakuwa na usalama na utulivu nchi nzima.
Hata hivyo, alisema Polisi haitaogopa wala kumwonea haya mtu yeyote bali itaendelea kutekeleza wajibu kwa kuzingatia haki za binadamu.
Waziri Chikawe alieleza Bunge sababu za chama hicho cha siasa kuzuiwa kufanya maandamano na kusema ni baada ya Jeshi la Polisi kuona kwamba yanaweza kusababisha kuvunjika amani na kuathiri usalama wa taifa.
Kwa mujibu wa Waziri, Januari 26 mwaka huu Jeshi lilipokea barua kutoka CUF, ikitoa taarifa kuhusu kufanyika maandamano na mkutano wa hadhara Januari 27 kuadhimisha kumbukumbu ya mauaji ya wafuasi wao yaliyotokea mwaka 2001.
Alisema baada ya Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam kupokea barua, iliwaita viongozi wa CUF kwa mazungumzo na kuwafahamisha matatizo yanayoweza kutokea.
Chikawe alisema matukio ya ugaidi hususani ulipuaji mabomu katika mikusanyiko kuwa ni miongoni mwa mambo ambayo yalihofiwa kwamba yanaweza kutokea kupitia maandamano hayo.
Alisema Polisi baada ya kupokea barua ya CUF, ilikutana na viongozi wao, ikawaeleza  kwamba kufanya maandamano hayo yanayolenga kuadhimisha mauaji, pia kunaweza kusababisha chuki. Pia ilielezwa kwamba taarifa za polisi zilionesha kunaweza kufanyika vurugu.
Waziri Chikawe alieleza Bunge kwamba, kesho yake Polisi ilipata taarifa kuhusu kuwapo kwa mkusanyiko mkubwa wa watu kwenye ofisi za CUF wilaya ya Temeke.
Alisema Kaimu Kamanda, Sebastian Zakaria alikwenda na kukuta wanachama wapatao 200 wakiwa na mabango yenye maandishi mbalimbali ikiwemo, ‘Polisi na wanajeshi acheni kutumika na CCM,’; ‘tunaadhimisha kumbukumbu ya kuuawa kwa wenzetu, polisi acheni kutunyanyasa na kutumikia CCM kama vibaraka.’
Alisema Profesa Lipumba aliwasili katika ofisi hizo na alionekana kukaidi zuio na kuhamasisha wanachama kufanya maandamano kuelekea Mbagala Zakhem.
Kaimu Kamanda huyo baada ya kuona  yakiendelea kinyume na zuio, alitangaza ilani ya kutawanyika, lakini waandamanaji walikaidi.
“Ndipo akaamuru waandamanaji wakamatwe. Polisi wakatumia mabomu,” alisema Waziri.
Waziri alisisitiza kwamba polisi wanayo mamlaka kuzuia mkutano au maandamano, wakiridhika kwamba yanaweza kusababisha uvunjifu wa amani.
Alisema sheria inaruhusu mtu asiyeridhika na masharti na amri iliyotolewa, kukata rufaa kwa waziri, jambo ambalo viongozi wa CUF hawakufanya.
Alisisitiza kwamba kilichotokea  ni uvunjaji wa sheria kwa makusudi na kutafuta umaarufu wa kisiasa.
Alisema hivi karibuni, umeibuka utamaduni mbaya wa uvunjaji sheria. Alisisitiza kwamba haiwezekani watu waamue kwa makusudi kutotii maelekezo ya vyombo vya usalama.
Alihimiza viongozi bila kujali vyama, itikadi za kidini, ni wajibu wao kutii sheria za nchi na vyama vya siasa vitii sheria bila shuruti. Alisema vurugu zinapotokea hazibagui wa kumgusa kwa maana ya watoto, wazee na wagonjwa. “Na hii hutokea na si kwa makusudi,” alisema. 
Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG), George Masaju aligonga mwamba bungeni kuzuia mjadala huo kuhusu vurugu baada ya ushauri wake kutozingatiwa na badala yake, Spika Anne Makinda kuuruhusu.
Baada ya Waziri Chikawe kuwasilisha taarifa yake, Masaju alishauri Bunge lisijadili suala hilo kwa kuwa liko mahakamani.
“Jana (juzi) wakati kiti kikifanya maamuzi kutolijadili jana isipokuwa leo (jana), Lipumba alikuwa hajafikishwa mahakamani. Kwa mujibu wa taarifa ya serikali kupitia kwa Waziri, Profesa Lipumba alifikishwa mahakamani na akafunguliwa shauri la jinai,” alisema Masaju.
Alisema kwa kuwa Bunge linaongozwa kwa mujibu wa Katiba, sheria na kanuni, haliwezi kujadili jambo linalosubiri  uamuzi wa Mahakama. Alisema Mahakama ni chombo cha mwisho cha utoaji haki na wakati huo huo mihimili mitatu inapaswa ifanye kazi bila kuingiliana majukumu yake.
“Katika mazingira kama haya, ningeshauri Bunge lako tukufu lisilijadili suala hili,” alisema Masaju ambaye wabunge wa upinzani waliingilia kati na kuanza kurusha maneno ya kumpinga, jambo lililozua kelele bungeni. 
Mwanasheria huyo wa Serikali alilazimika kujitetea kwa wabunge wamwelewe kwamba ni mtetezi wa mamlaka ya Bunge, isipokuwa ushauri wake umejengwa katika msingi wa Katiba na kanuni. 
“Kwa wananchi, wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambao wana kumbukumbu na kinachoendelea hapa nchini wanafahamu juhudi kubwa nilizofanya mimi mwenyewe kama Naibu Mwanasheria Mkuu wa Serikali kutetea maslahi ya Bunge hili na mamlaka yake ilipokuwa mamlaka haya yanapingwa mahakamani lazima tuwe balanced kidogo  wabunge.
“Kwa nafasi yangu, nafasi yangu ni kuwashauri nimefanya hivyo wananchi wengine wanafahamu, naweza nikataja na hasa yale mashauri yaliyofanya Bunge hili muhimu likatekeleza wajibu wake kwa ufanisi wakati baadhi ya wananchi walitaka lisitekeleze wajibu huo. Leo mheshimiwa Spika baada ya ushauri wangu naomba kiti chako kitupatie mwongozo," alisema.
Spika Anne Makinda alisema alipoamua mjadala ufanyike jana, hakulenga kwamba Serikali iende mahakamani.  Alisema sababu ya kusubiri suala hilo lijadiliwe jana, kwa kuwa watu walikuwa hawafahamu kinachoendelea. Aliruhusu mjadala  kwa kutoa dakika tatu kwa kila mchangiaji, jambo ambalo pia lilipingwa na hivyo kulazimu atoe dakika 10.
Akihitimisha mjadala wa hoja aliyoiwasilisha bungeni juzi, Mbatia alishauri kuwepo tume ya kusimamia serikali vizuri kwa mujibu wa Katiba ili kuona namna ya kufanyia marekebisho sheria kadhaa, kusaidia Jeshi la Polisi na Serikali kwa ujumla.
Mbatia alisema Bunge linahitaji kuangalia upya sheria ya vyama vya siasa, Sheria ya Haki na Kinga za Bunge Namba 3 ya 1988 na sheria ya Polisi.
“Na wote kwa pamoja tuombe Bunge lako aidha liwe na tume, ya kuisimamia serikali vizuri kwa mujibu wa Katiba ili kuweza kuona ni namna gani sheria hizi zifanyiwe marekebisho haraka ili uchaguzi mkuu ujao uwe na amani na utulivu na tulisaidie Jeshi la Polisi, tuisaidie serikali na nchi kwa pamoja,” alisema Mbatia.
Aliongeza kuwa, vipo vitendo vya kihuni ndani ya Jeshi la Polisi jambo ambalo alitaka Mkuu wa Jeshi la Polisi, Inspekta Jenerali (IGP), Ernest Mangu arejee kwa Saidi Mwema aliyestaafu wadhifa huo kushauriwa.
Mbunge huyo alimpongeza Spika Anne Makinda kwa busara zake za kuruhusu mjadala huo na kuonya wabunge kuacha kuingiza siasa katika suala hilo, kwani wakianza kurushiana maneno, hawatakuwa wanajenga taifa.
Akizungumza baada ya mjadala huo, Spika Makinda alisema Kamati  ya Bunge ya Kanuni inatarajia kukaa kuangalia kama kanuni ziko sawa au  la. Alitoa mfano wa kanuni ya 47 iliyotumiwa kujadili suala hilo, Spika Makinda alisema suala hilo lilikuwa kubwa na halikuwa la dharura kama ambavyo kanuni inatamka.
Awali katika mjadala, wakati baadhi ya wabunge walilenga kujadili suala hilo kwa misingi ya vyama vyao, Mbunge wa Mkanyageni, Mohamed Habib Mnyaa (CUF) alionya kulichukulia kivyama.
“Ushauri wangu kwa Bunge, kwa heshima na taadhima suala hili hata kama ni kweli kwamba CCM inasaidiwa, jambo hili tusilichukulie kivyama. Najua wabunge wengine wa CCM wameshaumizwa na Jeshi hili  la Polisi,” alisema Mnyaa.
Alishauri, “Naomba Bunge suala hili tulijadili na tupate maazimio yatakayojenga Jeshi la Polisi katika utaratibu wa kistaarabu tunakokwenda tusiharibikiwe; Nia ni kujenga.”
Mnyaa ambaye alisema Jeshi la Polisi limegawanyika, alisema, “Tukiacha jeshi hili, nani anatabiri kitakachotokea katika uchaguzi ujao. Ni suala la kutofumbia macho.Yako mambo ambayo jeshi linaonekana limegawanyika. Majambazi wa nchi hii wanatokea ndani ya jeshi. Yako mambo Jeshi la Polisi lenyewe limegawanyika. Wapo badhi ya polisi wadogo hawana la kusema wala pa kukimbilia. Bunge liwe kimbilio kwa hawa wanaodhulumiwa”.
Alishutumu kwamba mbali ya kutumia nguvu, polisi ilitumia silaha zisizowajibika kutumiwa na jeshi, ikiwemo matumizi ya  spana ya kutolea tairi kupiga watu vichwani.
Mbunge wa Sikonge, Said Nkumba (CCM)  alisisitiza kwamba katika jambo lenye maslahi ya taifa, umoja wa wabunge ni jambo zuri.
“Wapo wanaotaka jambo hili liwe la maslahi ya kisiasa. Ni kweli CCM imeunda serikali na yanayofanywa na dola si yote ni ya chama,” alisema. Nkumba ambaye hata hivyo alisisitiza kwamba nchi inaongozwa kwa sheria na lazima kuwapo utii, alishauri polisi waliohusika katika matumizi ya nguvu kupita kiasi, wachukuliwe hatua.
“Hakuna mbunge wa kutetea maovu. Wanaotenganisha wabunge wa CCM na upinzani katika suala la maslahi ya taifa, watakuwa na ajenda binafsi,” alisema.
Miongoni mwa hoja zilizosababisha wabunge kugawanyika katika msingi wa kivyama, ni pamoja na iliyotaka Waziri Mkuu, Mizengo Pinda na Waziri wa Mambo ya Ndani, Mathias Chikawe, wajiuzulu na kutupia lawama moja kwa moja kwa CCM kwamba ndiyo inayotumiwa na askari kunyanyasa watu.
Mbunge wa Singida Mashariki, Tundu Lissu (Chadema) alishutumu Jeshi la Polisi akisema wapinzani wanapigwa na polisi, si kwa sababu wana makosa, bali wapo mafashisti ndani ya jeshi hilo na serikalini.
 Alisema viongozi wote wa vyama vya siasa, hakuna asiyekuwa na majeraha ya Jeshi la Polisi na hakuna ambaye hajawahi kukamatwa na kunyanyaswa. “Tuunde tume au kamati teule kuchunguza mauaji yote, polisi kujeruhi kupiga watu ili tupate ufumbuzi wa kudumu wa hili suala,” alisema Lissu.
Mbunge wa Donge, Sadifa Juma Khamis (CCM) alisema pamoja na haki ya kuandamana kuwapo, lakini hakuna haki isiyo na mipaka. “Haki ya kuandamana tusiitumie vibaya tukailaumu Polisi,” alisema Sadifa ambaye katika mjadala aliiita CUF kuwa ni Saccos, jambo ambalo Spika  Makinda aliamuru aondoe maneno hayo.
Hata hivyo, Sadifa alianza kugoma kuyaondoa akimuomba Spika amwamuru pia Lissu aondoe maneno aliyosema CCM ni mafashisti.
Kwa upande wake, Mbunge wa Muhambwe, Felix Mkosamali (NCCR-Mageuzi) alisema kinachoendelea katika jeshi hilo, kimekwishafanyiwa uchambuzi na Jumuiya ya Madola kwamba lina mifumo ya kikoloni, ambayo lengo lake ilikuwa ni kuhakikisha wakoloni wanabaki madarakani na Waafrika hawaingii madarakani.
Mbunge wa Chwaka, Yahya Kassim Issa (CCM) alihadharisha akisema si kila aliye ndani ya Serikali ni mwana CCM. Alihoji kwamba wapo askari wanaouawa lakini wabunge hawawazungumzii. “Nani atatetea askari katika Bunge hili? Wanakufa hakuna anayewatetea.”
Mbunge wa Mtera, Livingstone Lusinde (CCM) alisema ni wajibu vyama vyote kulinda amani. Alihadharisha juu ya ushauri wa kutaka viongozi kujiuzulu akisema lazima kuwa makini na wanaotoa ushauri huo vinginevyo, viongozi wote wataondolewa madarakani.

No comments: