Baadhi ya Wajumbe wa Baraza la
Wawakilishi wameitaka Wizara ya Mawasiliano na Miundombinu kuweka vifaa vya
kisasa vya ukaguzi kwa abiria katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Zanzibar
na kuacha tabia ya kuwakagua abiria kwa kuwapapasa mwili.
Mwanajuma Faki Mdachi, Mwakilishi wa
Viti Maalumu kwa tiketi ya Chama cha Wananchi (CUF), akichangia bajeti hiyo
alisema anakerwa na tabia ya kupapaswa mwilini inayofanywa na wafanyakazi wa
uwanja wa ndege wakati abiria wanapoondoka nchini.
Alisema haipendezi hata kidogo kuona
abiria wanapapaswa mwilini wakati wa kufanya ukaguzi badala ya kutumia vifaa
vya kisasa kama ilivyo kwa nchi nyingine.
“Mheshimiwa Spika tunaitaka Wizara
ya Mawasiliano na Miundombinu kutafuta vifaa vya kisasa vya kufanya ukaguzi wa
abiria na mizigo na kuacha tabia ya kutupapasa mwilini...hii si tabia nzuri
hata kidogo,” alisema.
Alisema wakati mwingine mwanamume
hufanya ukaguzi kwa kuwapekua abiria wanawake kitendo ambacho hakikubaliki hata
kidogo kwani huo ni sawa na udhalilishaji wa kijinsia.
Naye Mwakilishi wa Jimbo la Chake
Chake kwa tiketi ya CUF, Omar Ali Shehe aliitaka mamlaka ya viwanja vya ndege
vya Zanzibar kutafuta vifaa vya kisasa vyenye uwezo wa kugundua vitu mbali
mbali ikiwemo madawa ya kulevya.
Alisema kwa sasa Uwanja wa Ndege wa
Kimataifa wa Abeid Amaan Karume hauna vifaa vya kisasa vya kufanya ukaguzi
ambapo wafanyakazi wake wanalazimika kuwapapasa abiria.
“Mheshimiwa Spika wakati umefika wa
kufanya mabadiliko makubwa katika viwanja vya ndege vya Zanzibar ikiwemo kuweka
vifaa vya kisasa vya kugunduwa vitu vya hatari ikiwemo madawa ya kulevya,”
alisema.
Aidha, aliitaka Wizara ya
Mawasiliano na Miundombinu ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kuufanyia
ukarabati mkubwa Uwanja wa Ndege wa Karume uliopo Pemba ambao hadi sasa hauna
taa za kuruhusu ndege kutua usiku.
Suala la Uwanja wa Ndege wa Karume
ulioko Pemba kukosa huduma za taa za kuruhusu ndege kutua usiku,wajumbe wengi
zaidi kutoka Pemba walitishia kuzuia bajeti hiyo.
“Mimi siungi mkono hadi pale
nitakapopewa maelezo lini Uwanja wa Ndege wa Karume Pemba utawekwa taa
zitakazoruhusu ndege kutua nyakati za usiku,” alisema Saleh Nassor Juma,
Mwakilishi wa Jimbo la Wawi kwa tiketi ya CUF.
Uwanja wa ndege wa Karume uliopo
Pemba hauna huduma za taa usiku ambapo ndege haziwezi kutua nyakati hizo na
hivyo kusababisha usumbufu mkubwa kwa wananchi.
No comments:
Post a Comment