SERIKALI SASA KUNUNUA MAFUTA KWA ELEKTRONIKI



Serikali itaanzisha mfumo mpya wa kielektroniki wa kununua, kutunza na kuuza mafuta yanayotumika katika magari yake. 
Hayo yalibainishwa na Waziri wa Fedha, Saada Salum Mkuya  aliposoma Hotuba ya Bajeti ya Serikali kwa mwaka 2014/15.
Alieleza kuwa ili kudhibiti matumizi na kupata thamani ya fedha katika ununuzi  wa bidhaa na huduma, serikali imeamua kuzingatia ununuzi wa pamoja (bulk procurement) kutoka kwa wazalishaji badala ya wakala, kama ilivyo sasa; na hatua imeanza kuchukuliwa ili ununuzi wa magari na vyombo vya TEHAMA ufuate utaratibu huo.
“Aidha, kutokana na wingi wa mafuta yanayotumika kwenye magari na mitambo, serikali itaanzisha mfumo mpya wa kielektroniki, utakaotumika katika kununua, kutunza na kuuza bidhaa hiyo ili kuwezesha serikali kupata thamani halisi ya fedha zinazotumika katika ununuzi wa mafuta,” alisema.
Vilevile, Waziri huyo wa Fedha aliagiza vitabu vya kumbukumbu (diaries) na kalenda za kila mwaka, kuanzia mwaka 2014/15 zitachapishwa na Ofisi ya Waziri Mkuu tu. 
“Hii ni kwa wizara, idara zinazojitegemea, wakala na taasisi za serikali, mikoa na mamlaka za serikali za mitaa, badala ya utaratibu wa sasa ambapo kila taasisi ya serikali inachapisha kwa utaratibu wake” alisema. 
Pia, alisema ili kupunguza matumizi ya umeme katika ofisi za serikali, serikali inatarajia kutumia vifaa vya umeme vyenye matumizi kidogo ya umeme (energy saving technology sensors).

No comments: