Watu sita wamekufa na wengine 12 kujeruhiwa
katika ajali, iliyohusisha magari manne kugongana.
Yaligongana katika barabara ya Bagamoyo, eneo
la njia panda ya Lugalo katika Manispaa ya Kinondoni jijini Dar es Salaam.
Ajali hiyo ilitokea jana saa 7:30 mchana
wakati daladala, linalofanya safari zake kati ya Tegeta na Makumbusho, lenye
namba za usajili T441 CKT, kuacha njia yake na kuhamia upande wa pili wa
barabara.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kinondoni, Camillius
Wambura alithibitisha kutokea kwa ajali hiyo.
Alisema daladala hilo, lililokuwa linatokea
Tegeta kwenda Makumbusho, lilipoteza mwelekeo na kuparamia tuta la barabara na
kisha kuhamia upande wa pili na kuligonga daladala lingine, aina ya Nissan Civilian lenye namba za
usajili T377 BEF, linalofanya safari zake kati ya Makumbusho na Kunduchi.
Wambura alisema watu waliokufa, watatu ni
wanaume na wengine wanawake, huku waliojeruhiwa wanaume ni wanane na wanawake
wanne. Hali zao ni mbaya na wamelazwa katika Hospitali Kuu ya Jeshi ya Lugalo.
"Baada ya daladala hilo kugonga daladala
lingine, nalo lilienda kugonga lori ambalo lilikuwa bado halina namba za
usajili, isipokuwa lina namba za chasis," alisema Kamanda Wambura.
Alisema baada ya lori hilo kugongwa, nalo lilikwenda
kuligonga gari aina ya Land Rover Discovery, lenye namba T454 AWZ, ambalo
liliharibika ubavuni.
Kamanda Wambura alisema majina ya marehemu na
majeruhi, bado hayajafahamika mpaka yatakapopelekwa ofisini kwao na watu
waliopewa kazi ya kufuatilia majina hayo.
No comments:
Post a Comment