BABU SAMBEKE KUZIKWA MAKABURI YA KARANGA KESHO...

Marehemu Ereneus Sambeke 'Babu Sambeke' enzi za uhai wake.
Maziko ya aliyekuwa mfanyabiashara maarufu mjini Moshi, Ereneus  Sambeke, maarufu Babu Sambeke aliyefariki dunia kwa ajali ya ndege, yanatarajiwa kufanyika  kesho kwenye makaburi ya Karanga mjini Moshi.

Akizungumza na mwandishi jana, Mwenyekiti wa mazishi ya Sambeke, Visent Laswai, alisema mwili utasafirishwa leo kutoka katika Hospitali ya Mount Meru, Arusha na kuwasili nyumbani kwa baba yake mjini Moshi  kwa ajili ya kutoa nafasi ya kuuaga.
Laswai alisema ibada ya maziko itafanyika kwenye Kanisa Katoliki la Karanga lilipo mjini Moshi na baadaye mwili utapelekwa kwenye makaburi ya Karanga kwa ajili ya maziko.
Katika hali isiyo ya kawaida wakati Mwenyekiti wa mazishi akiendelea kuzungumza na mwandishi, ndugu wa marehemu aliyetambulika kwa jina la Suzan, alikatisha maongezi hayo kwa madai kuwa taarifa ambazo zimekuwa zikiripotiwa na vyombo vya habari zimekuwa zikisema uongo.
Suzan alisema familia yao imechoshwa na habari zinazoripotiwa, hivyo wasingependa kuona marehemu kaka yao akizungumziwa kwenye vyombo vya habari, kutokana na mambo ya uongo yaliyoandikwa.
Babu Sambeke alifariki dunia Aprili 13  saa 6:30 jioni wakati akiwa kwenye ndege aliyokuwa akiendesha mwenyewe aina ya MT 7-yenye namba 5H-QTT na kuanguka kwenye uwanja wa ndege baada ya kugonga mti.

No comments: