DALADALA LAACHA NJIA NA KUUA WATU SITA, LAJERUHI ZAIDI YA 12


Watu sita wamekufa na wengine 12 kujeruhiwa katika ajali, iliyohusisha magari manne kugongana.
Yaligongana katika barabara ya Bagamoyo, eneo la njia panda ya Lugalo katika Manispaa ya Kinondoni jijini Dar es Salaam.
Ajali hiyo ilitokea jana saa 7:30 mchana wakati daladala, linalofanya safari zake kati ya Tegeta na Makumbusho, lenye namba za usajili T441 CKT, kuacha njia yake na kuhamia upande wa pili wa barabara.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kinondoni, Camillius Wambura alithibitisha kutokea kwa ajali hiyo.
Alisema daladala hilo, lililokuwa linatokea Tegeta kwenda Makumbusho, lilipoteza mwelekeo na kuparamia tuta la barabara na kisha kuhamia upande wa pili na kuligonga daladala lingine,  aina ya Nissan Civilian lenye namba za usajili T377 BEF, linalofanya safari zake kati ya Makumbusho na Kunduchi.
Wambura alisema watu waliokufa, watatu ni wanaume na wengine wanawake, huku waliojeruhiwa wanaume ni wanane na wanawake wanne. Hali zao ni mbaya na wamelazwa katika Hospitali Kuu ya Jeshi ya Lugalo.
"Baada ya daladala hilo kugonga daladala lingine, nalo lilienda kugonga lori ambalo lilikuwa bado halina namba za usajili, isipokuwa lina namba za chasis," alisema Kamanda Wambura.
Alisema baada ya lori hilo kugongwa, nalo lilikwenda kuligonga gari aina ya Land Rover Discovery, lenye namba T454 AWZ, ambalo liliharibika ubavuni.
Kamanda Wambura alisema majina ya marehemu na majeruhi, bado hayajafahamika mpaka yatakapopelekwa ofisini kwao na watu waliopewa kazi ya kufuatilia majina hayo.

No comments: