MBEYA CITY YAITULIZA SIMBA 2-1 UWANJA WA TAIFA



Timu ya soka ya Simba ya Dar es Salaam imejikuta ikiangukia pua baada ya kuchapwa mabao 2-1 na Mbeya City katika pambano la Ligi Kuu ya Vodacom lililomalizika muda mfupi uliopita kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Katika pambano hilo lililoshuhudia mwamuzi Abdallah Kambua kutoka Shinyanga akitoa penalti mbili kila upande katika dakika za nyongeza, Simba ikitandaza soka safi iliwenda mapumziko ikiwa mbele kwa bao 1-0 lililowekwa kimiani na Ibrahim Salum Hajib dakika ya 45+2.
Bao hilo lilitokana na mpira wa adhabu ndogo umbali ya takribani mita 20 kutoka langoni mwa Mbeya City baada ya Awadh Juma kufanyiwa madhambi.
Kipindi cha pili kilianza kwa kasi huku vijana wa Mbeya City inayonolewa na Juma Mwambusi wakizinduka na kulisakama lango la wapinzani wao Simba kama nyuki na hatimaye juhudi zao zikazaa matunda katia dakika ya 77 baada ya kusawazisha bao kupitia kwa Hamad Kibopile.
Kibopile alifunga bao hilo kwa kutumia makosa yaliyofanywa na mabeki wa Simba kuchanganyana na kipa wao, Manyika Peter.
Wakati kila shabiki akiamini mechi hiyo itamalizika kwa sare, dakika ya 90+2 vijana wa Mbeya City wakapata penalti baada ya kipa wa Simba Manyika kumkamata mguu Raphael Daudi akiwa katika harakati za kufunga. Yussuf Abdallah akauweka mpira kimiani na kuiandikia timu yake bao la pili.
Kama filamu vile, dakika moja baada ya bao hilo mwamuzi akaizawadia Simba penalti ambayo hata hivyo ikashuhudia shuti la beki Nassor Masoud ‘Chollo’ likigomba mwamba wa juu na kutoka nje.
Hii ni mechi ya kwanza kwa kocha wa Simba, Goran Kopunovic kupoteza baada ya kushinda 2-0 dhidi ya Ndanda na kutoka sare ya 1-1 dhidi ya Azam.
Kwa matokeo hayo, Simba sasa inabaki na pointi zake 13 kutokana na mechi 11, huku Mbeya City ikifikisha pointi 15 kutokana na mechi 11.

No comments: