Wagonjwa wa saratani za tumbo na ini wataanza
kupatiwa matibabu katika kituo cha magonjwa hayo katika Hospitali ya Taifa
Muhimbili.
Matibabu kwa wagonjwa wenye matatizo hayo
yataanza kutolewa hospitalini hapo baada ya Makamu wa Rais, Dk Mohamed Gharib Bilal kuzindua kituo cha
Tiba, Uchunguzi na Mafunzo ya Magonjwa ya Saratani za Tumbo na Ini.
Kituo hicho ambacho kimetolewa kwa msaada wa
Chama cha Magonjwa ya Tumbo cha Munich cha Ujerumani, kupitia taasisi ya Else
Kroner-Fresenius Stiftung, kimeelezwa kuwa ni cha kwanza katika Ukanda wa Afrika
Mashariki na cha nne kwa Afrika.
Akizungumza katika uzinduzi huo, Dk Bilal
alisema kinatarajiwa kuwa msaada mkubwa kwa wagonjwa walio wengi na pia
kuipunguzia serikali gharama za kwenda kutibiwa nje ya nchi.
"Magonjwa ya mfumo wa chakula na ini ni
miongoni mwa matatizo makubwa ya kiafya yanayoikabili dunia nzima kwa sasa.
Mtindo wa maisha kama unywaji wa pombe kupindukia na uvutaji wa sigara ni sababu kubwa," alisema Dk Bilal.
Alisema kuwa ni wajibu wa hospitali hiyo,
kuhakikisha inaongeza wataalamu watakaoendesha kitu hicho, pia kuhakikisha
huduma hizo zinafikishwa mpaka mikoani na kwenye kanda nyingine ili kuwafikia
Watanzania wengi.
"Katika kusaidia kukabiliana na upungufu
wa wataalamu waliopo, serikali yangu itasaidia kufanikisha mafunzo kwa wataalamu
zaidi ndani na nje ya nchi," alisema.
Mwenyekiti wa Chama cha Madaktari wa Matibabu
ya mfumo wa Chakula cha Munich, Ujerumani, Profesa Meinhard Classen alisema
anaamini kituo hicho kitakuwa msaada mkubwa kwa Watanzania, waliokuwa
wakiteseka na magonjwa hayo.
Alisema mbali na kuwasaidia wagonjwa lakini
pia itapunguza gharama za kuwapeleka wagonjwa nchi za nje kama vile India kwa
ajili ya matibabu ya aina hiyo.
Katika ujenzi wa kituo hicho serikali
ilichangia Sh milioni 800 na chama hicho kupitia taasisi ya Stiftung ilichangia
zaidi ya Sh bilioni moja kwa ajili ya ununuzi wa vifaa vya matibabu ya kituo
hicho.
No comments:
Post a Comment